• HABARI MPYA

    Tuesday, September 23, 2014

    OSCAR JOSHUA KUWAKOSA WAJELAJELA JUMAPILI, MAXIMO AMUANDAA BEKI WA JESHINI KUZIBA NAFASI YAKE

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    BEKI wa kushoto wa Yanga SC, Oscar Joshua Fanuel anaweza kuukosa mchezo wa Jumapili wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Prisons ya Mbeya Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Oscar aliumia katika mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu dhidi ya Mtibwa Sugar, Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro na kutolewa dakika ya 33 akimpisha kiungo Omega Seme.
    Seme alikwenda kucheza nafasi ya kiungo wa ulinzi, wakati Mbuyu Twite alihamia nafasi aliyokuwa akicheza Joshua katika mchezo ambao Yanga ililala 2-0 Jumamosi. 
    Oscar Joshua akiwa benchi Jumamosi Morogoro baada ya kuumia nyama

    Daktari wa Yanga SC, Sufiani Juma amesema kwamba Oscar aliumia nyama siku hiyo na atakuwa nje hadi Jumamosi atakapoanza mazoezi mepesi.
    Lakini habari njema kwa Yanga SC ni kwamba, kiungo Mbrazil, Andrey Coutinho anaweza kucheza mechi yake ya kwanza ya Ligi Kuu Jumapili- baada ya kuwa fiti kabisa kufuatia kuumia enka katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Polisi Dar es Salaam wiki mbili zilizopita.
    Baada ya kukosa mechi mbili, ya Ngao ya Jamii Yanga SC ikishinda 3-0 na ya kwanza ya Ligi, timu yake ikichapwa mabao 2-0, Coutinho anatarajiwa kuanza tena kazi Jumapili.
    Katika mchezo huo unaotarajiwa kuwa mgumu pia kwa Yanga kulingana na historia ya timu hizo zinapokutana, kocha Mbrazil Marcio Maximo anaweza kumuanzisha beki chipukizi Edward Charles katika sehemu ya Joshua. Maximo ameonekana kumuandaa beki huyo aliyesajiliwa msimu huu kutoka timu ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Ruvu kuziba pengo la Oscar.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: OSCAR JOSHUA KUWAKOSA WAJELAJELA JUMAPILI, MAXIMO AMUANDAA BEKI WA JESHINI KUZIBA NAFASI YAKE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top