• HABARI MPYA

    Tuesday, June 18, 2019

    SIMBA SC YAENDELEA KUANIKA SILAHA ZA MSIMU UJAO, YASAJILI BEKI RASTA WA SINHIDA

    Na Asha Said, DAR ES SALAAM
    BEKI wa kati wa kimataifa wa Tanzania, Kennedy Wilson Juma amesaini mkataba wa miaka miwili kujiunga na mabingwa wa Bara, Simba SC akitokea Singida United.
    Wilson ametambulishwa mchana wa leo akisaini mkataba na mmoja wa Wakurugenzi wa klabu, Salum Abdallah ‘Try Again’ aliyekuwa kaimu wa Rais wa Simba SC.
    Baada ya misimu miwili mizuri na Singida, wa kwanza akiiwezesha kumaliza katika nafasi ya pili Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Azam Sports Federation Cup (ASFC) mwaka juzi wakifungwa na Mtibwa Sugar 3-2 katika fainali, Wilson anahamia Dar es Salaam.

    “Uwepo wa Kennedy kwenye kikosi kwa kushirikiana na mabeki wengine tulionao ni hakika safu yetu ya ulinzi itakuwa imara zaidi,” imesema taarifa ya Simba katika utambulisho wa mchezaji huyo.
    Wilson amekuwa sehemu ya kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars kwa miaka mitatu  sasa na alishiriki mechi za kufuzu Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON).
    Aliitwa kwenye kikosi cha kwanza kabisa cha wachezaji 39 kwa ajili ya fainali na AFCON zinazotarajiwa kuanza Ijumaa wiki mjini Cairo nchini Misri.
    Hata hivyo, beki huyo mwenye rasta akaenguliwa kwenye mchujo wa kwanza tu pamoja na beki mwingine, Shomari Kapombe na viungo Jonas Mkude, wote wa Simba na Ibrahimu Ajibu wa Yanga, Kennedy Wilson wa Singida United, Ally Ally wa KMC, Khamis Khamis wa Kagera Sugar na Ayoub Lyanga wa Coastal Unon ya Tanga.
    Mchujo wa pili wa Kocha Mnigeria, Emmanuel Amunike ukawapitia mabeki kipa Suleiman Salula Malindi SC ya Zanzibar, mabeki Claryo Boniface wa timu ya vijana chini ya umri wa miaka 20, Ngorongoro Heroes, David Mwantika wa Azam FC, Abdi Hassan Banda wa Baroka FC ya Afrika Kusini, kiungo na Shiza Ramadhani Kichuya anayecheza ENNPI kwa mkopo kutoka Pharco zote za Misri. 
    Wengine walioenguliwa ni, kiungo Freddy Tangalu wa Lipuli FC na washambuliaji Miraj Athumani wa Lipuli FC na kinda wa Serengeti Boys (U17), Kelvin John ‘Mbappe’.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YAENDELEA KUANIKA SILAHA ZA MSIMU UJAO, YASAJILI BEKI RASTA WA SINHIDA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top