• HABARI MPYA

    Monday, June 12, 2017

    STARS YAELEKEZA NGUVU KWENYE KOMBE LA COSAFA

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
    TIMU ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars itaingia kambini tena Juni 14, mwaka huu kujiandaa na michuano inayoratibiwa na Baraza la Soka la Kusini mwa Afrika (COSAFA).
    Michuano hiyo inatarajiwa kuanza Juni 25, mwaka huu ambako Taifa Stars itakwenda Afrika Kusini, Juni 20, mwaka huu.
    Kocha wa Taifa Stars, Salum Mayanga amepanga kufanya mabadiliko madogo ya kikosi cha Taifa Stars kitakaochokwenda kushiriki michuano hiyo.
    Mabeki wa Taifa  Stars kutoka kulia Salim Mbonde, Shomary Kapombe, Abdi Banda na Gardiel Michael
    Kocha kesho atafanya uteuzi wa wachezaji wengine atakaowajumuisha kwenye kikosi chake, atafanya mabadiliko kidogo hivyo  kesho atatangaza majina ya wachezaji ambao wataingia kambini kujiandaa na michuano hii ya Cosafa inayoanza Juni 25 huko Afrika Kusini.
    Stars itaingia kwenye maandalizi ya Cosafa ikitoka kuanza vibaya mbio za kuwania tiketi ya Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2019 nchini Cameroon baada ya kulazimishwa sare ya 1-1 na Lesotho usiku wa Jumamosi Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam katika mchezo wa kwanza wa Kundi L.
    Sare hiyo inamaanisha kocha Salum Mayanga ameshindwa kuvunja mwiko wa muda mrefu wa Taifa Stars kutoshinda mechi zaidi ya mbili, baada ya kushinda mechi mbili za kirafiki mwezi Machi 2-0 dhidi ya Botswana na 2-1 dhidi ya Burundi.
    Katika mchezo huo, Tanzania ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 27 kupitia kwa Nahodha wake, Mbwana Ally Samatta kwa shuti la mpira wa adhabu baada ya beki wa kushoto, Gardiel Michael kuangushwa nje ya boksi.                        
    Hata hivyo, bao hilo halikudumu, kwani Lesotho, au Mamba walisawazisha dakika ya 34 kupitia kwa Thapelo Tale aliyeunganisha pasi nzuri ya Jane Thaba-Ntso.
    Wakati huo huo, awamu ya pili ya kozi ya Daraja A inayoendeshwa na Shirikisho la soka Afrika (CAF) imeanza leo kwenye ukumbi wa Shirikisho la soka Tanzania (TFF).
    Kozi hiyo inahusisha makocha 20 ambao walishiriki kwenye kozi hiyo ya awamu ya kwanza iliyofanyika jijini Dar es Salaam Novemba, mwaka jana.
    Mkufunzi wa kozi hiyo ni Mtanzania Sunday Kayuni ambaye pia atakuwa na wataalam wa masuala ya Lishe, Masoko, Tiba, Habari, Bima pamoja na mtaalam wa masuala ya upingaji wa matumizi ya utumiaji wa dawa za kuongeza nguvu michezoni.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: STARS YAELEKEZA NGUVU KWENYE KOMBE LA COSAFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top