• HABARI MPYA

    Saturday, June 10, 2017

    TAFCA YAAGIZA WANACHAMA WAKE KUWASILISHA TAARIFA ZA UCHAGUZI HARAKA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KAMATI ya Utendaji ya Chama cha Makocha wa Mpira wa Miguu nchini (TAFCA), imeagiza vyama vya mikoa viwe vimetuma kabla ya Juni 14 mwaka huu muhtasari wa mikutano ya uchaguzi waliofanya.
    Pia Kamati hiyo imeunda Kamati ya Uchaguzi yenye wajumbe watano, akiwemo Mbunge wa Kilolo (CCM), Venance Mwamoto.
    Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari Dar es Salaam jana na Katibu Mkuu wa TAFCA, Michael Bundara, ilisema uamuzi huo ulifikia katika kikao cha dharura cha Kamati ya Utendaji ya chama hicho kilichofanyika jana.
    Kocha Msaidizi wa Singida United, Fredy Felix Minziro ni miongoni mwa wanachama wa TAFCA

    “Leo (jana) Kamati ya Utendaji ya TAFCA imekutana kwa dharura hapa Dar es Salaam kupitia barua kutoka TFF (Shirikisho la Soka Tanzania) inayoeleza masuala ya msingi yanayotakiwa yafanyiwe kazi kabla ya uchaguzi wetu utakaofanyika Julai 30 mwaka huu.
    “Baada ya kupitia barua hiyo ya TFF, Kamati ya Utendaji ya TAFCA inatoa maagizo yafuatayo kwa wanachama wake ambao ni vyama vya mikoa:
    “Kila mwanachama wa TAFCA atume nyaraka za muhtasari wa chaguzi walizofanya kabla ya Juni 14 mwaka huu, ambapo mwanachama asiyetuma nyaraka hizo hadi tarehe hiyo hataruhusiwa kuingia kwenye Mkutano Mkuu,” ilisema taarifa hiyo.
    Wakati huohuo, TAFCA imeunda Kamati ya Uchaguzi ya chama hicho, ambapo Mwenyekiti ni Ewdin Kidifu, Katibu Abdillahi Abdulaziz, wakati Wajumbe ni Ramadhani Mambosasa, Hemed Mteza na Mwamoto.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TAFCA YAAGIZA WANACHAMA WAKE KUWASILISHA TAARIFA ZA UCHAGUZI HARAKA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top