• HABARI MPYA

    Monday, June 24, 2019

    TSHABALALA ASAINI MKATABA MPYA WA MIAKA MIWILI KUENDELEA NA KAZI SIMBA SC

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    NAHODHA Msaidizi wa Simba SC, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ amesaini mkataba mpya wa miaka miwili kuendelea kuwatumikia mabingwa hao wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.
    Tshabalala ambaye yupo na kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania kilichopo Misri kwenye Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON), alisaini mkataba huo kabla ya kuondoka nchini Juni 7, mwaka huu.
    Tshabalala anaingia kwenye orodha ya wachezaji wengine muhimu walioongeza mikataba chini ya Nahodha Mkuu, John Bocco, kipa Aishi Manula, mabeki Erasto Nyoni, Shomari Kapombe, kiungo Jonas Mkude na mshambuliaji Meddie Kagere raia wa Rwanda.

    Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ amesaini mkataba mpya wa miaka miwili kuendelea kupiga kazi Simba SC

    Na hiyo ni baada ya kazi nzuri msimu huu kwa pamoja na wenzao wakiiwezesha klabu kutetea ubingwa wa Ligi Kuu na kufika Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika ambako walitolewa na vigogo, TP Mazembe ya DRC.
    Tshabalala alijiunga na Simba SC Jun mwaka 2014 akitokea Kagera Sugar ya Bukoba baada ya awali kupitia akademi ya Azam FC. 
    Pamoja na kuwaongezea mikataba wachezaji wake wa msimu uliopita, Simba SC pia imesaini wachezaji wanne ambao ni mshambuliaji Mbrazil, Wilker Henrique da Silva kutoka Bragantino ya Daraja la Nne nchini kwao, kipa Beno Kakolanya kutoka Yanga, beki wa kati, Kennedy Wilson Juma kutoka Singida United wote Watanzania na kiungo wa kimataifa wa Sudan, Sharaf Eldin Shiboub Ali Abdalrahman.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TSHABALALA ASAINI MKATABA MPYA WA MIAKA MIWILI KUENDELEA NA KAZI SIMBA SC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top