• HABARI MPYA

    Wednesday, June 21, 2017

    IBRAHIM HAJIB NI MCHEZAJI MPYA WA YANGA

    Na Mahmoud Zubeirym, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa Simba SC, Ibrahim Hajib Migomba inadaiwa amesaini mkataba wa awali wa miaka miwili kujiunga na mahasimu, Yanga SC.  
    Habari za kuaminika kutoka ndani ya Yanga SC zinasema kwamba Hajib amemalizana na klabu hiyo na sasa kinachosubiriwa ni amalize mkataba wake Simba mwezi ujao ili akasaini mkatabaa kamili Jangwani.
    “Sisi na Hajib ni kama tayari tumekwishamalizana, kwa sababu huyu kijana amekwishasaini mkataba wa awali na kinachosubiriwa ni amalize mkataba wake Simba ili aje kusaini rasmi huku na tumtambulishe,”amesema kiongozi mmoja wa Yanga ambaye hakutaka kutajwa.
    Ibrahim Hajib Migomba (kushoto) inadaiwa amesaini mkataba wa awali wa miaka miwili kujiunga na mahasimu, Yanga SC  

    Habari za Hajib kuondoka Simba zilitarajiwa, kwani mchezaji huyo amekuwa hana furaha katika klabu hiyo kutokana naa kile kilichoonekana kama kutokubalika mbele ya viongozi wengi wa klabu hiyo.
    Walikuwa wanamchukulia kama mchezaji asiye na faida kikosini pamoja na kukiri juu ya uwezo wake mkubwa kisoka, jambo ambalo lilimfanya muda mrefu wa msimu awe anawekwa benchi.
    Na Hajib mwenyewe mapema tu alionyesha nia ya kuondoka Msimbazi ingawa mpango wake wa awali ulikuwa ni kwenda nje.
    Mwanzoni mwa msimu uliopita alikwenda Afrika Kusini kwa majaribio ambako iliripotiwa alifuzu klabu ya Lamontville Golden Arrows FC ya Ligi Kuu ya ABSA, lakini mkataba wake na Simba ukamzuia kuondoka.
    Na katikati ya msimu uliopita pia, Hajib alikwenda Haras El Hodoud ya Misri ambako iliripotiwa pia amefuzu na atajiunga na klabu hiyo akimaliza mkataba wake Simba, lakini sasa anaibukia Yanga.
    Hajib ni mchezaji aliyeibukia timu ya vijana ya Simba, ambayo ilimtoa Boom FC ya Ilala mwaka 2013, lakini baadaye akaondoka kwenda kujikomaza kwenye timu ambazo angepata nafasi ya kucheza. Alichezea Mwadui FC na kuisaida kupanda Ligi Kuu msimu wa 2014-2015.
    Alikuwa na mwanzo mzuri Simba SC chini ya kocha Mserbia, Goran Kopunovic na nyota yake kidogo iliendelea kung’ara chini ya kocha Muingereza, Dylan Kerr ingawa baada ya ujio wa Mganda Jackson Mayanja na baadaye Mcameroon, Joseph Marius Omog mambo yakaanza kuwa tofauti kidogo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: IBRAHIM HAJIB NI MCHEZAJI MPYA WA YANGA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top