Na Mwandishi Wetu, YAOUNDE
KIKOSI kipya cha Cameroon kimeendeleza wimbi la ushindi katika kuwania tiketi za Fainali za Mataifa ya Afrika mwakani Morocco, baada ya jana kuifumua Ivory Coast mabao 4-1 mjini Yaounde.
Clinton N'Jie na Vincent Aboubakar kila mmoja alifunga mabao mawili kwa Simba Wasiofungika huku bao pekee la Tembo wa Ivory Coast likifungwa na Mwanasoka Bora Afrika, Yaya Toure.
Aibu yao: Yaya Toure aliiongoza Ivory Coast jana ikifungwa 4-1 Cameroon iliyosukwa upya baada ya Kombe la Dunia
Cameroon iliyosukwa upya baada ya Kombe la Dunia, ilishinda mechi ya kwanza ya Kundi D mabao 2-0 dhidi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Jumamosi iliyopita.
Cameroon, Algeria, Kongo Brazzaville, Burkina Faso, Cape Verde, Senegal na Tunisia zimefanikiwa kushinda mfululizo mechi mbili za mwanzoni wakati Misri ina hali mbaya baada ya kufungwa mfululizo.
Mabingwa watetezi Nigeria wameendeleza rekodi ya kutofungwa na kuruhusu nyavu zao kuguswa na Afrika Kusini, baada ya kulazimisha nao sare ya bila kufungana 0-0 mjini Cape Town.
Super Eagles walipambana mno kupata sare hiyo ugenini, baada ya kupoteza mechi ya kwanza nyumbani mbele ya Kongo Jumamosi iliyopita.
Uganda imeifunga 2-0 Guinea, Algeria imeshinda 1-0 dhidi ya Mali mjini Blida, Kongo imeifunga Sudan 2-0 mjini Pointe-Noire, Burkina Faso imeichapa Angola 3-0 mjini Luanda na Cape Verde imewafunga mabingwa wa 2012 Zambia 2-1 mjini Praia.
Senegal imeshinda 2-0 dhidi ya Botswana mjini Gaborone na Tunisia imewafunga mabingwa wa kihistoria Misri 1-0 mjini Cairo, wakiwaacha Mafarao bila pointi katika Kundi G.
0 comments:
Post a Comment