SAMSON MFALILA, Gazeti la Mwanaspoti
KOCHA wa Azam, Stewart Hall amelia na wadau
wa Simba na Yanga wanavyoipiga vita timu yake, ambayo imeibuka kuwa kigogo cha
Ligi Kuu Tanzania Bara.
Akizungumza na Mwanaposti katika mahojiano
maalumu, Hall anasema anashangazwa na mashabiki hasa wa Simba na Yanga kwa
kuijengea chuki timu yake kutokana na kutishia ubabe wao.
Hall anaonya kuwa tabia ya wadau wa Simba
na Yanga wanaotaka kuona ligi ya Tanzania ikitawaliwa na timu mbili zao tu kitu
ambacho si sahihi kwa maendeleo ya soka.
"Timu hizi zimekuwepo kwa miaka mingi
sana lakini nashangaa zimeshindwa kusaidia kukuza soka la Tanzania.
"Ninachokiona katika soka la Tanzania
kinanisikitisha na kinachonikera zaidi wameingia watu makini wa Azam, ambao
wameingiza fedha lakini wanapigwa vita," anasema Hall, ambaye ni raia wa
Uingereza.
Anasema Watanzania wanapaswa kuruhusu
ushindani na kutolea mfano Ligi Kuu Scotland inavyoshindaniwa na timu mbili tu
za Rangers na Celtic na kufanya soka la sehemu hiyo kuwa chini.
Ligi Kuu Tanzania Bara
Hall anasema anafurahia timu yake kushika
nafasi ya pili kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara ikiwa miaka chache tangu
kuanzishwa kwake.
Anaeleza ni kitu kizuri kuona timu yake
iliyoanzishwa mwaka 2004, imeipiku Yanga iliyoasisiwa katika miaka ya 1930.
Azam safari hii imenyakua nafasi ya pili na
mwakani itashiriki katika mashindano ya Kombe la Shirikisho.
Hall anaonya Watanzania wanapaswa
kubadilika kama kweli wanataka soka la nchi hii ibadilike.
Anasema kuwa Shirikisho la Soka Tanzania
(TFF) linatakiwa kuwa makini katika kuendesha katika ligi hiyo.
Analalamikia vitendo vya rushwa kwenye ligi
hiyo na viwango duni vya uchezeshaji miongoni mwa waamuzi.
Hall anaeleza kuwa anashangaa kuona rushwa
na upangaji matokeo vinakubalika kama sehemu ya soka la Tanzania.
"Ni hatari kwa soka la nchi yenu kama
mtakubali masuala ya upangaji matokeo," anasema Hall, ambaye timu yake
ililazimika kurudiana na Mtibwa kwenye mzunguko wa pili baada ya mechi ya
kwanza kukatizwa kutokana na makosa ya mwamuzi Rashid Msangi.
Pia mechi za Yanga na Polisi Dodoma
zilimalizika kwa waamuzi kupigwa kutokana na timu hizo kudai mwamuzi alikuwa
anaibeba Azam.
Kocha huyo anakanusha vikali madai hayo na
kudai kuwa watu wanaionea wivu tu timu yake kutokana na kuwa na fedha nyingi.
Hall anasema TFF kwa kushirikiana na wadau
wa soka la Tanzania wanapaswa kupiga vita kwa nguvu zote masuala ya rushwa.
Anatahadharisha ni ndoto kwa timu za
Tanzania kufanya vizuri kwenye michuano ya kimataifa kama wadau wa soka
watakumbatia rushwa kama sehemu ya soka la Tanzania.
Anasema wapangaji matokeo wanapaswa
kuchukua hatua kali kama Marseille ya Ufaransa ilivyoadhibiwa mwaka 1993 baada
ya kubainika ilikuwa inanunua baadhi ya mechi za Ligi Kuu Ufaransa au ile
kashfa ya upangaji matokeo ya Italia iliyokuja kujulikana kwa jina la
Calciopoli.
Anaonyesha kuwa ubaya wa timu kununua mechi
unasababisha Tanzania kuwakilishwa na timu dhaifu kwenye michuano ya Afrika.
"Bwana mwandishi jiulize, timu gani ya
Tanzania imetwaa kutwaa taji la Afrika? Jibu linafahamika na ni wazi kuwa
linasababishwa na rushwa ndani ya Ligi Kuu," anaeleza Hall, ambaye amewahi
kuwa Mkurugenzi wa Ufundi wa Birmingham.
Hall, hata hivyo, anadai anategemea
ushindani mkali zaidi msimu ujao kwenye Ligi Kuu kwani ameona timu kama Mtibwa
na Coastal Union ziko juu.
Mashabiki wa Simba na Yanga
Hall anaeleza pia mashabiki wa Simba na
Yanga kwa kiasi kikubwa nao wanachangia kwa kiasi kikubwa kuvuruga soka la
Tanzania.
Anasema mashabiki hao wanaweka presha kubwa
kwa wachezaji na viongozi wa soka kuhakikisha timu zao zinashinda.
Hall anatolea mfano vurugu za mechi ya
Yanga na Azam kuwa zilichangiwa zaidi na viongozi na mashabiki wa Yanga kuwapa
shinikizo wachezaji wao kushinda.
"Unajua tulikuwa tumeifunga Yanga mara
kadhaa, sasa safari hii wakaona hapana wanapaswa kushinda kwa njia zozote. Basi
baada ya kuona mambo hayaendi vizuri wakampiga mwamuzi," anasema Hall,
ambaye pia ni Mshauri wa Ufundi wa timu ya Zanzibar.
Hall anasema anaelewa mashabiki wa soka wa
Tanzania wamegawanyika kushabikia timu hizo lakini amesema zinapaswa
kubadilika.
Anaeleza mashabiki wa timu hizo wanapaswa
kuhakikisha timu zao zinaendeshwa kisasa zaidi ndani na nje ya uwanja badala ya
kuendekeza siasa za nje ya uwanja.
Hall anaeleza kutokana na presha na wingi
wa mashabiki wa Simba na Yanga kumefanya wababaike wanapochezesha mechi za
baina ya timu hizo.
Pia ameponda mashabiki hao kwa kukosa
uzalendo na kuzishabikia timu za kigeni zinapokuja kucheza Tanzania.
"Nimefundisha soka katika nchi
mbalimbali duniani lakini sijawahi kuona timu ya kigeni inashabikiwa,"
anasema Hall.
Katika miaka ya karibuni, imekuwa kitu cha
kawaida kwa mashabiki wa Simba na Yanga kushangilia timu za kigeni zinapocheza
na mahasimu wao.
Hall anasema ameshangazwa kuwa tabia hiyo
imeingia katika timu ya taifa.
"Mashabiki wa Simba na Yanga wanaua
soka lenu kwani wameingiza siasa zao kwenye timu ya taifa," anaeleza Hall,
ambaye alikuwa anazungumzia vituko vya Kombe la Chalenji mwaka jana wakati mashabiki
wa Yanga walipokuwa wanaizomea timu ya Bara kutokana na kuwa na wachezaji
wachache wa Yanga.
Pia anatolea mfano jinsi mashabiki hao
walivyokuwa wanamsakama mshambuliaji wake John Boko na kumfanya ajitoe kwenye
kikosi cha timu ya taifa.
"Boko ni mchezaji mdogo sana lakini
ameacha kuchezea Stars kutokana na kujengewa chuki na mashabiki hawa. Watu hawa
wanaua soka la Tanzania," anaeleza Hall.
Pia anaeleza kuwa mashabiki hao wamejenga
chuki kubwa dhidi ya timu yake kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa na
matajiri wa timu hiyo.
Azam imejenga uwanja na hosteli ya
wachezaji na ina mfumo mzuri wa timu kuanzia watoto wenye umri wa miaka 12.
Pia wachezaji wa timu hiyo wanaangaliwa
vizuri kwa kulipwa mishahara na marupurupu kwa wakati.
"Mimi nilitegemea kuwa mashabiki hawa
wangetuunga mkono na kushinikiza viongozi wao kubadilika na kuendesha timu zao
vizuri lakini badala yake wanatupiga vita," anaeleza Hall kwa mshangao.
Hall anatoa mwito kwa wadau wa soka la
Tanzania kuiangalia Azam kama kioo cha soka la Tanzania badala ya kuichukulia
kama adui.
Maendeleo ya Azam
Hall anaeleza kuwa anasema licha ya
changamoto za waamuzi lakini anapongeza timu yake kwa kushika nafasi ya pili
nyuma ya Simba iliyotwaa ubingwa.
Amesema amefurahia kuona malengo yao
yametimia msimu kwani walikuwa wanataka kuvunja ubabe wa Simba na Yanga kwenye
Ligi Kuu Tanzania Bara.
"Lengo letu kubwa lilikuwa kushika
nafasi mbili za juu, kitu ambacho tumefanikiwa kwa kiasi kikubwa.
"Sasa msimu ujao tunataka kupigania
ubingwa jambo ambalo ninaamini tuna ubavu nalo," aliongeza Hall, ambaye
amewahi kuzifundisha timu za taifa za St.Vincent, Grenada na Pune ya India.
Hall anafichua kuwa timu hiyo imeandaa
programu ya miaka 10 yenye lengo la kuifanya timu hiyo kuwa miongoni mwa timu
kubwa Afrika.
"Tunataka tufikie hatua kutoa upinzani
kwa timu kama TP Mazembe au Al-Ahly ya Misri," anaongeza Hall.
Amesema kuwa anasikitishwa na kuona timu
yake inapigwa vita na wadau wa soka.
Hall anasema kutokana na haya yanayowakuta
Azam yatafanya watu wengine wenye fedha kuogopa kuingiza fedha zao kwenye soka.
"Unajua kuna watu wanaangalia
tunayofanya sasa watu wenye fedha zao wakishuhudia jinsi Azam inavyonyanyasika
basi hawatataka kushiriki katika mchezo huu," anasema Hall, ambaye
anaongeza fedha ni muhimu kwa maendeleo ya soka.
|
NFL Odds: Patriots, Panthers Are Underdogs and 49ers Are Favored in Every
Game in '24
-
Oddsmakers are expecting long NFL seasons in New England and Carolina. The
Patriots and Panthers are listed as underdogs in each of their 17 games
next sea...
22 minutes ago
0 comments:
Post a Comment