• HABARI MPYA

    Saturday, February 21, 2009

    STARS NDIO HOHE HAHE WA KUTUPWA ABIDJAN

    MICHUANO mipya ya soka kwa nchi za Afrika, ijulikanayo kama michuano ya Ubingwa wa Mataifa ya Afrika (CHAN), ambayo itakuwa ikishirikisha timu zinazoundwa na wachezaji wanaocheza ligi za nchini mwao pekee, inatarajiwa kuanza Jumapili ya leo, Februari 22 mjini Abidjan, Ivory Coast na kufikia tamati Jumapili ya Machi 8, mwaka huu.
    Nchi nane ndizo zitafungua historia ya michuano hiyo, iliyoanzishwa maalumu kuongeza wigo wa kukua kwa soka barani, ambazo ni pamoja na wenyeji Ivory Coast wanaojulikana pia kama Cote d’Ivoire, DR Congo, Ghana, Libya, Senegal, Tanzania, Zambia na Zimbabwe. Pata wasifu wa timu zote zinazoshiriki michuano hiyo.

    TANZANIA: Hohe hahe wanaowania kupata chochote

    HII ndiyo timu hohe hahe zaidi kati ya zote nane zinazofungua ukurasa wa michuano hii, kwani haina chochote cha kujivunia hadi sasa kwenye soka ya kimataifa.
    Tanzania, inayojulikana kama Taifa Stars, iliwahi kufuzu kwenye fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika, mara moja tu mwaka 1980 mjini Lagos, Nigeria na kutolewa kwenye Raundi ya Kwanza tu.
    Timu hiyo ilitolewa raundi ya kwanza kutokana na kufungwa mechi zote za Kundi A kabla ya kuambulia sare moja tu. Ilifungwa 3-1 na wenyeji Nigeria, ikafungwa 2-1 na Misri kabla ya kutoka sare ya 1-1 na Ivory Coast.
    Tangu hapo, Tanzania kama ilishiriki michuano ya kimataifa basi ni ile ya kwenye kanda yao, Kombe la Challenge linaloandaliwa na Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) au michuano mingine isiyo rasmi.
    Katika michuano ya mwisho ya Challenge iliyofanyika Kampala, Uganda angalau Tanzania ilijitutumua na kushika nafasi ya tatu, baada ya kutoka nyuma kwa mabao 2-0 na kuibuka na ushindi wa 3-2 dhidi ya Burundi na kuashiria kwamba soka yake kwa sasa iko juu kidogo, tofauti na miaka ya katikati. Tanzania imewahi kutwaa taji hilo la CECAFA mara mbili tu, mwaka 1974 mjini Dar es Salaam na 1994 mjini Nairobi, Kenya.
    Stars inayonolewa na Mbrazil, Marcio Maximo anayesaidiwa na mzalendo Ally Bushiri sambamba na Meneja, Leopold ‘Tussle’ Mukebezi, ilikuwa ya kwanza kukanyaga ardhi ya Ivory Coast katika timu saba ngeni zinazoshiriki michuano hiyo.
    Stars iliwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Felix Houphouet Boigny (rais wa zamani wa Ivory Coast) Jumatano, majira ya saa 8: 00 mchana, ikifuatiwa na wapinzani wao wa kwanza kwenye michuano hii, Senegal iliyotua mjini humo saa 3:00 usiku.
    Lakini kwa ajili ya michuano hii, Taifa Stars imejiandaa vizuri na alipozungumza na mwandishi wa makala hii kabla ya kuondoka, Katibu Mkuu wa TFF, Frederick Mwakalebela, alisema kwamba timu iko vizuri kwa asilimia 100.
    “Tumehakikishiwa na benchi la ufundi, hakuna tatizo lolote kwenye timu, timu iko vizuri, wachezaji wana ari, na tunaamini watafanya vizuri,” alisema.
    Pamoja na yote, Stars inabakia kuwa timu iliyofuzu kwenye michuano hiyo katika hali ya kustaajabisha, ikiwang’oa Sudan kwa jumla ya mabao 5-2, ikianza kushinda nyumbani 3-1 na ugenini pia 2-1.
    Awali ilizitoa Kenya kwa jumla ya mabao 2-1, ikafungwa ugenini 1-0 na kushinda nyumbani 2-0, kabla ya kuitoa na Uganda pia kwa jumla ya maao 3-1, ikianza na ushindi wa nyumbani 2-0 na kwenda kulazimisa sare ya 1-1 mjini Kampala.
    Wapinzani wao kundini (A) ni Ivory Coast, Senegal na Zambia.
    Katika michuano hii, Tanzania kikosi chake kinaundwa na wachezaji wengi zaidi wa wawakilishi wake kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika, Yanga ya Dar es Salaam, ambayo imekuwa kwenye kiwango cha juu kisoka kwa miaka mitatu mfululizo sasa.
    Yanga inatoa wachezaji 10 kwenye kikosi cha Maximo, ambao ni Nahodha Nsajigwa Shadrack, Nurdin Bakari, Nadir Haroub ‘Cannvaro’, Amir Maftah, Athumani Iddi ’Chuji’, Kiggi Makasy, Geoffrey Boniface, Abdi Kassim ‘Babbi’, Mrisho Ngassa na Jerry Tegete.
    Watani wa jadi, Simba wao wanachangia wachezaji sita kwenye kikosi kilichokwenda Ivory Coast, ambao ni Deogaratius Boniventure, Kelvin Yondani, Juma Jabu, Henry Joseph, Haruna Moshi na Mussa Hassani Mgosi, wakati Mtibwa Sugar inatoa wachezaji wawili ambao ni Salum Sued na Shaaban Nditi sawa na JKT Ruvu yenye Shaabani Dihile na Mwinyi Kazimoto.
    Wengine ni Farouk Ramadhan wa Miembeni, Erasto Nyoni wa Azam FC na Nizar Khalfan wa Moro United. Pamoja na kwamba Tanzania ni nchi hohehahe zaidi kwenye CHAN ya kwanza, lakini kwa morali waliyonayo vijana, hakika inaweza kufanya maajabu. Mungu ibariki Tanzania, ibariki Taifa Stars. Amin.


    ZAMBIA: Chipolopolo waliopania kurejesha hadhi

    BAADA ya kupoteza makali yake kwenye soka Afrika kwa zaidi ya muongo mmoja sasa, Zambia ni miongoni mwa zinazotarajiwa kutumia michuano hii kujiweka sawa na kurejesha hadhi yake.
    Katika miaka michache iliyopita, Zambia inayojulikana kwa jina la utani kama Chipolopolo, ilibahatika kuwa na wachezaji wanaocheza Ligi za Ulaya, ambao kwa hakika walichangia mafanikio ya nchi hiyo kwenye soka ya Afrika wakati huo.
    Hivyo basi, CHAN inatarajiwa kabisa kuwa nafasi ya kuibuka tena kwa nyota wa Zambia, ikianza na nyota wake wanaocheza Ligi za nyumbani.
    Ikumbukwe Chipopololo haikuwa kazi nyepesi kukata tiketi ya CHAN, ililazimika kushinda vita dhidi ya Swaziland, Botswana na wawakilishi wa Afrika kwenye fainali za Kombe la Dunia mwaka 2006 nchini Ujerumani, Angola.
    Januari mwaka huu, timu hiyo ilikaribishwa kushiriki michuano ya Challenge ya CECAFA ambako ilionyesha kiwango duni hata ikatolewa katika hatua ya makundi tu, baada ya sare ya bila kufungana na Kenya, 1-1 na Burundi na kufungwa 2-0 na Sudan, wakati wao walipata ushindi mmoja tu dhidi ya vibonde, Djibouti wa mabao 3-0.

    REKODI YA ZAMBIA:
    KOMBE LA MATAIFA YA AFRIKA:
    Washindi wa pili 1974 na1994
    Nusu Fainali 1982, 1990 na 1996
    Michuano ya Vijana Afrika:
    Nusu Fainali 1991,1999 na 2007
    Michezo ya Afrika:
    Fainali mwaka 1999
    Nusu Fainali 2003 na 2007

    LIBYA : Wa Kijani wasiofikirika…

    The Greens of Libya (Kijani wa Libya) wamepotelea kwenye kiza kinene kidogo tangu walipotinga fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika, mwaka 1982 na kufungwa na Ghana.
    Iliwachukua takribani miaka 24 kwa Kijani hao wa Libya kufuzu fainali nyingine za Mataifa ya Afrika, mwaka 2006 nchini Misri, ambako walitolewa kwenye hatua ya makundi tu.
    Katika CHAN, ni kwamba Libya, timu yake ya taifa inaundwa kwa asilimia kubwa na wachezaji wanaocheza ligi yake ya nyumbani, ambao watakuwa mjini Bouake kupeperusha bendera ya nchi yao.
    Timu ya taifa ya Libya, inaundwa na wachezaji wengi wa klabu za Al Ittihad, ambayo imejijengea sifa kubwa katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
    Mwaka 2007, timu hiyo ya Jiji la Tripoli ilikaribia kutwaa taji hilo, baada ya kutolewa katika Nusu Fainali na Al Ahly mjini Cairo kwa matokeo ya jumla ya 1-0.
    Katika kuwania kufuzu kwenye fainali za CHAN, Libya iliibuka kinara katika kanda ya Kaskazini kwa kuvibwaga vigogo vya ukanda huo, Tunisia na Morocco.
    Kitendo cha kulipa kisasi cha kuchapwa mabao 3-1 dhidi ya Simba wa Atlas ya Morocco kwenye mchezo wa kwanza ugenini kwa kuibuka na ushindi wa 3-0 kwenye mchezo wa marudiano nyumbani, ndicho kilichowahakikishia tiketi ya CHAN.
    Libya ni miongoni mwa timu ambazo matokeo yake ya hivi karibuni zimedhihirisha nguvu zake kali zinapocheza nyumbani, lakini timu yoyote inaweza kuwadharau wao wakiwa kwenye ardhi yao kutokana na wachezaji wake, kwa kujiamini bila ya papara.
    Kwa hakika, kulingana na kiwango cha timu hiyo, suala la kufika Nusu Fainali kwa wawakilishi hao wa Kanda ya Kaskazini mwa Afrika, linaweza kuwa si gumu.

    REKODI YA LIBYA:
    Kombe la Mataifa ya Afrika:
    Washindi wa Pili mwaka 1982


    GHANA: Nyota Weusi waliopania kutwaa taji

    Ghana ilikuwa timu inayong’ara mithili ya dhahabu miaka ya 1960 kwa bara la Afrika kwa staili ya kucheza kandanda ya kitabuni yenye kuvutia, imewafanya wataendelea kuheshimika miaka yote.
    Hakika katika CHAN, kocha Mserbia Milovan Rajevac itakuwa ni sehemu ya kujihakikishia ajira yake katika kipindi kijacho, kwani kwa matokeo yoyote mabaya, dhahiri atatupiwa virago.
    Ghana ina hazina ya kutosha ya wachezaji wazuri kutokana na ligi yake ya nyumbani na miaka yote imekuwa ikishiriki michuano mikubwa duniani, ingawa kwa miaka ya karibuni wamekuwa wakishindwa kutimiza malengo yao.
    Lakini kwa miaka ya karibuni, Nyota Weusi hao wameonyesha kuanza kufunga mabao ya msingi, hasa baada ya kutimiza ndoto yao ya muda mrefu, kucheza fainali za Kombe la Dunia nchini Ujerumani mwaka 2006, hiyo ikiwa ni mara ya kwanza kabisa kwao.
    Ghana haijaweza kutwaa Kombe la Mataifa ya Afrika tangu ilipotwaa kwa mara ya mwisho mwaka 1982 hadi walipokuja kuambulia nafasi ya tatu katika fainali za 26 za michuano hiyo, ambazo wao ndio walikuwa wenyeji mwaka 2006.
    Ni mafanikio ambayo yalitokana na matunda ya timu zao za vijana, zilizotwaa ubingwa wa Dunia mara mbili katika miaka ya 1991 na 1995, mafanikio ambayo hayajafikiwa na timu yake ya wakubwa.
    Kufika CHAN ya kwanza, Ghana ilifanya vitu adimu katika hatua za mtoano, kwani baada ya kuzitoa Niger na Togo, walikutana na wapinzani wao wa kihistoria, Nigeria na kufanikiwa kuwang’oa kwa ushindi wa mabao 3-2 kwenye mchezo wa marudiano nyumbani.
    Hii pekee inaweza kutosha kuwatia homa wapinzani wao kundini na kwenye michuano hii kwa ujumla, kwamba Black Stars (Nyota Weusi) ni wa kufikirika kabisa katika timu zinazoweza kutwaa taji la kwanza la CHAN.
    Ingawa hawafahamu sana kuhusu wapinzani wao, Libya, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Zimbabwe, Ghana itapambana na nguvu zao moja kwa moja uwanjani itakapokutana nao.

    REKODI YA GHANA:
    Kombe la Mataifa ya Afrika:
    Mabingwa miaka ya 1963, 1965, 1978 na 1982
    Washindi wa Pili miaka ya 1968, 1970 na 1992
    Nusu Fainali miaka ya 1996, 2008
    Ubingwa wa Vijana Afrika:
    Mabingwa miaka ya1993, 1999, 2009
    Ushindi wa Pili mwaka 2001
    Nusu Fainali mwaka 1991
    Michuano ya vijana Afrika chini ya miaka 17:
    Ubingwa miaka ya 1995, 1999
    Ushindi wa pili mwaka 2005
    Nusu fainali miaka ya 1997, 2007
    Michezo ya Afrika:
    Nusu Fainali miaka ya 1973, 1978 na 2003


    IVORY COAST: Tembo wanaojitosa vitani
    kwa kazi moja tu, kubakisha taji nyumbani


    Tembo wa Ivory Coast wanajitosa kwenye fainali ambazo wao ndio wenyeji wakiwa na dhamira moja kubwa, kuhakikisha taji linabaki nyumbani, shinikizo ambalo dhahiri litatokana na kucheza mbele ya maelfu ya mashabiki wake, kwenye uwanja waliouzoea.
    Katika michuano hii, kikosi cha tembo hawa wakubwa wa Ivory Coast, kitategemea zaidi mabingwa wa mwaka 1998 wa Ligi ya Mabingwa Afrika, ASEC Mimosas.
    Tembo hao waliojitenga na mafanikio tangu watwae ubingwa wa Kombe la Mataifa ya Afrika 1992, waliibuka na kukaribia kutwaa tena taji hilo katika fainali za mwaka 2006 nchini Misri, ambako walifungwa kwa mikwaju ya penalti na wenyeji.
    Kiwango duni kilichoonyeshwa na Tembo wadogo katika michuano ya 16 ya vijana Afrika, iliyofanyika mjini Kigali, Rwanda, ambako walishindwa kushinda hata mchezo mmoja, kinatia shaka kama wenyeji hawa wanaweza kufanya chochote cha maana kwenye michuano hii.
    Aidha, kuchanganyikiwa kutokana na kushindwa katika michuano mikubwa, hakika kunaizidi kuwaongezea shinikizo wenyeji hawa wahakikishe wanaopigana kufa na kupona ili wafute mikosi hiyo.
    Kila kitu kinawezekana, kwa mazingira yanayowakabili vijana hao wa kocha Georges Kouadio, kwani kwa upande wa pili, presha ya mashabiki yao inaweza kuwafanya wajiamini zaidi na kuhisi kama tayari wamekwishatwaa taji hata kabla ya michuano kuanza.
    Tembo hao wanaweza kufikiria zaidi mazuri yanayolenga kwenye michuano hiyo lakini timu hiyo inapaswa kuchunga sana juu ya timu za wapinzani Senegal, Tanzania na Zambia.
    Kouadio alikuwa Uganda kutazama wapinzani wake kundini Tanzania na Zambia waliokuwa wakishiriki michuano ya Kombe la Challenge.

    REKODI YA IVORY COAST:
    Kombe la Mataifa ya Afrika: Ubingwa mwaka 1992
    Ushindi wa pili mwaka 2006
    Nusu Fainali miaka ya 1965, 1968, 1970, 1086, 1994 na 2008
    Michuano ya vijana Afrika:
    Ushindi wa pili miaka ya 1991 na 2003
    Nusu fainali mwaka 1997
    Michuano ya vijana chini ya miaka 17 Afrika:
    Nusu Fainali mwaka 2005
    Michezo ya Afrika:
    Nusu Fainali mwaka 1965

    DRC: Kama ingekuwa enzi za Mobutu…

    Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ilikuwa miongoni mwa nchi za nguvu kwenye soka ya Afrika kati ya mwaka 1965 na 1975, enzi hizo nchi hiyo ikiwa chini ya Rais Mobutu Sese Seko Nkuku Ngbendu wa Za Banga, aliyeitawala nchi hiyo kwa miaka 32 tangu mwaka 1965 hadi 1997.
    Lakini tangu hapo, imeingia kwenye maradhi ya kupanda na kushuka kwa soka yake na pia haijaweza kufikia rekodi zake za mafanikio ya wakati huo. Utovu wa nidhamu, utawala mbovu wa umma, kukosekana vyanzo vya fedha, kwa miaka mingi vimekuwa ni vitu ambavyo vimechangia kudorora kwa mchezo huo kwenye nchi hiyo ya Afrika ya Kati.
    Chui hao wa Kongo, mafanikio yao ya mwisho makubwa katika soka barani, ilikuwa ni kushika nafasi ya tatu katika michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 1998 nchini Burkina Faso, ingawa iliponea chupuchupu kukosa tiketi ya kushiriki fainali hizo.
    Kama Tanzania wangeweza kushinda mechi ya mwisho ya kundi nyumbani, ndio wangekata tiketi ya kwenda Burkina Faso, lakini kitendo cha kukubali kufungwa Uwanja wa Taifa, kiliwabeba DRC.
    Kama si uimara wa klabu ya Tout Puissant Mazembe katika michuano ya klabu barani, nchi hiyo ingedoda zaidi kwenye ulimwengu wa soka.
    TP Mazembe ni klabu kubwa yenye maskani yake Lubumbashi, na kwa pamoja yenyewe na klabu nyingine TP Engelbert ndio wanatoa wachezaji wa kuunda timu ya taifa ya DRC kwa ajili ya fainali za kwanza za CHAN.
    Wachezaji wa kikosi cha sasa DRC wana nguvu ya kutosha na wamezoeana kutokana na kucheza pamoja kwa muda mrefu.
    Wachezaji wengine kutoka klabu ya Vita ya Kinshasa na Daring Club Motema Pembe pia wamo kikosini chini ya nahodha wa zamani wa Chui wa DRC, Mutumbile Santos, ambaye pia ni kocha wa zamani wa timu ya taifa na TP Mazembe.
    Kwa sababu hiyo, Chui wa DRC wanataka kutumia CHAN hii ya kwanza, kama mwanzo wa kurejesha enzi zao za kutawala kwenye soka ya Afrika.
    Timu hiyo iliweka kambi ya wiki mbili Afrika Kusini ambayo bila shaka inaweza kumsaidia kocha kuweka sawa mambo ya kiufundi, kwani nguvu ya Chui hao, ni kucheza kitimu kwa kuwa hawana mchezaji mwenye jina kubwa kwenye timu yao.
    REKODI ZA DRC:
    Kombe la Mataifa ya Afrika:
    Mabingwa miaka ya 1968 na 1974
    Nusu fainali miaka ya 1972, 1998

    SENEGAL: Simba wakarimu waliotua kinyonge Abidjan


    Hakika Simba wa Teranga, au Simba waliotua kinyonge Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Felix Houphouet Boigny (rais wa zamani wa Ivory Coast) mjini Abidjan, Ivory Coast Jumatano majira ya saa 1:00 usiku.
    Kwani wametua mjini humo wakiwa na kumbukumbu za kuandamwa na vyombo vya habari vya nyumbani kutokana na matokeo yake mabaya ya hivi karibuni.
    Kufanya vibaya kwenye fainali za mwisho za Mataifa ya Afrika nchini Ghana na kutolewa mapema kwenye kinyang’anyiro cha tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia mwaka 2010 sambamba na za Afrika, ni vitu vinavyowanyima raha mno.
    Kwa sababu hii si mara ya kwanza, inatokea kwenye historia ya soka ya nchi yoyote na CHAN inaweza kuwa suluhisho la kurejesha makali ya soka ya taifa hilo.
    Senegal ilikwishajizatiti kwenye ulimwengu wa soka kuanzia mapema miaka ya 2000, lakini wakali wake wa miaka hiyo sasa wamefikia kikomo na jitihada za kuisuka Senegal ya baadaye zinatarajia kuanzia kwenye CHAN.
    Hii itakuwa nafasi nzuri kwa nchi hiyo kutumia vipaji vya vijana wao, ambao wana ndoto moja kwa pamoja, kwenda kucheza soka ya kulipwa. Hakika CHAN ni matarajio ya kweli na kujenga mwanzo wa kurejesha ubora wa Simba wa Teranga.
    Wasenegali hao walipigana kiume hadi kupata tiketi ya fainali hizi, waliitoa Mali mjini Bamako kwa mikwaju ya penalti kabla ya kuitupia virago Guinea.
    Kocha wa timu hiyo, Joseph Koto anaamini kabisa timu yake itatoa upinzani na ikibidi kutwaa taji mjini Abidjan.

    REKODI ZA SENEGAL:
    Kombe la Mataifa ya Afrika:
    Washindi wa pili mwaka 2002
    Nusu fainali miaka ya 1965, 1990 na 2006


    ZIMBABWE: Mashujaa wenye matumaini ya kusonga mbele

    Mashujaa wa Zimbabwe, The Warriors, hakika wanategemea nguvu ya wana Nusu Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, mwaka 2008, Dynamos FC ya Harare, ikiwa ni miaka kumi tangu klabu hiyo icheze fainali ya michuano hiyo dhidi ya ASEC ya Abidjan.
    Dynamos imekuwa klabu yenye kuiwakilisha kwa mafanikio zaidi nchi hiyo katika michuano ya barani, kwani msimu uliopita waliifunga ASEC nyumbani na ugenini kadhalika na Zamalek ya Misri pia kabla ya kugonga mwamba kwa mabingwa wa Afrika, Al-Ahly ya Misri.
    Ni kwa matokeo hayo, Zimbabwe iliyolazimisha sare ya bila kufungana na Tanzania mjini Dar es Salaam kabla ya kwenda Ivory Coast, ambayo inaundwa na asilimia kubwa ya wachezaji wa klabu hiyo, inatarajiwa pia kuwika kwa matunda ya Dynamo.
    Kwani Zimbabwe si dhaifu sana kwenye soka ya kimataifa, ikiwa imeshiriki fainali za Mataifa ya Afrika katika miaka ya 2004 na 2006, japokuwa mara zote imekuwa ikitolewa raundi ya kwanza tu.
    Katika fainali za mwaka 2004 timu hiyo ilifungwa na Misri 2-1, Cameroon 5-3 kabla ya kuambulia ushindi pekee dhidi ya Algeria 2-1, matokeo ambayo waliyapata katika fainali za mwaka 2006 nchini Misri ambako baada ya kufungwa na Senegal 2-0, Nigeria 2-0 pia ilifanikiwa kuilaza Ghana mabao 2-1.
    Ni matokeo ambayo yanawafanya Mashujaa wa Zimbabwe wawe miongoni mwa timu za kuchungwa kwenye CHAN ya kwanza.
    Katika kuwania kufuzu, waliing’oa Namibia kwa jumla ya bao 1-0, baada ya sare katika michezo yote miwili, Harare na Windhoek. Lakini katika Raundi ya Pili ndipo Zimbabwe walipouduwaza ulimwengu wa soka baada ya kuwaangusha vigogo Afrika Kusini mjini Harare 1-0 na kwenda kuwamaliza kabisa nyumbani kwao kwa kipigo cha 2-0.
    Kama wengine wengi, Zimbabwe inaingia kwenye michuano hiyo kama wageni na haipewi nafasi ya kufika fainali au kutwaa kombe, lakini ukweli ni kwamba mashindano haya mapya yanawapa nafasi zaidi wale wenye matumaini makubwa, bila kutazama umaarufu au mafanikio ya nchi kwenye soka ya Afrika.

    REKODI ZA ZIMBABWE:
    Michezo ya Afrika:
    Walifika fainali mwaka 1995
    Nusu fainali mwaka 1991

    VIKOSI:

    IVORY COAST:
    1 Cisse Abdoul Karim
    2 Mansou Kouakou Amoro Jr.
    3 N’gouan Konan Ruffin
    4 Diomande Hamed Herve
    5 Nene Bi Tra Sylvestre
    6 Saoure Florent
    7 Bohou Dieudonne
    8 Guehi Kouko Djedje Hilaire
    9 Guedegbe Corbin
    10 Karamoko Alassane
    11 Tanoh Jacques Alain-Elisee
    12 Krecoumou Acihelou
    13 Mangoua Kesse Jean-Paul
    14 Ngossan Antoine Jean-Etienne
    15 Irie Bi Bi Sehi Elysee
    16 Okoua Christian Fabrice
    17 Dje Bi Trazie Charles
    18 Diomande Aboubacar
    19 Adou Dago Blaise
    20 N’goran Kouassi Nicaise Aristide
    21 Bile Georges Eric
    22 Zegbe Moise Valery
    23 Angban Atchouailou Vincent De Paul

    GHANA:
    1 Maccarthy Philemon
    2 Inkoom Samuel
    3 Yeboah Daniel Nana
    4 Mantey Francis
    5 Appiah Ofosu
    6 Yahaya Iddrisu
    7 Opoku Jordan
    8 Ayew Ibrahim
    9 Antwi Yaw
    10 Poku Kwadwo
    11 Yeboah Samuel Ayew
    12 Owusu Isaac
    13 Mohammed Habib
    14 Asampong Taylor Charles Bismark
    15 Manu Stephen
    16 Sowah Ernest
    17 Coffie Francis
    18 Owusu Ansah Edmund
    19 Badu Agyeman Emmanuel
    20 Andoh Ebo
    21 Afful Harrison
    22 Agyei Daniel
    23 Bonsu Godwin Osei

    LIBYA:
    1 Abud Samir
    2 Shaban Hesham
    3 Ejlal Walid
    4 Dawoud Omar
    5 Shibani Younes
    6 Esnani Mohamed
    7 Alsbaay Ali
    8 Allafi Riyad
    9 Rewani Salem
    10 Osman Ahmed
    11 Zuway Ahmed
    12 Aktait Guma
    13 Nakuaa Arafa
    14 El Borki Mansur
    15 El Amari Ashraf
    16 Abdusalam Nader
    17 Zubya Mohamed
    18 Hmadi Osama
    19 Ben Saleh Osama
    20 El Mughrabi Mohamed
    21 Msallem Abdussalam
    22 Muftah Ahmed
    23 Slil Abdulnaser

    DRC:
    1 Kidiaba Muteba
    2 Diba Ilunga
    3 Ebunga Simbi
    4 Nkulukuta Miala
    5 Mutombo Kazadi
    6 Mihayo Kazembe
    7 Kasongo Ngandu
    8 Mputu Mabi
    9 Ntela Kalema
    10 Bedi Mbenza
    11 Kanda Deo Amkok
    12 Mabele Bawaka
    13 Salakiaku Matondo
    14 Lofo Bongeli
    15 Kimuaki Joel
    16 Vuanga Kwenda
    17 Ngoy Mbomboko
    18 Bokese Gladys
    19 Kaluyituka Dioko
    20 Onoseke Wembi
    21 Pambani Makiadi
    22 Mvete Luyeye
    23 Bombasa Bengele

    SENEGAL:
    1 Ba Mamadou
    2 Diallo Moustapha
    3 Coly Mohamed
    4 Ndiaye Sidy
    5 Diouf Mor
    6 Djilabodji E. H. Papy Mison
    7 Traore Mamadou Baila
    8 Badiane Vito
    9 Diamanka Pape Maly
    10 Ly Mouchid Iyane
    11 Guene Yally Fall
    12 Diagne Libasse Laye
    13 Ndiour Babacar
    14 Ndao El Hadji Sara
    15 Fall Malick
    16 Sy Biti
    17 Ndiaye M. Benjeloun
    18 Diallo Karamba
    19 Sow Alpha Oumar
    20 Hane Amadou Fall
    21 Diallo Mame Cheikh
    22 Dembele Moussa
    23 Ndiaye P. Latyre

    TANZANIA:
    1 Munishi Deogratias
    2 Swedi Salum
    3 Haruna Moshi
    4 Athumani Iddi
    5 Kevin Patrick Yondan
    6 Henry Joseph
    7 Kigi Makasi
    8 Mrisho Ngassa
    9 Geoffrey Bonny
    10 Jerry Tegete
    11 Mussa Mgosi
    12 Nurdin Bakari
    13 Nadir Haroub
    14 Shadrack Nsajigwa
    15 Abdi Kassim
    16 Nizar Khalfan
    17 Amir Maftah
    18 Shaaban Mohamed Dihile
    19 Shaaban Nditi
    20 Farouk Ramadhan Mzee
    21 Juma Jabu
    22 Erasto Edward Nyoni
    23 Mwinyi Kazimoto

    ZAMBIA:
    1 Banda Jacob
    2 Kasonde Francis
    3 Mulenga Nyambe
    4 Sakuwaha Jonas
    5 Tana Elijah
    6 Banda Dennis
    7 Banda Henry
    8 Kasunga Patirick
    9 Banda Stanley
    10 Njobvu William
    11 Mudenda Kennedy
    12 Chilufya George
    13 Chilufya Jimmy Chisenga
    14 Mbola Emmanuel
    15 Singuluma Given
    16 Poto Mike
    17 Lwipa Ignatius
    18 Bwalya Simon
    19 Hachipuka Kebby
    20 Mubanga Perry
    21 Sakala Makundika
    22 Kaumbwa Davy
    23 Makandawire Elson

    ZIMBABWE:
    1 Manyatera Willard
    2 Nyamupangedengu Maxwell
    3 Kutyauripo David
    4 Sweswe Thomas
    5 Jambo Zhaimu
    6 Zhokinyu Guthrie
    7 Machapa Oscar
    8 Magariro George
    9 Veremu Daniel
    10 Banda Gilbert
    11 Gomba Carrington
    12 Tafirenyika Pride
    13 Moyo Mtshumayeli
    14 Karuru Ovidy
    15 Gutu Archford
    16 Kamusoko Thabani
    17 Meleka Elvis
    18 Chitato Edmore
    19 Nyamandwe Tawanda
    20 Marufu Phillip
    21 Malajila Cuthbert
    22 Dube Tafadzwa
    23 Kawinga Clive
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: STARS NDIO HOHE HAHE WA KUTUPWA ABIDJAN Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top