• HABARI MPYA

    Friday, May 11, 2012

    MAN CITY NA MAN UNITED MSIMU HUU ZAKUMBUSHIA VITA YA 2010 FERGUSON NA CHESLEA


    Moja ya mechi zilizoikutanisha City na United msimu huu

    MSIMU huu wa Ligi Kuu ya England, unatarajiwa kufungwa Jumapili, huku macho ya wengi yakiwa kwenye mechi mbili zinazozihusu timu mbili kutoka Jiji moja, Manchester.
    Timu hizo, Manchester City na Manchester United, mojawapo itatawazwa kuwa bingwa Jumapili- lakini City wanapewa nafasi kubwa zaidi.
    Zikiwa zinalingana kwa pointi, City inajivunia hazina yake kubwa ya mabao, ikiwa inaizidi mabao nane United.
    City itamalizia nyumbani na QPR, ambayo inapigana kuepuka kushuka daraja wakati United itamaliza na Sunderland.
    Mark Hughes na kikosi chake wameahidiwa pauni Milioni 1 na mmliki wa klabu hiyo, iwapo wataifunga au japo kutoka sare na City.
    Hughes alikuwa kocha wa City, kabla ya kufukuzwa na nafasi yake kupewa Roberto Mancini- na watu sasa wanasubiri kuona kama atalipa kisasi cha kufutwa kazi ‘kinyama’?
    Sahau kuhusu hayo- ana kibarua cha kuinusuru timu yake kushuka daraja, maana yake mechi hiyo kila timu itapigana kufa na kupona, City ikiwania ubingwa na QPR ikitaka kubaki Ligi Kuu.
    Tayati Sir Alex Ferguson amekwishakata tamaa, akisema City inachukua ubingwa, hali ambayo ni tofauti na wiki tatu zilizopita, wakati United lipokuwa ikipewa nafasi kubwa kabla ya kuteleza na kuiachia tena City kupaa juu.
    Msimu huu wa Ligi Kuu unakaribia kufanana na msimu wa 2009/2010 ambao bingwa alipatikana katika mechi ya mwisho, United tena wakipigana na Chelsea.
    Chelsea iliizidi pointi moja tu United (86-85), lakini hadi timu hizo zinaingia kwenye mechi za mwisho Mei 9, 2010 zilikuwa zinalingana kwa wastani wa mabao (GD 24).
    Chelsea iliifunga 8-0 nyumbani Wigan na United ilishinda nyumbani pia 4-0 dhidi ya Stoke City.
    United walikuwa wanaiombea Chelsea ilazimishwe sare na Wigan na wao waifunge Stoke- lakini duwa la kuku halikumpata mwewe na hapana shaka kwa kukumbuka hilo, sasa Ferguson amekubali kupokea Medali ya Fedha.
    Yatokee maajabu, labda City ipate ushindi mwembamba wa 1-0 na ili United iwe bingwa inahitaji kushinda 10-0 dhidi ya Sunderland.
    Haitakuwa ajabu kwa United kupata ushindi huo mnono, ikiwa msimu huu iliifunga mabao nane timu bora katika ligi hiyo, Arsenal.
    Lakini pia katika soka timu au wachezaji hujituma kulingana na mahitaji- kama suala ni ushindi tu timu inaweza kuridhika baada ya kutikisa nyavu za wapinzani mara mbili au tatu.
    Lakini kama suala ni idadi ya mabao, tumeshuhudia mara kadhaa timu zikipigania hilo na bila kwenda mbali hata hapa Tanzania ishatokea, Simba iliwahi kufungwa 4-0 nyumbani na Mufurila Wanderers ya Zambia, ikaenda kushinda 5-0 ugenini mwaka 1978- au Arsenal na AC Milan katika Ligi ya Mabingwa msimu huu.
    Ligi ya England ni tamu na itazidi kujikusanyia wapenzi kutokana na upinzani wake- kwani katika wakati huu ambao tayari La Liga, Bundesliga, Serie A zimekwishapata mabingwa wake- England mambo yote yatajulikana baada ya kipyenga cha mwisho cha msimu.

    ZILIVYOMALIZA CHELSEA NA UNITED 2009/2010:
                                   P    W   D    L     GD  Pts
    1.Chelsea                   38   27   5    6     32   86  
    2.Manchester United     38   27   4    7     28   85 

    ZINAVYOKABANA MSIMU HUU CITY NA UNITED
    P    W   D    L     GD Pts
    1 Man City           37   27   5    5    63   86
    2 Man Utd           37   27   5    5    55   86

    Tathmini hii imeandikwa na Mahmoud Zubeiry wa BIN ZUBEIRY blog usiku huu.



    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAN CITY NA MAN UNITED MSIMU HUU ZAKUMBUSHIA VITA YA 2010 FERGUSON NA CHESLEA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top