KAMATI ya
Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania katika kikao chake cha juzi jioni ilifikia uamuzi
wa kuipokonya klabu ya Yanga pointi tatu kwa kile ilichokiita kosa kumtumia beki
Nadir Haroub Ally ‘Cannavaro’ katika mechi ya ligi hiyo dhidi Coastal Union ya
Tanga, Jumamosi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Coastal
ilikata rufaa baada ya kufungwa 1-0 na Yanga Jumamosi Uwanja wa Mkwakwani,
Tanga ikipinga klabu hiyo kumtumia Cannavaro ambaye inadai alikuwa hajamaliza
adhabu yake ya kukosa mechi tatu baada ya kupewa kadi nyekundu kwa vurugu
kwenye mechi dhidi ya Azam FC
Ikumbukwe
mwishoni mwa wiki iliyopita, Mwenyekiti wa Kamati ya Nidhamu na Usuluhishi ya Shirikisho
la Soka Tanzania (TFF), Kamanda Mstaafu wa Jeshi la Polisi, Kanda Maalum Dar es
Salaam, Alfred Tibaigana alisitisha adhabu zote zilizotolewa na Kamati ya Ligi,
kuwafungia wachezaji watano wa Yanga kwa kufanya fujo kwenye mechi na Azam FC,
ikiwemo kumpiga refa.
Awali, Kamati
ya Ligi iliyokutana Machi 12, mwaka huu iliwafungia wachezaji watano wa Yanga
kwa tuhuma za utovu wa nidhamu walioufanya kwenye mechi ya Azam FC, Machi 10,
mwaka huu, Uwanja wa Taifa.
Iliyowafungia
ni mabeki Stefano Mwasyika aliyempiga ngumi refa Israel Nkongo mwaka mmoja na
faini ya Sh Milioni 1, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ mechi sita na faini ya Sh.
500,000, viungo Nurdin Bakari mechi tatu na faini Sh. 500,000 sawa na Omega
Seme na mshambuliaji Jerry Tegete.
Lakini
Kamati ya Tibaigana ikawaachia huru wachezji hao baada ya kuridhika na utetezi
wa klabu hiyo juu ya adhabu hizo.
Akitangaza
kusitisha adhabu hiyo, Tibaigana alisema kwa mujibu wa taratibu za TFF, Kamati
ya Ligi haina mamlaka ya kumfungia mchezaji yeyote wala kutoa adhabu, isipokuwa
Kamati ya Nidhamu.
Baada ya
kufuta adhabu zote akidai kwamba Kamati ya Ligi haina mamlaka ya kutoa adhabu,
ispokuwa Kamati yake, Tibaigana alipanga kukutana na Wajumbe wenzake wa Kamati
hiyo jana kujadili suala hilo.
Lakini ajabu
juzi, Kamati ya Ligi Kuu imekutana tena na kupitia rufaa ya Coastal Union na
kuamua kuiopokonya Yanga pointi, jambo ambalo dhahiri haliko sahihi na yeyote
hawezi kusita kusema kamati hiyo haikutumia busara kukutana juzi kabla ya
Kamati ya Tibaigana kukutana jana.
Kukutana
kwao juzi ni kama kutaka kuzidi kuleta vurugu na kulifanya suala hili liwe
kubwa, bila sababu za msingi.
KAMATI YA
LIGI DHIDI YANGA:
Binafasi
nina shaka na Kamati hii ya Ligi Kuu kama inaweza kuitendea haki Yanga katika
suala hili kwa ujumla, kutokana na Wajumbe waliomo kwenye kamati hiyo.
Mwenyekiti
ni Wallace Karia huyu ni mtu ambaye Coastal Union ndio imempa tiketi ya kuingia
ndani ya TFF, Makamu Mwenyekiti wake ni Said Mohamed kutoka Azam FC, Wajumbe
wengine ni pamoja Damas Ndumbaro ambaye
ni mpenzi wa Simba, Geoffrey Nyange huyu ni Makamu Mwenyekiti wa Simba SC na
kwenye vikao vingi vya Kamati hiyo yeye ndiye huwa mwenye sauti.
Hao ni
baadhi tu ya Wajumbe, wengine ni Steven Mnguto, Seif Ahmed, Henry Kabera, ACP
Ahmed Msangi, Meja Charles Mbuge na Ahmed Yahya.
Kwa
kuzingatia kuwa Yanga inasaka pointi za kutetea ubingwa wake na wapinzani wake
wakuu ni Simba SC na Azam, Kamati yenye wajumbe kutoka klabu hizo dhahiri
inaweza kufanya chochote kumuangamiza mpinzani wao.
Lakini hata
isifanye hivyo, kwa mgongano wa kimaslahi tu, Mzee Said (Azam), Karia Coastal
iliyocheza na Yanga na kufungwa hadi kukata rufaa, Kaburu na Ndumbaro wa Simba,
pekee wanaipa hoja Yanga kupinga maamuzi yoyote ya Kamati ya Ligi.
Ndiyo, Azam
na Simba wanashindana nao katika mbio za ubingwa na nafasi ya pili, ambazo
hutoa fursa kwa timu kushiriki michuano ya Afrika wakati Coastal ndio ambao
waliwafunga, wakakata rufaa.
Na ukitazama
namna ambavyo Kamati hii imekuwa ikikutana haraka sana kujadili masuala
yanayoihusu Yanga kuanzia lile la Azam na hili la Coastal, tofauti na
ilivyozoeleka katika soka ya nchi hii, wazi unapata wasiwasi juu yake.
Ni kama kuna
ajenda fulani, ambayo inawezekana baadhi ya Wajumbe hawaijui na wanakokotwa tu,
lakini hadi kufikia wengine kutotaka kufuata taratibu na kutishia kujiuzulu
kulinda maamuzi yao, hakika inatia shaka kama ndani ya Kamati hiyo Yanga
inaweza kutendewa haki.
Kimsingi TFF
ilikosea katika kuunda Kamati hii, kwa kuweka viongozi wa juu wa Azam na Simba
na Yanga wakamteua Mjumbe tu wa Kamati ya Utendaji, Seif ambaye tena ni wa
kuteuliwa si wa kupigiwa kura na wanachama.
Yanga kama
bingwa wa nchi, hata katika uundwaji wa Kampuni ya Ligi Kuu kama ingeanza
kufanya kazi mwaka huu, maana yake Mwenyekiti wake ndiye angekuwa Mwenyekiti wa
Kampuni hiyo, ila kwa sababu ambazo huwezi kujua sababu zake, Yanga haina
uwakilishi wa nguvu kwenye Kamati ya Ligi Kuu.
SUALA LA
CANNAVARO
Na kwa
sababu haina uwakilishi wa nguvu kwenye Kamati ya Ligi, ndiyo maana adhabu
zilizotolewa kwa wachezaji wao zilikuwa kali mno, kwa mfano ya Cannavaro tofauti
na uzito wa kosa lake.
Watu
wanajifanya wataalamu wa kutafsiri kanuni na wanatumia fursa hiyo kupotosha mno
umma wa wapenda soka nchini hii, hususan katika suala la Cannavaro.
Refa Nkongo
alikiri hadharani kwamba Cannavaro hakupiga ngumi, bali ni Mwasyika ambaye naye
mchezaji huyo alikiri na sasa anahaha kuomba radhi hadi Chama cha Marefa ili
apunguziwe adhabu.
Lakini ajabu
wanasema Cannavaro kwa kuwa alimkimbilia refa kwa kasi na alipomkaribia
akazuiwa na wachezaji wenzake, alitaka kupiga naye anastahili kupewa adhabu
sawa na mtu aliyepiga.
Ndumbaro ni
Mwanasheria Kitaalamu, anataka kuwaambia wapenzi wa soka kwamba anayeua na
anayetaka kuua wanapewa hukumu sawa? Iweje hivyo wakati katika sheria hizo hizo
kuna kipengele cha muuwaji ambaye hakukusudia?
Bila kuzuiwa
na mtu yeyote, Cannavaro inawezekana alikuwa anatishia kwa sababu hata katika
sheria watu wanahukumiwa kwa kutishia tu. Lakini bado hukumu ya mtu aliyetishia
na aliyetekeleza zipo tofauti.
Cannavaro
hakupiga refa, anaishia kwenye kutishia na kwa sababu hiyo adhabu yake lazima
iendane na uzito wa kosa lake na kwa sababu kanuni zipo wazi, ndio maana inatia
shaka mno juu ya Kamati hiyo ya Ligi dhidi ya Yanga.
VITA YA
UBINGWA LIGI KUU:
Azam, Simba
au Yanga yeyote anaweza akawa bingwa msimu huu na yeyote anaweza kuwa wa pili
na wa tatu mwishoni mwa msimu.
Simba
inaongoza Ligi Kuu kwa pointi zake 50 baada ya kucheza mechi 22, Azam FC ni ya
pili kwa pointi zake 47 baada ya kucheza mechi 22 pia na Yanga iliyocheza mechi
21 ni ya tatu kwa pointi zake 46, bila kutoa zile zilizokatwa na Kamati ya Ligi
juzi.
Kumekuwa
kuna tuhuma za muda mrefu kuhusu hujuma na upangaji matokeo katika Ligi Kuu ya
Bara ambazo inasikitisha TFF haijazifanyia kazi kwa muda mrefu sasa, ingawa ni
kazi nyepesi tu baada ya vyanzo vya ushahidi kupatikana.
Katika
dakika kama hizi ligi inaelekea ukingoni ndipo sasa mapambano ya kile wanachokiita
wenyewe ‘fitina’ yanakuwa mazito- sasa iwapo TFF (Kamati ya Utendaji) haitakuwa
makini, ligi itaingia doa.
MUSTAKABALI
WA KAMPUNI:
Klabu za
Ligi Kuu zimekuwa katika harakati za kuanzisha Kampuni ya kuendesha Ligi Kuu
badala ya ilivyo sasa ligi hiyo kuendeshwa na TFF.
Hakuna shaka
wengi wanajua mimi ni muumini wa kampuni na nimekuwa nikiunga mkono jitihada
hizo. Lakini sasa kwa mwenendo wa Kamati tu ya Ligi, ambayo inaundwa na
viongozi wa klabu hizo hizo za Ligi Kuu kuonekana kuna dalili za ubinafsi ndani
yake napata shaka hata juu ya huo mustakabali wa kampuni.
Kampuni
safi, ipo dunia nzima. Lakini kwa kuwa wajumbe wa Kamati ya Ligi Kuu ndio hao
hao viongozi walio kwenye harakati za uundwaji wa Kampuni. Na kuwa kuwa
tumekwishasoma picha yao kupitia maamuzi yao dhidi ya Yanga, hakika inatia
shaka hata juu ya mustakabali mzima wa hiyo kampuni.
HITIMISHO:
Kamati ya
Ligi Kuu haikustahili kukutana juzi, ikiwa jana Kamati ya Tibaigana ilipanga
kukutana- lakini yote kwa yote kuna dalili za kutosha, Kamati hiyo haiwezi
kuitendea haki Yanga kwa sababu za kimgongano wa maslahi. Nawasilisha.
Alamsiki.



.png)
0 comments:
Post a Comment