• HABARI MPYA

    Wednesday, December 05, 2012

    HAKUNA MAJERUHI STARS, VIJANA WAKO TAYARI KUCHINJA KORONGO

    Kikosi cha Stars

    Na Mahmoud Zubeiry, Kampala
    KOCHA wa timu ya Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars, Mdenmark Kim Poulsen amesema hana majeruhi hata mmoja kikosini mwake kuelekea mechi ya Nusu Fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Tusker Challenge kesho, Uwanja wa Mandela, Namboole mjini hapa.
    Akizungumza leo mjini hapa baada ya mazoezi kwenye Uwanja wa Chuo Kikuu Kyambogo, Poulsen alisema kwamba timu iko tayari kwa mchezo huo wa kesho unaotarajiwa kuwa wa kukata na shoka.
    “Vijana wamejiandaa vizuri kabisa na wote wako katika hali nzuri ya kucheza ila tunachoomba ni fair play kutoka kwa muamuzi maana tunacheza na wenyeji ambao wana watazamaji wengi,” alisema.
    Alisema timu zote mbili ni nzuri na iwapo muamuzi atachezesha vizuri basi utakuwa ni mchuano mkali. “Vijana wana ari na mchezo huu na tukipewa fair play tutacheza vizuri kama tulivyofanya katika michezo  dhidi ya Rwanda,” alisema Poulsen.
    Refa wa mechi ya Cranes na Stars anatarajiwa kuwa Mohamed El Fadil kutoka Sudan ambaye pia alichezesha mechi ya Stars dhidi ya Rwanda Robo Fainali.
    Alisema ana furaha kwa kuwa hakuna majeruhi hata mmoja na pia aliwasifu wachezaji wake kwa kuonyesha umoja na nidahmmu ya hali ya juu. “Hawa wanakaa kama familia si unawaona walivyo pamoja?” alisema Poulsen na kuongeza kuwa hilo ni muhimu sana kwa mchezaji.
    Naye kocha msaidizi, Sylvester Mash alisema Stars ina nafasi kubwa sana ya kushinda mechi hii kwa sababu wenyeji wao, The Cranes watakuwa wanacheza kwa wasiwasi kwa kuwa wako nyumbani .
    “Timu yetu ina hamasa kabisa na ukizingatia Uganda wako nyumbani, wao ndio wana tension kubwa zaidi,” alisema na kuongeza kuwa mchezo huu utakuwa wa kusisimua sana.
    Akizungumza kutoka Dar es Salaam, Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, wadhaminiwa Stars, George Kavishe alisema Stars ina kila sababu ya kutinga fainali na kunyanyua kombe kwa mara ya nne.
    “Sisi kama wadhamini tunasubiri ushindi maana tuna imani na Stars na hatua waliyofikia ni nzuri nay a kutia moyo kwa hivyo watanzania wajitokeze kwa wingi na kuufuatilia mchezo huu kesho,” alisema Kavishe.
    Mchezo wa Stars na Cranes utatanguliwa na semi fainali ya kwanza kati ya Zanzibar na Kenya ambao pia ni mchezo wa kusisimua kwani timu zote mbili zimeshaonyesha uwezo mkubwa.
    Kocha wa Zanzibar Salum Nassor ameshatangaza mara mbili akiwa Zanzibar na hapa Kampala kuwa iwapo hataondoka na kombe basi atabwaga manyanga.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: HAKUNA MAJERUHI STARS, VIJANA WAKO TAYARI KUCHINJA KORONGO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top