![]() |
| Bocoo 'Adebayor' akipoza koo baada ya kumaliza mazoezi leo. Picha kwa hisani ya Meneja wa Azam FC, Patrick 'Torres' Kahemele. |
Na Mahmoud Zubeiry
WAKATI SuperSport United inajiandaa na mechi ya kwanza ya Nusu
Fainali ya MTN8 Jumapili dhidi ya Orlando Pirates kwenye Uwanja wa Peter Mokaba,
mshambuliaji wa kimataifa wa Tanzania, John Raphael Bocco ‘Adebayor’ amekuwa
akiipa changamoto nzuri safu ya ulinzi ya timu hiyo.
Bocco yupo kwenye majaribio Super Sport tangu Jumamosi na
anaendelea na mazoezi na timu hiyo, akiipa mikiki ya kutosha safu ya ulinzi ya
timu hiyo kanla ya kuivaa Pirates.
Tayari wakala wa mshambuliaji huyo wa Azam FC, Yussuf Bakhresa
amesema hataweka tamaa ya fedha iwapo mchezaji huyo atafuzu.
Yussuf anayetambuliwa na Shirikisho la Soka la Kimataifa
(FIFA), ambaye awali miaka mitatu iliyopita alimpeleka Israel Adebayor huyo wa
Chamaz kwa majaribio na akafanya vizuri, alisema kwamba anachojali ni mchezaji
huyo kupata timu itakayompa maslahi bora na kumuendeleza zaidi kisoka.
“Mimi nataka klabu inayotaka kumnunua iilipe tu klabu yake,
mimi sitataka hata senti moja yao, kwa sababu najua wachezaji wa Tanzania bado
hawajakubalika sana katika soko la soka ya kulipwa, hivyo kufanya tamaa
kunaweza kusababisha umharibie mchezaji mwenyewe wakati mwingine,”alisema
Yussuf, ambaye mwaka 2009 alimpeleka Mrisho Ngassa majaribio West Ham United.
Super Sport ilivutiwa na soka ya Bocco, katika michuano ya
Klabu Bingwa ya soka Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame, mwezi uliopita,
hivyo kumuita kwa majaribio, ambayo akifuzu ataweka historia ya kuwa mchezaji
wa pili wa Tanzania kuchezea klabu hiyo, baada ya Suleiman Matola 2005 hadi
2007, akitokea Simba SC.
Katika Kombe la Kagame, Bocco ambaye ataondoka Jumamosi
kwenda kujaribiwa, alifunga mabao matano na kushika nafasi ya tatu katika
wafungaji bora, nyuma ya Hamisi Kiiza na Said Bahanuzi wa Yanga, aliyeibuka
mfungaji bora.
Lakini Bocco pia alikuwa mfungaji bora wa Ligi Kuu ya
Vodacom Tanzania Bara msimu uliopita, kwa mabao yake 18 akiwapiku hadi
washambuliaji wa kigeni waliocheza ligi hiyo msimu huo, Emmanuel Okwi, Kenneth
Asamoah, Davies Mwape na Dalington Enyiana.
Tangu aipandishe Ligi Kuu Azam FC msimu wa 2008/2009 kwa
mabao yake, akiibuka mfungaji bora wa Ligi Daraja la Kwanza, Bocco amekuwa
akiingia kwenye mbio za kuwania kiatu cha dhahabu cha Ligi Kuu, msimu wa kwanza
akizidiwa na Boniphace Ambani aliyekuwa Yanga, msimu wa pili Mussa Mgosi
aliyekuwa Simba na msimu wa tatu na Mrisho Ngassa, kabla ya msimu uliopita
kutimiza ndoto zake za kuwa mfungaji bora wa ligi hiyo.



.png)
0 comments:
Post a Comment