• HABARI MPYA

    Tuesday, April 04, 2017

    KASEJA ALIVYOWACHOMA ‘MKUKI WA MOYO’ SIMBA JUMAPILI KAITABA

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KATIKA dirisha dogo la usajili wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kulikuwa kuna tetesi za Juma Kaseja kurejeshwa Simba SC, lakini mwishowe klabu ikamsajili kipa Mghana Daniel Agyei na kumuacha Muivory Coast, Vincent Angban.
    Simba SC hawakuwahi kutamka kutaka kumsajili Kaseja na wala kipa huyo hakuwahi kutamka kutaka kurejea Msimbazi alikofanya kazi tangu 2003 hadi 2009 alipohamia Yanga kabla ya kurejea 2011 hadi 2013 alipokwenda tena Jangwani.
    Lakini Bin Zubeiry Sports – Online inajua kuna viongozi wa Simba marafiki wa Kaseja walikuwa wanampigia debe kipa huyo arejeshwe kazini Msimbazi.
    Juma Kaseja (kushoto) akifurahia na Anthony Matogolo (kulia) baada ya mchezo dhidi ya Simba Jumapili Uwanja wa Kaitaba  
    Juma Kaseja (kulia) na Matogolo wakifurahia baada ya mchezo huo
    Hapa Juma Kaseja akipongezwa na wachezaji wenzake baada ya mchezo

    Hata hivyo, mpango huo ulikwama baada ya waliopinga kipa huyo kusajiliwa kwa mara nyingine tena kushinda kwa hoja za kwamba uwezo wake umekwisha.
    Wakati huo Kaseja alikuwa kipa wa Mbeya City, timu aliyojiunga nayo mwaka jana baada ya kuondoka Yanga SC na hakutaka kurejea Nyanda za Juu Kusini, akaamua kusaini Kagera Sugar kwa kocha Mecky Mexime.
    Kaseja sasa ni kipa namba moja wa Kagera Sugar na Jumapili alisimama langoni katika mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya timu yake ya zamani, Simba SC Uwanja wa Kaitaba, Bukoba.  
    Wengi waliipa nafasi Simba kushinda mechi hiyo na haswa baada ya kuona Kaseja ndiye anayedaka wakiamini uwezo wake uliomjengea heshima miaka ya 2000 nchini umepungua na asingeweza kuwazuia akina Laudit Mavugo, Ibrahim Hajib na Shiza Kichuya kufunga.
    Lakini kwa mastaajabu ya wengi, Kaseja aliyekuwa kipa tegemeo wa timu ya taifa kuanzia mwaka 2003 hadi 2010 katika mchezo huo alidaka vizuri mno na Kagera Sugar ikaifunga 2-1 Simba SC.
    Aliokoa michomo zaidi ya minne ya hatari na akadaka shuti la ana kwa ana na beki wa Simba, Abdi Banda kutoka umbali wa mita tatu.
    Aliiongoza vyema safu ya ulinzi ya Kagera kuwadhibiti wachezaji hatari wa Simba akina Kichuya, Mavugo na Hajib na kwa ujumla akaiongoza vyema timu kucheza kwa tahadhari dhidi ya wachezaji wenye vipaji wa Wekundu wa Msimbazi kama Said Ndemla. 
    Wazi hayo yote Kaseja aliyafanya ili kuwaonyesha Simba SC kile wanachokikosa kwa sasa – wanamkosa golikipa mwenye kipaji cha zaidi ya kusimama kwenye milingoti mitatu, bali kiongozi wa timu uwanjani.
    Juma Kaseja akitembelea magoti kwa mbwembwe kupoteza muda katika mchezo wa Jumapili
    Juma Kaseja akiwa amedaka kwenye mchezo wa Jumapili
    Juma Kaseja akidondoka na mpira wake baada ya kudaka Jumapili 
    Juma Kaseja (kushoto) baada ya mechi alikwenda kumsalimia rafiki yake wa siku nyingi, Mussa Mgosi ambaye ni Meneja wa Simba

    Na wakati akiyafanya hayo yote, jukwaani walikuwepo Makamu wa Rais wa Simba, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya klabu hiyo, Zacharia Hans Poppe.
    Walikuwa jukwaa la ‘Watu muhimu sana’, kwa kifupi VIP (Very Important person), ingawa walikuwa wamenuna tu kutokana na kutofurahia kazi ya Kaseja ya kuizuia Simba kuondoka na pointi tatu.
    Kama Kaseja aliumia kwa kutorejeshwa Simba Desemba, basi Jumapili alilipa kisasi kwa kuwaumiza Simba, hususan Kaburu na Hans Poppe kwa kuiongoza Kagera Sugar kushinda 2-1.
    Kwa sababu matokeo yale yamewarudisha nyuma mno Simba katika mbio za ubingwa, sasa wakirudi nafasi ya pili na kuwapisha juu mabingwa watetezi, Yanga kwa tofauti ya pointi moja, 55-56 baada ya timu zote kucheza mechi 25.
    Na kwa kujua kabisa aliwaumiza Simba kwa matokeo yale na kuwaathiri mno katika kampeni zao za ubingwa, ndiyo maana Kaseja alikuwa mwenye furaha kubwa baada ya mchezo huo. Na kwa akili ya kawaida ndiyo maana makala hii inasema; “Kaseja alivyowachoma mkuki wa moyo Simba Jumapili Kaitaba”. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KASEJA ALIVYOWACHOMA ‘MKUKI WA MOYO’ SIMBA JUMAPILI KAITABA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top