Wachezaji wa Coastal Union |
Na Princess
Asia
MABINGWA wa zamani wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Coastal
Union ya Tanga leo watashuka dimbani kwenye Uwanja wa Mbarak Sports kumenyana
na Bandari ya huko, inayoundwa na wachezaji kibao wa Tanzania.
David Naftali |
Beki wa Bandari inayopigania kurejea Ligi Kuu ya Kenya kutoka
Daraja la Kwanza, David Naftali ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwa simu kutoka Mombasa
kwamba wanatarajiwa mchezo huo utakuwa mzuri kwa sababu Coastal Union imesajili
vizuri na wao (Bandari) timu yao nzuri pia.
Bandari yenye nyota wengine wa Tanzania, zaidi ya Naftali kama
Meshack Abel, kiungo Mohamed Banka na mshambuliaji Thomas Maurice, kwa sasa inaongoza
ligi hiyo kwa pointi zake 44, ikifuiatiwa na Kariobang Sharks yenye pointi 40.
Coastal Union inayojivunia ufadhili wa Bin Slum na Simba Cement,
imepania kufanya vizuri msimu ujao, ili kukumbushia enzi zile ikitikisa katika
soka ya Tanzania miaka ya 1980 na 1990, kabla ‘haijafulia’.
Mfadhili Mkuu wa Coastal Union, Nassor Bin Slum aliiambia BIN
ZUBEIRY wiki iliyopita, kwamba Wagosi hao wa Kaya watakuwa tishio
katika msimu ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, kutokana na usajili
mzuri waliofanya.
Nassor ambaye pia ni mfadhili wa Villa Squad ya Kinondoni,
alisema kwamba uongozi wa Coastal ulikuwa makini na wenye utulivu wa hali ya
juu katika zoezi la usajili, kuhakikisha kwamba wanasajili wachezaji
watakaorejesha hadhi ya timu hiyo, iliyokuwa tishio siku za mwanzoni za soka ya
Tanzania.
“Mchezaji kama Razack Khalfan, huyu ni bora kabisa mwenye
kiwango cha kucheza timu ya taifa, huwezi kupata sababu kwa nini Yanga
walimuacha, ila msimu ujao watamuona. Bado kuna wanaume wengine wa shoka kibao
tumesajili, kwa kweli msimu ujao tutatisha,”alisema Nassor.
Mabingwa hao wa 1988, tayari wamekamilisha usajili wa msimu
ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara na wametaja kikosi chao, kupitia
facebook page yao.
Kikosi cha Coastal msimu kitaundwa na makipa; Juma Mpongo,
Abraham Chove na Rajab Kaumba, mabeki; Said Sued (Nahodha) Mbwana Kibacha
(Nahodha Msaidizi) Othman Omary, Juma Jabu, Ismail Suma, Jamal Machelenga,
Cyprian Lukindo na Philipp Mugenzi.
Viungo watakuwa ni Jerry Santo, Razack Khalfan, Mohamed
Binslum, Khamis Shango, Mohamed Issa, Mohamed Soud, Suleiman Kassim ‘Selembe’,
Lameck Dayton, Joseph Mahundi, Aziz Gilla na Shaffih Kaluani, wakati
washambuliaji ni Nsa Job, Atupele Green, Danny Lianga na Pius Kisambale.
Kikosi hicho kitakuwa chini ya Kocha Mkuu, mshambuliaji wake
wa zamani, Juma Mgunda, atakayekuwa akisaidiwa na beki wa zamani wa Pan
African, Habibu Kondo, kocha wa viungo, mchezaji wake wa zamani, Ally Jangalu
na kocha wa makipa Bakari Shime.
Msimu ujao, kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu, mkoa wa
Tanga utakuwa na timu mbili Ligi Kuu, zaidi ya Coastal nyingine ni Mgambo FC
iliyopanda msimu huu, hivyo kukumbushia enzi zile zile za African Sports ‘Wana
Kimanumanu’ na Wagosi hao wa Kaya.
0 comments:
Post a Comment