• HABARI MPYA

    Wednesday, June 08, 2016

    HANS POPPE: HATUBABAISHWI NA USAJILI WA KAMPENI ZA MANJI YANGA

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    MWENYEKITI wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe amesema kwamba hawababaishwi na usajili unaofanywa na mahasimu wao, Yanga hivi sasa ambao ni kwa ajili ya kampeni za uchaguzi wa klabu hiyo Juni 11, mwaka huu.
    Akizungumza na BIN ZUBEIRY SPORTS – ONLINE jana kutoka Harare, Zimbabwe ambako amekwenda kusaka wachezaji, Poppe amesema Mwenyekiti wa Yanga, Yussuf Manji anasajili ili kuwafurahisha wanachama wa klabu hiyo wampigie kura Juni 11 katika uchaguzi na hasajili kwa mahitaji ya timu.

    Hans Poppe amesema Simba hawababaishwi na usajili za Manji Yanga

    “Mimi sioni kama ni usajili wenye tija kwa timu yao, ni usajili kwa ajili ya Mwenyekiti kujipigia debe kwa wanachama wamchague tena. Wanasajili wachezaji ambao dirisha dogo watawafukuza au kuwatoa kwa mkopo,”amesema Hans Poppe.
    Kapteni huyo wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) amesema kwamba wao (Simba) wamegawana majukumu na sasa wanahaha kutafuta wachezaji wa kiwango cha juu kwa ajili ya kusajili.
    Poppe amewataka wanachama na wapenzi wa Simba wawe wenye subira, wakati viongozi wao wanahangaika kujenga timu itakayorejesha heshima msimu ujao.
    Na Poppe pia akasema hadi sasa Yanga haijamfikia mchezaji yeyote ambaye anatakiwa na Simba. “Wachezaji ambao tunawahitaji wote wako salama, wakati ukifika tutaanza kuwatambulisha,”amesema. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HANS POPPE: HATUBABAISHWI NA USAJILI WA KAMPENI ZA MANJI YANGA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top