• HABARI MPYA

    Wednesday, July 05, 2017

    WAKILI MSEMWA AJITOA KUWATETEA AKINA MALINZI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    WAKILI Jerome Msemwa amejitoa katika kesi namba 213/2017 inayomkabili Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi na Katibu wake, Selestine Mwesigwa pamoja na Mhasibu, Nsiande Isawafo Mwanga. 
    Katika barua yake ya leo kwenda kwa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Dar es Salaam, Wilbord Mashauri, Wakili Msemwa amesema amefikia uamuzi huo kutokana na wateja wake, Malinzi na wenzake kutompa maelekezo sahihi.
    Malinzi, Mwesigwa na Nsiande wapo rumande hadi Julai 17, upepelezi wa kesi yao utakapokamilika baada ya kunyimwa dhamana Julai 3 katika kesi inayowakabili.
    Mambo yanazidi kuwa magumu kwa Rais wa TFF, Jamal Malinzi

    Watatu hao walipandishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kwa mara ya kwanza Juni 29 na kusomewa mashitaka 28 ya kughushi na kutakatisha fedha kupitia akaunti ya TFF iliyopo katika banki ya Stanbic, Dar es Salaam.
    Hakimu Mashauri aliwanyima dhamana washitakiwa hao Alhamisi kwa sababu makosa yao mengine, ya utakatishaji fedha hayastahili dhamana.
    Katika mashitaka hayo, 25 yanakwenda moja kwa moja kwa Rais wa shirikisho hilo, Malinzi akidaiwa kughushi michakato mbalimbali ya kifedha, huku matatu yakiwahusu wote na Katibu wake na Mhasibu wake Nsiande Isawafo Mwanga.
    Katika kesi hiyo, Serikali inawakilishwa na jopo la mawakili watano, wakiongozwa na Pius Hila huku upande wa washtakiwa ukiwakilishwa na mawakili watano, wakiongozwa na Jerome Msemwa. Mawakili hao watano kwa pamoja wameshindwa kuafikiana ili washitakiwa wapatiwe dhamana.
    Na wakati kesi hiyo ikiahirishwa kutokana na upepelezi kutokamilika, upande wa washitakiwa unapata pigo kwa Wakili wao kujitoa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: WAKILI MSEMWA AJITOA KUWATETEA AKINA MALINZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top