![]() |
| Mtakatifu Tom kushoto, akiwa na BIN ZUBEIRY |
Na Mahmoud Zubeiry
KOCHA wa Yanga, Mbelgiji
Tom Saintfiet amesema kwamba mshambuliaji wake Said Bahanuzi ‘Spider Man’
aliumia goti akiwa na timu ya soka taifa ya Tanzania, Taifa Stars, lakini
anasikitika si kocha wa timu hiyo, Mdenmark, Kim Poulsen wala kiongozi yeyote
wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), aliyeipa taarifa klabu hiyo juu ya tatizo
la mchezaji huyo.
![]() |
| Bahanuzi 'Sp;ider Man' |
Mtakatifu Tom amesema
kwamba anasikitishwa mno na hilo, kwani ni kinyume cha utaratibu. “TFF
walipaswa kusema baada ya mchezaji kurudi klabuni kwamba ana matatizo haya,
lakini hawajasema kitu hadi leo, imenisikitisha sana,”alisema Tom.
Yanga jana ilicheza mechi
ya kirafiki dhidi ya African Lyon bila kinara wake huyo wa mabao na kuibuka na ushindi wa mabao 4-0 Uwanja wa
Taifa, Dar es Salaam.
Yanga ilitumia mchezo
huo kuwapima wachezaji wake kabla ya kuanza kwa Ligi Kuu na haukuwa mwanzo
mbaya, timu ikicheza kwa utulivu na hata kuhimili vishindo vya wapinzani.
Didier Kavumbangu,
mshambuliaji mpya wa klabu hiyo aliyesajiliwa kutoka Atletico Olympique ya
Burundi, alikuwa wa kwanza kuwainua vitini mashabiki wa Yanga dakika ya sita baada
ya kupiga mpira uliombabatiza beki wa Lyon na badaye kumgonga kipa na kuingia
nyavuni.
Hadi mapumziko, Yanga
walikuwa mbele kwa bao hilo 1-0 na kipindi cha pili, Haruna Niyonzima
aliifungia Yanga bao la pili kwa penalti dakika ya 57, baada ya Simon Msuva
kuchezewa rafu na Semmy Kessy kwenye eneo la hatari.
Frank Damayo aliyeingia
kuchukua nafasi ya Athumani Iddi ‘Chuji’ kipindi cha pili alitoa pasi nzuri kwa
Simon Msuva ambaye aliifungia Yanga bao la tatu dakika ya 72, kabla ya Jerry
Tegete kufunga la nne dakika ya 90+1.
Baada ya mchezo huu,
Yanga ambao ni mabingwa wa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame
inatarajiwa kuondoka Dar es Salaam leo sa 10:00 jioni kwenda Kigali, Rwanda
ambako itaweka kambi ya wiki mbili kujiandaa na Ligi Kuu.
Ikiwa
huko, Yanga itacheza mechi kadhaa za kujipima nguvu na vigogo wa Rwanda, kama
APR, Rayon, Atracao na Polisi kabla ya kurejea Dar ves Salaam kuanza maandalizi
ya Ligi Kuu.




.png)
0 comments:
Post a Comment