NAHODHA wa Lazio amekamatwa na polisi kwa uchunguzi wa kupanga matokeo mchezoni.
Kiungo Stefano Mauri, mwenye umri wa miaka 32, alishikiliwa kwa pamoja na kiungo wa zamani wa Genoa, Omar Milanetto, polisi ilisema.
Kocha wa Juventus, Antonio Conte, ambaye ameiongoza klabu hiyo kutwaa ubingwa wa Serie A katika msimu wake wa kwanza kazini, ni miongoni mwa waliohojiwa na polisi.
Maofisa wa Polisi walitembelea pia kambi ya mazoezi ya timu ya taifa ya Euro 2012 kumuhoji beki Domenico Criscito, mwenye umri wa miaka 25.
Polisi walipekua nyumba zaidi ya 30, zikiwemo za wachezaji, makocha na viongozi wa klabu za Serie A, Serie B na madaraja ya chini zaidi.
Polisi ilisema Conte alifanyiwa uchunguzi juu ya shaka ya kushiriki mchezo mchafu wa kupanga matokeo mchezoni kati ya klabu yake ya awali, Siena na Novara, Aprili mwaka 2011. Watu wengine watano walikamatwa pia nchini Hungary kwa kuhisiwa kuwa sehemu ya mchezo huo mchafu, unaopigwa vita kali.