• HABARI MPYA

    Saturday, May 26, 2012

    SIMBA YASAJILI BEKI LA JESHINI MIAKA MITATU

    SIMBA imesajili beki mpya wa kushoto, Paul Ngalema ambaye ameingia kwa gia kubwa ya kujigamba kuwa atawatoa Amir Maftah na Juma Jabu kwenye kikosi cha kwanza. 
    Gazeti la Mwanaspoti leo, limeandika kwamba Ngalema amesaini mkataba wa miaka mitatu kwa ajili ya kuitumikia Simba msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Kombe la Kagame na Ligi ya Mabingwa Afrika akitokea Ruvu Shooting ya Kibaha, Pwani aliyoichezea kwa mafanikio makubwa. 
    Aliliambia Mwanaspoti kuwa: "Najisikia furaha kujiunga na Simba kwani ni moja ya ndoto zangu. 
    "Malengo yangu Simba ni kucheza kwa bidii ili niwe kikosi cha kwanza, nitumike kwa ajili ya kuipa mafanikio Simba na naamini hilo litawezekana,"alisema Ngalema, ambaye kwa sasa yuko nyumbani kwao, Masasi mkoani Mtwara. 
    Akizungumzia ushindani, Ngalema alisema: "Hakuna kisichowezekana kwa Mwenyezi Mungu kwani kwa kitu chochote kilicho chini ya jua, nitafanikiwa tu. 
    "Ushindani upo na ni kitu kizuri kwani inapokuwa hivyo kila mmoja atapigana kwa nguvu zote ili afanikiwe yeye pamoja na klabu kwa ujumla, tofauti na utakavyokosa mpinzani,"aliongeza Ngalema huku akisisitiza kuwa mwenye uamuzi wa mwisho ni kocha Milovan Cirkovic. 
    Ngalema kabla ya kujiunga na Ruvu, alikuwa akiichezea Majimaji ya Songea na aliihama baada ya kushuka daraja. 
    Ngalema anakuwa mchezaji wa nne kusajiliwa na Simba baada ya Mkongomani Patrick Mbiyavanga, Mganda Mudde Mussa na Abdalah Juma ambaye ni mshambuliaji aliyetokea pia Ruvu Shooting.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA YASAJILI BEKI LA JESHINI MIAKA MITATU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top