• HABARI MPYA

    Wednesday, September 24, 2014

    SIMBA SC ITAMTIBU KIONGERA KWA GHARAMA ZOZOTE AWE FITI AFANYE KAZI, YAJALI KIPAJI CHAKE…HANS POPPE ASEMA NI MKALI KWELI WA MABAO

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    SIMBA SC imekiri mshambuliaji wake, Paul Raphael Kiongera ana matatizo ya goti, lakini mpango wao si kumtema, bali kumtibu vizuri apone kabisa na kucheza tena.
    Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe amesema kwamba mchezaji huyo amefanyiwa vipimo jana na anahitaji tiba pamoja na mapumziko ya wiki sita, lakini baada ya mzunguko wa kwanza Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara atapatiwa tiba zaidi.
    “Tumelijua hilo tatizo, na sisi hatutaki kuwaumiza wachezaji, sisi tutamtibu kwa gharama zozote, kwa sababu tunathamini kipaji chake. Atatusaidia hata msimu ujao,”.
    Simba SC itamtibu Paul Kiongera hadi awe fiti kabisa

    “Kwa sababu kwa sasa hatuna tatizo la mshambuliaji, kama utakumbuka hadi dirisha la usajili linakaribia kufungwa tulikuwa hatuna Okwi (Emmanuel), ni mchezaji aliyekuja kwetu kwa bahati tu, sasa huyo ataziba pengo la Kiongera wakati huu,” amesema Poppe.
    Kapteni huyo wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) amesema kwamba tatizo kubwa la wachezaji wengi wanapoumia wakishauriwa kupumzika huwa hawataki kwa sababu wanapata riziki yao kwa kucheza.
    “Lakini sisi tumejifunza sana matatizo ya wachezaji, mfano Owino (Joseph). Aliumia akaenda kutibiwa India akaambiwa apumzike miezi sita, yeye akaenda kusaini Azam FC akacheza akaumia tena. Ia aliporudi tena India na kutibiwa, akaambiwa apumzike miezi sita, akapumzika. Akapona na sasa yuko fiti kabisa,”ameongeza Poppe.
    Hans Poppe katikati akiwa Muslah Ruwaih kulia na Salim Abdallah kushoto

    Amesema watawekeza kwa kumtibu mchezaji huyo kwa matumaini ya kumtumia baadaye kwa manufaa zaidi. “Huyu mchezaji ni mfungaji hodari, sisi tunajua uwezo wake, sasa tunachokifanya kwa sasa, faida yake itaonekana baadaye,”amesema.    
    Kiongera aliumia katika mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu Jumapili Uwanja wa Taifa, Simba SC ikilazimishwa sare ya 2-2 na Coastal Union, licha ya kuongoza kwa 2-0 hadi mapumziko.
    Kiongera alitokea benchi dakika ya 67, lakini dakika mbili kabla ya filimbi ya mwisho akampisha Amri Kiemba baada ya kuumia, kufuatia kugongana na kipa wa Coastal Union, Shaaban Kado.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC ITAMTIBU KIONGERA KWA GHARAMA ZOZOTE AWE FITI AFANYE KAZI, YAJALI KIPAJI CHAKE…HANS POPPE ASEMA NI MKALI KWELI WA MABAO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top