• HABARI MPYA

    Monday, June 20, 2016

    NGASSA: KWA SOKA ILE, YANGA WATAFIKA MBALI KOMBE LA SHIRIKISHO

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa Free State Stars ya Afrika Kusini, Mrisho Khalfan Ngassa amesema kwamba kwa soka waliyocheza Yanga jana dhidi ya Mouloudia Olympique Bejaia ya Algeria, wanaweza kufika mbali katika Kombe la Shirikisho mwaka huu.
    Yanga SC usiku wa jana imeanza vibaya mechi za Kundi A Kombe la Shirikisho Afrika, baada ya kufungwa bao 1-0 wenyeji Mouloudia Olympique Bejaia Uwanja wa Unite Maghrebine mjini Bejaia usiku huu.
    Na Ngassa amesema pamoja na kufungwa, timu yake hiyo ya zamani ilicheza vizuri na lolote lingeweza kutokea kabla ya filimbi ya mwisho.
    Mrisho Ngassa (katikati) akiwa na Juma Abdul (kulia) na Simon Msuva (kushoto)

    "Walicheza vizuri, walifungwa bao la kimchezo, walitengeneza nafasi, bahati mbaya wakashindwa kuzitumia, waliendelea kutafuta bao hadi dakika ya mwisho, wamecheza mpira wa matumaini kabisa,"amesema Ngassa ambaye kwa sasa yupo mapumzikoni nyumbani.
    Baada ya mchezo huo, Yanga wanarejea kambini Uturuki na watarejea Dar es Salaam siku mbili kabla ya kumenyana na mabingwa mara tano wa Afrika, TP Mazembe Juni 28 katika mchezo wake wa pili wa Kundi A.
    Na katika mchezo huo, Shirikisho la Soka Afrika (CAF) limechanganya marefa kutoka nchi tatu tofauti, ambao ni Janny Sikazwe wa Zambia atakayepuliza filimbi, akisaidiwa na washika vibendera Jerson Emiliano Dos Santos wa Angola na Berhe O'michael wa Eritrea.
    Mchezo dhidi ya Mazembe iliyoifunga 3-1 Medeama jana mjini Lubumbashi unatarajiwa kuwa mkali kutokana na Yanga kutaka ushindi wa kwanza nyumbani dhidi ya timu ngumu kufungika.
    Yanga jana ilimaliza pungufu mchezo huo baada ya beki wake wa kushoto, Mwinyi Hajji Mngwali kuonyeshwa kwa kadi ya pili ya njano na kutolewa kwa kadi nyekundu dakika ya 90. 
    Na Mwinyi alitolewa baada ya kuingia kuchukua nafasi ya Oscar Joshua kipindi cha kwanza.
    Shujaa wa MO Bejaia alikuwa ni beki Yassine Salhi aliyefunga bao hilo pekee dakika ya 20, akimalizia kazi nzuri ya mshambuliaji Ismail Belkacemi. 
    Matokeo hayo yanaifanya MO Bejaia ishike nafasi ya pili katika kundi hilo, nyuma ya TP Mazembe ambayo iliifunga Medeama ya Ghana 3-1 katika mchezo wa kwanza mjiji Lubumbashi Jumapili, wakati Yanga inashika nafasi ya tatu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NGASSA: KWA SOKA ILE, YANGA WATAFIKA MBALI KOMBE LA SHIRIKISHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top