• HABARI MPYA

    Sunday, August 19, 2012

    UKUTA MZIMA SIMBA WAPANDISHWA A

    Kikosi cha Simba B, mabingwa wa BankABC Supe8R

    Na Prince Akbar
    SAFU yote ya ulinzi ya Simba B, kuanzia kipa Abuu Hashimu na mabeki wake, William Lucian ‘Gallas, Omary Salum, Hassan Isihaka na Hassan Hatibu inapandishwa kikosi cha kwanza, ili kukomazwa, BIN ZUBEIRY imeambiwa.
    Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe aliiambia BIN ZUBEIRY juzi kwamba, mradi mzuri wa soka ya vijana unaelekea kuipunguzia gharama za kusajili klabu hiyo.
    “Karibu safu yote ya ulinzi ile ya Simba B, kocha anavutiwa nayo na katika mipango yake atakuwa anawatumia hao wachezaji katika timu A. Na kama kuna kitu ambacho Simba itajivunia baadaye, basi ni wale mabeki wawili wa kati, akina Hassan,”alisema Hans Poppe.
    Lakini tayari Kocha Mkuu wa Simba SC, Milovan Cirkovick amewapandisha katika kikosi cha kwanza chipukizi wengine wa Simba B, Jonas Mkude, Edward Christopher na Ramadhan Singano ‘Messi’.
    Nyota saba kati ya hao wanane, ukimuondoa Mkude, jana aliiongoza Simba B kutwaa ubingwa wa michuano mipya, BankABC Sup8R jioni ya leo, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, baada ya kuifunga Mtibwa Sugar ya Morogoro mabao 4-3, katika mchezo uliodumu kwa dakika 120.
    Shujaa wa Simba hivi jana alikuwa ni Christopher Edward ambaye alifunga mabao matatu peke yake na kufikisha jumla ya mabao tisa, hivyo kujinyakulia tuzo ya ufungaji bora wa michuano hiyo na kuzawadiwa Sh. Milioni 2.  
    Hadi mapumziko, timu hizo zilikuwa zimekwishafungana bao 1-1, Simba iliyotumia kikosi chake cha pili kwenye michuano hiyo, Simba B ikitangulia kupata bao dakika ya 13, mfungaji Christopher Edward aliyepokea pasi safi ya Ramadhan Singano ‘Messi’.
    Mtibwa walisawazisha bao hilo kwa penalti dakika ya 32, mfungaji Shaaban Kisiga ‘Malone’, baada ya Jamal Mnyate kuangushwa kwenye eneo la hatari na Hassan Hatibu.
    Mnyate hakuweza kuendelea na mchezo baada ya pigo hilo na nafasi yake ikachukuliwa na Hassan Seif.
    Kipindi cha pili, Simba inayofundishwa na Suleiman Matola, ilirudi kwa kasi tena na kufanikiwa kupata bao la pili dakika ya 54, Edward akiunganisha krosi maridhawa ya Rashid Ismail.
    Dakika ya 57 Mtibwa Sugar walisawazisha bao hilo kwa mpira wa adhabu nje kidogo ya eneo la penalti, ambalo lilipigwa na Shaaban Kisiga ‘Malone’ na kumpita kipa Abuu Hashim, aliyepewa tuzo ya Mchezaji Bora wa Mashindano (MVP) na kuzawadiwa Sh. Milioni 2.5. 
    Simba ilipata bao la tatu dakika ya 66, safari hii akifunga Haroun Athumani, kabla ya Hassan Seif kuisawazishia Mtibwa dakika ya 79 kwa mpira wa adhabu tena, uliompita kirahisi kipa mfupi Abuu.
    Hadi dakika 90 za mchezo huo zinamalizika, timu zote zilikuwa zimefungana mabao 3-3 na katika dakika 30 za nyingeza, Edward aliihakikishia Simba B Sh. Milioni 40 na Kombe la michuano hiyo mipya kwa bao lake safi dakika ya 112, akiunganisha pasi ya Haroun.
    Safari hii, Watoto wa Matola hawakurudia kosa la kucheza rafu karibu na lango lao, walitulia na kucheza soka ya kuonana kwa pasi nzuri za uhakika na kwenye shambulizi wanabutua mpira, Mtibwa warushe na hadi kipyenga cha mwisho, Simba B waliibuka vinara.
    Mgeni rasmi, Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Dk Fenella Mukangara alikabidhi Kombe na mfano wa Hundi, yenye thamani ya Sh. Milioni 40 kwa Nahodha wa Simba B, Hassan Hatibu, wakati wachezaji wa timu hiyo, kila mmoja walipewa mfano wa Medali za Dhahabu.
    Mtibwa Sugar walipewa Hundi ya Sh. Milioni 20 na mfano wa Medali za Fedha kila mmoja.
    Katika mchezo huo, kikosi cha Simba kilikuwa; Abuu Hashimu, William Lucian ‘Gallas, Omary Salum/ Jesse Nyambo, Hassan Isihaka, Hassan Hatibu, Said Ndemla, Haroun Athumani, Abdallah Seseme, Rashid Ismail, Edward Christopher na Ramadhan Singano ‘Messi’/Frank Sekule.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: UKUTA MZIMA SIMBA WAPANDISHWA A Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top