• HABARI MPYA

    Tuesday, April 04, 2017

    MBARAKA YUSSUF ABEID MCHEZAJI BORA WA LIGI MACHI 2017

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI chipukizi wa kimataifa wa Tanzania, Mbaraka Yussuf Abeid wa Kagera Sugar FC ya Bukoba amechaguliwa kuwa mchezaji bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kwa mwezi Machi kwa msimu wa 2016/2017.
    Mbaraka amewashinda wachezaji Salum Abubakar ‘Sure Boy’ wa Azam FC na Kenny Ally wa Mbeya City kutokana na kuonyesha kiwango cha hali ya juu, hivyo kuisadia timu yake kupata matokeo mazuri.
    Katika mwezi huo ilichezwa raundi moja tu na Mbaraka ambaye alicheza kwa dakika zote 90 aliisaidia timu yake kukusanya pointi zote tatu zilizoifanya timu yake kubaki katika nafasi ya nne (4) katika msimamo wa ligi kwa mwezi huo.
    Mbaraka Yussuf akimtoka kiungo wa Simba, Muzamil Yassin Jumapili Uwanja wa Kaitaba
    Katika mchezo huo mmoja, Mshambuliaji huyo alifunga goli moja, na alionyesha nidhamu ya hali ya juu, hivyo kutopata onyo lolote la kadi.
    Kwa kushinda tuzo hiyo, Mbaraka atazawadiwa kitita cha sh. 1,000,000 (milioni moja) kutoka kwa wadhamini wa Ligi hiyo, kampuni ya Vodacom Tanzania PLC.
    Ushindi huo ni mwendelezo wa furaha kwa chipukizi huyo, baada ya wiki iliyopita kuifungia Tanzania, Taifa Stars bao la ushindi ikiilaza 2-1 Burundi na Jumapili kuifungia bao la kwanza Kagera Sugar ikiilaza 2-1 timu yake ya zamani, Simba SC. 
    Na hii inakuwa mara ya pili ndani ya miezi mitatu Kagera Sugar kutoa mchezaji Bora wa Ligi Kuu, baada ya kipa wake, Juma Kaseja kuwa mchezaji Bora wa Januari. 
    Na kwa ujumla Tuzo ya Mchezaji Bora VPL inabaki Kanda ya Ziwa kwa mwezi wa tatu mfululizo, baada ya Hassan Kabunda wa Mwadui FC ya Shinyanga kuwa mchezaji Bora wa Februari.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MBARAKA YUSSUF ABEID MCHEZAJI BORA WA LIGI MACHI 2017 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top