• HABARI MPYA

    Monday, August 20, 2012

    MBUYU TWITE AKWAMA KUJA DAR, HAYUMO KIKOSINI YANGA LEO

    Twite kulia akikabidhiwa jezi na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Yanga, Abdallah Bin Kleb

    Na Mahmoud Zubeiry
    BEKI wa kimataifa wa Rwanda, Mbuyu Twite mwenye asili ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), hatacheza mechi ya leo ya kirafiki kati ya timu yake mpya, Yanga dhidi ya African Lyon Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, kwa sababu ameshindwa kuwasili nchini.
    Na sasa kama ambavyo BIN ZUBEIRY iliwahi kuandika awali, beki huyo atajiunga na Yanga ikiwa Kigali, Rwanda kwenye kambi fupi ya kujiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Habari za ndani kutoka Yanga, zimesema kwamba tayari Twite amekwishazungumza hadi na kocha Mkuu wa klabu, Mbelgiji Tom Saintfiet kumjulisha juu ya hilo. Kwa sasa, Mbuyu yupo nyumbani kwao kwa asili, DRC kwa mapumziko mafupi kabla ya kuja kuanza maisha mapya Jangwani.
    Katika mchezo wa leo, Yanga pia itamkosa mfungaji bora wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Said Bahanuzi ‘Spider Man’, ambaye anasumbuliwa na maumivu ya goti.
    Meneja wa Yanga, Hafidh Suleiman aliiambia BIN ZUBEIRY mapema leo kwamba, Bahanuzi anasumbuliwa na maumivu ya goti na leo atamuona daktari wa klabu, Dk Sufiani Juma kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
    Saa mbili zijazo, Yanga SC itashuka dimbani Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, kumenyana na African Lyon katika mechi ya kirafiki, huo ukiwa mchezo wa kwanza wa kirafiki kwa Yanga, tangu itwae ubingwa wa Kombe la Kagame mwezi uliopita na kwa wakati huo imekuwa ikijifua tu kwenye Uwanja wa sekondari ya Loyola, Mabibo, Dar es Salaam.
    Pamoja na kukosekana kwa Twite na Bahanuzi, lakini mashabiki wa Yanga leo watapata fursa ya kumshuhudia kwa mara ya kwanza, mshambuliaji Didier Kavumbangu waliyemsajili kutoka Atletico Olimpique ya Burundi akiichezea timu yao.
    Kavumbangu ndiye aliyewafunga Yanga mabao yote mawili, walipomenyana na timu hiyo ya Burundi na kulala 2-0 na kwa kuwa mfungaji bora wa Kagame, Said Bahanuzi ‘Spider Man’ ni mgonjwa, Didier lazima ataanza.
    Tayari Yanga imewasilisha usajili wake Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), hivyo kocha Tom Saintfiet raia wa Ubelgiji anaweza kumpanga yeyote atakaye.
    Kikosi kamili cha Yanga ni; Makipa; Yaw Berko, Ally Mustafa ‘Barthez’ na Said Mohamed.
    Mabeki; Shadrack Nsajigwa (Nahodha), Godfrey Taita, Juma Abdul, Oscar Joshua, David Luhende na Stephano Mwasika, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Mbuyu Twite, Ibrahim Job na Ladislaus Mbogo.
    Viungo; Athuman Idd ‘Chuji’, Juma Seif ‘Kijiko’ na Salum Telela, Nizar Khalfan, Shamte Ally, Idrisa Rashid, Omega Seme, Haruna Niyonzima, Rashid Gumbo na Nurdin Bakari.
    Washambuliaji; Said Bhanaunzi ‘Spider Man’, Hamisi Kiiza ‘Diego’, Didier Kavambagu na Jerry Tegete.
    Kiungo Frank Domayo na mshambuliaji Simon Msuva, wanaendelea kukomazwa katika kikosi cha kwanza, wakitokea kikosi cha pili. Awali Yanga ilikuwa icheze na Coastal Union, lakini mechi hiyo imefutwa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MBUYU TWITE AKWAMA KUJA DAR, HAYUMO KIKOSINI YANGA LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top