Coastal Union; wamefungwa 3-2 Mombasa |
Na Prince Akbar
BANDARI ya Mombasa, Kenya inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza
nchini humo, jioni hii imeifunga mabao 3-2 Coastal Union ya Tanga inayoshiriki
Ligi Kuu ya Tanzania Bara, katika mchezo wa kirafiki, uliofanyika kwenye Uwanja
wa Mbarak Sports, Mombasa.
Bandari walitangulia kupata bao lililofungwa na Nahodha wao kabla
ya Nsa Job kuisawazishia Coastal Union kwa penalti pia.
Bandari wakafunga bao la pili kupitia kwa Shaaban Kenga, lakini
mshambuliaji wa zamani wa Simba, Yanga, Azam na Moro United, Nsa Job akasawazisha
tena kwa penalty na hadi mapumziko, timu hizo zilikuwa zimefungana 2-2.
Bandari ilipata bao lake la ushindi kupitia kwa Erick Okoth
na jitihada za mabingwa wa Bara 1988 kusaka bao la kusawazisha ziligonga
mwamba.
“Mchezo ulikuwa mzuri, wenye ushindani, Coastal wamerudi Tanga
baada ya mechi, sisi tunasafiri kuelekea Nairobi kwa ajili ya mechi ya Jumamosi
ya Ligi na Iron Strikers,” alisema beki wa Bandari, Mtanzania, David Naftali
alipozungumza na BIN ZUBEIRY kutoka Mombasa jioni hii.
0 comments:
Post a Comment