• HABARI MPYA

    Monday, December 03, 2012

    STARS YATINGA NUSU FAINALI TUSKER CHALLENGE

    Wafungaji wa mabao ya Stars leo, Kiemba kulia na Bocco kushoto wakipongezana

    Na Mahmoud Zubeiry, Kampala
    TANZANIA Bara imefanikiwa kuingia Nusu Fainali ya Kombe la Mataifa ya afrika Mashariki na kati, CECAFA Tusker Challenge baada ya kuilaza Rwanda mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Lugogo mjini hapa mchana huu.
    Hadi mapumziko, Stars walikuwa mbele kwa bao 1-0 lililotiwa kimiani na kiungo Amri Kiemba, dakika mya 33 akiunganisha pasi ya Mwinyi Kazimoto aliyewapunguza wachezaji wawili wa Rwanda kabla ya kutoa pasi maridadi.
    Katika mechi hiyo iliyochezeshwa na refa Mohamed El Fadil kutoka Sudan, mshambuliaji John Raphael Bocco ‘Adebayor’ alikuwa mwiba mchungu kwa safu ya ulinzi ya Rwanda na aliwafanya waende kwenye vyumba vya kupumzikia wakiwa hoi.
    Katika hicho kipindi cha kwanza, Rwanda walikosa bao la wazi dakika ya 12 baada ya krosi ya Jean Claude Iranzi kuokolewa na beki Kevin Yondan kwa kichwa na dakika ya 19 Jean Baptiste Mugiraneza alipiga juu akiwa nje kidogo ya eneo la hatari.
    Stars pamoja na kufunga bao hilo kipindi hicho cha kwanza, katika dakika ya 30 krosi nzuri ya Salum Abubakar ‘Sure Boy’, Mrisho Ngassa na Bocco walishindwa kuiunganisha na ikawapita wote.
    Ngassa tena, katika dakika ya 38 alipiga shuti kali kutoka wingi ya kushoto, lakini likaenda nje sentimita chache.
    Kipindi cha pili,
    Kipindi cha pili Stars walirudi vizuri tena na kuendelea kucheza kwa kuonana, ingawa na Rwanda nao waliendelea kucheza kwa bidii kutafuta bao la kusawazisha.
    Hata hivyo, walikuwa ni Stars tena waliofanikiwa kupata bao la pili 53 baada ya John Bocco kuuwahi mpira uliotemwa na kipa Jean Claude Ndoli kufuatia shuti kali la Mwinyi Kazimoto kutoka nje ya eneo la hatari.
    Baada ya bao hilo, Rwanda walionekana kupagawa, lakini hawakusahau kushambulia lango la Stars na dakika ya 86 Dadi Birori hakujali ameotea akasukuma mpira nyavuni, lakini refa akakataa bao hilo.
    Kwa ushindi huo, Stars sasa inasubiri mshindi kati ya Uganda na Ethiopia kesho kukutana naye kwenye Nusu Fainali.
    Stars; Juma Kaseja, Erasto Nyoni, Amir Maftah, Shomary Kapombe, Kevin Yondan, Amri Kiemba, Salum Abubakar/Athumani Iddi dk51, Frank Domayo, Mwinyi Kazimoto, Mrisho Ngassa na John Bocco/Shaaban Nditi dk 85.
    Rwanda; Jean Claude Ndoli, Emery Basiyenge, Ismail Nshutimayamangara/Fabrice Twagizimana dk19, Jimmy Mbaraga/Imran Nshiyimana dk67, Charles Tibingana/Barnabe Mbuyumbyi dk61, Michel Rusheshangoga, Jean Baptiste Mugiraneza, Haruna Niyonzima, Jean Claude Iranzi, Dadi Birori na Tumaine Ntamuhanga.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: STARS YATINGA NUSU FAINALI TUSKER CHALLENGE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top