• HABARI MPYA

    Saturday, June 15, 2019

    YANGA B YAIPIGA SIMBA B 2-1 NA KUBISHA HODI NUSU FAINALI LIGI KUU YA U20

    Na Asha Said, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Yanga imeibuka na ushindi wa 2-1 dhidi ya mahasimu wa jadi, Simba SC katika mchezo wa Kundi A Ligi Kuu ya Tanzania Bara kwa vijana chini ya umri wa miaka 20 Ijumaa Uwanja wa Azam Complex, Chamazi mjini Dar es Salaam.
    Kwa ushindi huo, Yanga SC inafikisha pointi nne baada ya sare ya 0-0 na Kagera Sugar kwenye mchezo wa kwanza, wakati Simba SC inabaki na pointi yake moja kufuatia sare ya 1-1 na Ruvu Shooting kwenye mchezo wao wa kwanza.
    Haukuwa ushindi mwepesi kwa Yanga SC, kwani walilazimika kusubiri hadi dakika ya mwisho kusawazisha bao kupitia kwa Yassin Saleh dakika ya 90 kufuatia Jackson James kutangulia kuifungia Simba dakika ya 27.


    Na wakati Simba SC wakiwa wanajiuliza kwa kuruhusu bao la kusawazisha dakika ya mwisho, Yanga wakapata bao la pili na la ushindi kupitia kwa Erick Msagati dakika ya nne ya muda wa nyongeza baada ya kukamilika kwa muda wa kawaida wa mchezo.
    Mechi nyingine ya Kundi A leo, mabao ya Jonathan Mrashani dakika ya 45 na ushei kwa penalti na 60 yakaipa Kagera Sugar ushindi wa 2-0 hapo hapo Azam Complex.
    Mechi za kundi hilo zitakamilishwa Jumapili kwa Simba kumenyana na Kagera Sugar na Yanga na Ruvu Shooting na kisha timu mbili za juu zitafuzu nusu fainali.
    Jumamosi kutakuwa na mechi za mbili za Kundi B, ambazo kama kawaida zitaonyeshwa na chaneli ya AzamSport2 ya Azam TV.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA B YAIPIGA SIMBA B 2-1 NA KUBISHA HODI NUSU FAINALI LIGI KUU YA U20 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top