• HABARI MPYA

    Sunday, May 06, 2012

    PREVIEW SIMBA NA YANGA


    Simba

    VIKOSI:
    SIMBA: Juma Kaseja, Nassor Chollo, Amir Maftah, Shomary Kapombe, Kelvin Yondan, Patrick Mafisango, Uhuru Suleiman, Mwinyi Kazimoto, Felix Sunzu, Haruna Moshi na Emanuel Okwi.
    BENCHI: Ally Barthez, Derrick Walullya, Obadia Mungusa, Victor Costa, Ramadhan Singano, Gervais Kago na Salum Machaku.
    Yanga

    YANGA: Yaw Berko, Nsajigwa Shadrack, Oscar Joshua, Nadir Cannavaro, Athumani Iddi, Juma Seif, Shamte Ally, Haruna Nironzima, Davies Mwape, Kenneth Asamoah na Hamisi Kiiza.
    BENCHI: Shaaban Kado, Omega Seme, Zuberi Ubwa, Job Ibrahim, Bakari Mbega, Nurdin Bakari, Idrisa Senga, Pius Kisambale na Geoffrey Bonny.    

    WATANI wa jadi katika soka ya Tanzania, Simba na Yanga wanashuka dimbani leo kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam katika mchezo wa funga dimba, Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, huku kila timu ikihitaji kulinda hadhi yake tu.
    SImba tayari bingwa- lakini ili sherehe za kukabidhiwa Kombe zinoge lazima wamfunge mtani wa jadi- lakini kwa Yanga, baada ya kupokonywa ubingwa wa Bara na kukosa hata nafasi ya pili, kitu pekee cha kuwafariji mashabiki wao ni kuua mnyama.
    Yanga leo itamkosa mshambuliaji wake mzoefu wa mechi za watani wa jadi, Jerry Tegete ambaye anatumikia adhabu ya kutocheza hadi mwisho mwa msimu.
    Simba inaingia kwenye mchezo wa leo ikiwa katika mwendo mzuri- ikishinda mechi za ligi na za Afrika- zaidi safu yake ya ushambuliaji inaonekana kuchanganya zaidi katika siku za karibuni.
    Hapana shaka, Mserbia Milovan Cirkovick ataendelea kuwapanga pamoja Haruna Moshi Shaaban ‘Boban’ na Felix Sunzu katikati na pembeni yao Emmanuel Okwi kushoto na Uhuru Suleiman kulia- hii maana yake atashambulia na wanaume wanne.
    Yanga kadhalika- kuna uwezekano Freddy Felix Minziro akatumia washambuliaji wanne- Kenneth Asamoah na Davies Mwape katikati na pembeni yao Hamisi Kiiza kushoto na Shamte Ally kulia.
    Haruna Niyonzima katika kiungo cha Yanga na Mwinyi Kazimoto katika kiungo cha Simba ni burudani nzuri inayotarajiwa Taifa leo.
    Patrick Mafisango atacheza kama kiungo wa ulinzi, lakini kwa sababu anapanda sana- inamaanisha Simba inawezaa kuifunika Yanga katika nafasi ya kiungo- itategemea Juma Seif ‘Kijiko’ atakuwa katika hali gani leo na atachezaje, maana jamaa huwa hatabiriki.
    Beki wa kulia wa Yanga atakuwa ‘babu’ Nsajigwa Shadrack upande ule ambao atakuwa anateleza Okwi- wakati kulia atakuwapo Oscar Joshua eneo ambalo ni njia ya Uhuru.
    Beki wa kulia wa SImba bila shaka atakuwa Nassor Masoud ‘Chollo’ ambako atakuwa anapita Kiiza na beki wa kushoto atakuwa Amir Maftah katika njia ya Shamte Ally.
    Katikati Yanga, Minziro anaweza kuamua kumpanga Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na Chacha Marwa au kuendelea kumchezesha pamoja na Athumani Iddi ‘Chuji’.
    Simba hapana shaka Milovan ataendelea kuwachezesha pamoja katikati Shomary Kapombe na Kelivn Yondan. Langoni Simba piga, ua atasimama Kaseja tu labda awe mgonjwa wa kushindwa kucheza hata kwa sindano ya ganzi. Yanga bila shaka atadaka Mghana Yawe Berko.     


    JE WAJUA?
    Mara ya mwisho Simba na Yanga kukutana katika mechi ya kulinda heshima- baada ya tayari kuwa bingwa amekwishapatikana ilikuwa ni Aprili 27, mwaka 2008 Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam na timu hizo zilitoka sare ya bila kufungana, Yanga ikiwa tayari imekwishatwaa ubingwa chini ya kocha Mserbia Profesa Dusan Savo Kondic.

    Kocha wa Simba katika mechi hiyo ya Aprili 27, 2008 alikuwa ni Profesa Milovan Cirkovic, ambaye baada ya mechi hiyo aliondoka SImba kutokana na uongozi wa klabu hiyo, chini ya aliyekuwa Mwenyekiti wake, Hassan Daalal kugoma kumuongezea mshahara.

    Pambano la kwanza la Ligi Kuu, wakati huo klabu ya bingwa ya taifa baina ya watani wa jadi lilifanyika Juni 7, mwaka 1965 Uwanja wa Ilala (sasa Karume), wakati huo Simba bado inaitwa Sunderland na Yanga ndio walioshinda mechi hiyo, bao pekee la
    Mawazo Shomvi dakika ya 15.

    Ushindi mkubwa zaidi kwa Yanga dhidi ya watani wao wa jadi, Simba ni wa mabao 5-0 Juni 1, 1968, siku hiyo Maulid Dilunga ‘Mexico’ akifunga mabao mawili katika dakika ya 18 kwa penalti na na 43, wakati mengine yalifungwa na Salehe Zimbwe dakika ya 54 na 89 na Kitwana Manara dakika ya 86.

    Simba ililipa kisasi cha 5-0 Julai 19, mwaka 1977 kwa kuwafunga Yanga mabao 6-0 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam- siku hiyo Abdallah ‘King’ Kibadeni akifunga mabao matatu peke yake katika dakika za 10, 42 na 89 wakati mengine yalifungwa na Jumanne Hassan 'Masimenti' dakika ya 60 na 73 na beki wa Yanga, Suleiman Sanga akajifunga dakika ya 20.

    Sare ya mabao 4-4 Novemba 9, mwaka 1996 Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha, inabakia kuwa sare ya kihistoria katika mapambano ya watani wa jadi kufungana mabao mengi. Mabao ya Yanga yalifungwa na Edibilly Lunyamila kwa penalti dakika ya 28, Mustafa Hozza alijifunga dakika ya 64, Said Mwamba 'Kizota' dakika ya 70 na Sanifu Lazaro ‘Tingisha’ dakika ya 75. Simba mabao yao yalifungwa na Thomas Kipese dakika ya saba, Ahmed Mwinyimkuu dakika ya 43 na Dua Saidi dakika ya 60 na 90.

    Leo Yanga inatarajiwa kuongozwa na kocha mzalendo, beki wake wa zamani Freddy Felix Minziro wakati Simba ina Mserbia, Milovan Cirkovic- hii ni mara ya kwanza benchi la Yanga kuwa na kocha mzawa katika mechi dhidi ya watani tangu alipofukuzwa Kenny Mwaisabula mwaka 2004.

    Juma Kaseja atakuwa ni mchezaji aliyeanza muda mrefu zaidi kucheza mechi za watani wa jadi, mwaka 2003 mechi yake ya kwanza ikiwa ni ya Aprili 20, mwaka 2003 akikaribishwa na kipigo cha mabao 3-0, yaliyotupiwa nyavuni na Kudra Omary dakika ya 30, Heri Morris dakika ya 32 na Salum Athumani dakika ya 47.

    Washambuliaji wote wa kigeni wa Yanga, Mghana Kenneth Asamoah, Mganda Hamisi Kiiza na Mzambia Davies Mwape wamekwishatikisa nyavu za Simba- ingawa bao la Kiiza lilikataliwa kwenye fainali ya Kombe la Kagame Julai mwaka jana, kwa madai aliotea, lakini lilionekana kuwa bao salama kabisa.

    Ni mshambuliaji mmoja tu wa kigeni wa Simba, Felix Mumba Sunzu Jr katika washambuliaji watatu wa kigeni wa Simba, wengine wakiwa Gervais Kago kutoka Jamhuri ya Afrika ya Kati na Emmanuel Okwi kutoka Uganda aliyeweza kutikisa nyavu za Yanga.

    Kiungo Patrick Mutesa Mafisango wa Simba kutoka Rwanda, amekwishatikisa nyavu za Yanga katika msimu wake huu wa kwanza Msimbazi- lakini Mnyarwanda mwenzake Haruna Hakizimana Fadhil Niyonzima anaingia kwenye mechi ya mwisho ya msimu leo- akiwa hajui nyavu za SImba zinatikisikaje.

    Hili linakuwa pambano la 11, kwa watani wa jadi kukutana Uwanja mpya wa Taifa tangu ufunguliwe, awali katika mapambano 10, Yanga ilishinda mechi tano, Oktoba 26, 2008 (1-0), Oktoba 29, 2011 (1-0), Julai 10, 2011 (1-0), Desemba 25, 2009 (2-1) na Agosti 18, 2010, iliposhindwa penalti 3-1 baadaye ya sare 0-0, wakati Simba imeshinda mechi tatu tu Oktoba 31, 2009 (1-0), Aprili 18, 2010 (4-3) na Agosti 17, 2011 (2-0) na timu zimetoka sare mara mbili, Aprili 19, 2009 (2-2) na Machi 5, 2011 (1-1).
    Kiiza kushoto na Chollo kulia, leo itakuwaje?

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: PREVIEW SIMBA NA YANGA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top