• HABARI MPYA

    Tuesday, September 23, 2014

    MAFUNZO YAISWEKA LUPANGO MALINDI LIGI KUU ZENJI, YAICHAPA 4-1

    Na Ameir Khalid, ZANZIBAR
    MABAO matatu yaliyofungwa na mchezaji Ali Juma, jioni ya leo yameipa Mafunzo ushindi mzuri wa mabao 4-1 dhidi ya Malindi SC katika mfululizo wa mechi za Ligi Kuu ya soka Zanzibar uwanja wa Amaan.
    Hicho ni kipigo cha pili kwa wakongwe Malindi, baada ya awali kulala mbele ya mabingwa watetezi wa ligi hiyo KMKM kwa kipigo cha mabao 2-0.
    Kwa jumla, Malindi ilicheza chini ya kiwango, na kuruhusu kufungwa bao la kwanza lililowekwa nyavuni na mchezaji Ali Juma katika dakika ya 37 akiunganisha pasi ya Mohammed Abdulrahman, na kudumu hadi wakati wa mapumziko.
    Wachezaji wa Mafunzo wakishangilia moja ya mabao ya leo

    Ali Juma akafunga tena mabao mawili mfululizo dakika ya 54 baada ya piga nikupige langoni kwa Malindi, na dakika ya 60 kwa mkwaju wa penalty.
    Penelti hiyo ilitolewa baada ya Mohammed Abdulrahman kuangushwa ndani ya eneo la adhabu.
    Wachunga wafungwa hao walizidisha mashambulizi na kupachika bao la nne dakika ya 70 kupitia kwa Salum Masoud baada ya kumvisha kanzu mlinda mlango wa Malindi Said Omar.
    Malindi ilifuta machozi kwa bao lao pekee lililoandikwa kitabuni na Salum Masoud  katika dakika ya 62, na katika dakika ya 67  Amour Suleiman akakosa mkwaju wa penelti uliopanguliwa na mlinda mlango Khalid Mahadhi.
    Kesho kutakuwa na mchezo mmoja katika uwanja wa Amaan kati ya Mtende Rangers na washika magendo wa KMKM.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAFUNZO YAISWEKA LUPANGO MALINDI LIGI KUU ZENJI, YAICHAPA 4-1 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top