• HABARI MPYA

    Friday, January 23, 2009

    YANGA SC: Mabingwa wenye ari mpya na Kilimanjaro Premium Lager

    KLABU bingwa ya soka Tanzania, Yanga ya Dar es Salaam, Agosti 18 mwaka 2008 ilipokea habari njema nyingine, ambayo ni kupata mdhamini mpya, bia ya Kilimanjaro Premium Lager, inayozalishwa na kampuni ya Bia Tanzania (TBL).
    Udhamini huo wa Kilimanjaro, unaifanya Yanga iwe na neema zaidi, kwani tayari ina mdhamini mwingine, ambaye ni kampuni ya Quality Group Limited, inayomilikiwa na Yussuf Mehboob Manji.
    Manji ni zaidi ya mdhamini Yanga, kwani pia amekuwa akitoa misaada mingi nje ya mkataba wake na klabu hiyo, hiyo zaidi ikitokana na mapenzi yake ya damu kwa klabu hiyo.
    Mkataba huo wa Kilimanjario, wenye thamani ya Sh. Bilioni 3, utakaodumu kwa miaka mitatu, ikiwa kila mwaka Kilimanjaro itakuwa ikitoa Sh. Bilioni 1, kwa klabu hiyo kwa ajili ya shughuli za uendeshaji wa timu.
    Mapema tu wakati wa hafla ya uzinduzi wa mkataba huo, iliyofanyika Agosti 18, mwaka huu kwenye hoteli ya Movenpick, Dar es Salasam, Kilimanjaro Premium Lager ilitoa hundi ya sh. 25,000,000 kwa klabu hiyo, ikiwa ni mwanzo wa utekelezaji wake.
    Akitoa mchanganuo wa mkataba huo, Meneja wa Bia ya Kilimanjaro, Oscar Shelukindo alisema kwamba klabu hiyo itavuna sh. Milioni 16, kila mwezi kwa ajili ya mishahara ya wachezaji, hiyo ikiwa ni mbali na kupatiwa basi dogo la kusafiria wachezaji.
    Shelukindo alisema kwamba, Kilimanjaro Premium Lager maarufu kwa jina la ufupi kama Kili, imeamua kuisaidia klabu hiyo, kwa sababu ina mwelekeo wa kweli wa kuendeleza soka ya Tanzania.
    Aidha, Kili pia itatoa zawadi kwa timu hiyo iwapo itafanikiwa kushika moja ya nafasi mbili za juu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, ikiwa bingwa itapata Sh. Milioni 25 na ikishika nafasi ya pili, itapewa Sh. Milioni 15.
    “Tunaamini kwa kufanya hivi, tutaiongezea morali klabu hii, italeta ushindani wa kweli kwenye ligi, kwa sababu mkataba huu unawanufaisha wachezaji moja kwa moja, watapata mishahara na posho kwa wakati mwafaka,”alisema Shelukindo.
    Alisema Yanga pia, maarufu kama Watoto wa Jangwani, itapewa vifaa vya thamani na vya kisasa vya michezo, lengo likiwa ni kuifanya iwe bora na mfano wa kuigwa katika ligi hiyo.
    Kilimanjaro Premium Lager, pia imetoa udhamini kama huo kwa klabu ya Simba.
    Akizungumzia neema hiyo, Mwenyekiti wa Yanga, Wakili Imani Madega alisema kwamba, hiyo ni hatua nyingine kubwa ya maendeleo ya klabu hiyo, chini ya uongozi wake, ulioingia madarakani Mei mwaka jana.
    Madega alisema kwamba udhamini huo umekuja katika wakati ambao ni mwafaka, klabu yake ikihitaji wadhamini zaidi, ili kujipatia fedha za kuweza kuendesha Yantga kwa ufanisi.
    Yanga ambayo jina lake halisi ni Young Africans, ni klabu nyingine kongwe nchini, ukiacha Simba ambayo hutumia jezi za rangi ya kijani na njano.
    Yanga ina mengi kiasi ya kujivunia kwenye soka ya kimataifa nayo, kubwa zaidi ikiwa ni klabu ya kwanza kucheza michuano ya Afrika, mwaka 1969 na kutolewa kwenye hatua ya Robo Fainali.
    Mwaka huo, Yanga ilianza vizuri raundi ya kwanzan ikiitoa Fitaridandro ya Madagascar kwa jumla ya mabao 4-3, ikishinda 4-1 nyumbani, kabla ya kwenda kufungwa 2-0 ugenini.
    Katika raundi ya pili, Yanga ilikutana na St. Georges ya Ethiopia, ambayo kwa sasa inanolewa na Mserbia, Milutin Sredojevic ‘Micho’, na mcherzo wa kwanza mjini Addis Ababa, timu hizo zilitoka sare ya bila kufungana na ziliporudiana Dar es Salaam, Watoto wa Jangwani walishinda 5-0.
    Katika Robo fainali, mechi ya iliyocheza mjini Kumasi, kati ya Yanga Asante Kototo ya Ghana na iliyochezwa Dar es Salaam, zote matokeo yalikuwa ni timu hizo kufungana bao 1-1.
    Kwa sababu hiyo, ilipigwa kura ya kurushwa sarafu juu, ili kupata timu ya kusonga mbele kwenda Nusu Fainali na hapo ndipo Kotoko ilipobahatika kupata tiketi ya kucheza mechi iliyofuata.
    Mwaka 1970, Yanga ilirejea na makali yake kwenye michuano hiyo na kufanikiwa kufika tena Robo Fainali, ambako ilikutana na Kotoko tena.
    Mechi ya kwanza mjini Dar es Salaam, timu hizo zilitoka sare ya kufungana bao 1-1 na marudiano matokeo yalikuwa ni sare tena ya bila kufungana, hivyo mchezo kusogea kwenye muda wa nyongeza.
    Hata hivyo, kutokana na giza kutawala uwanjani, ililazimika mechi hiyo kuvunjika dakika ya 19 ya muda wa nyongeza kabla ya kuhamishiwa kwenye Uwanja huru mjini Addis Ababa, Ethiopia.
    Katika mechi hiyo ya tatu, Yanga walikubali kipigo cha mabao 2-0 na kutolewa kwenye hatua hiyo dhidi ya wapinzani wale wale,Kotoko.
    Zaidi ya hapo, mafanikio mengine makubwa kwa Yanga kwenye michuano hiyo ni kufika Robo Fainali kwa mara ya tatu, mwaka 1998. Lakini safari hiyo Robo Fainali ilichezwa kwa mtindo wa Ligi, mfumo ulioanza kutumika mwaka 1997.
    Yanga iliitoa Rayon ya Rwanda katika raundi ya kwanza, Coffee ya Ethiopia katika Raundi ya Pili, hivyo kukata ya kuycheza Ligi ya Mabingwa Afrika, ikiandika historia ya kuwa timu ya kwanza ya Tanzania kucheza michuano hiyo.
    Aidha, Yanga mbali na kujivunia kutoa mchezaji wa kwanza kucheza soka ya kulipwa Ulaya, Sunday Manara, pia inajivunia kuwa klabu pekee iliyotoa mchezaji aliyecheza kwa mafanikio zaidi barani Ulaya, huyo si mwingine zaidi ya Nonda Shabani ‘Papii’.
    Nonda, ambaye kwa sasa anacheza Galatasaray ya Uturuki, baada ya kuwika FC Zurich ya Uswisi, Rennes, Monaco za Ufaransa AS Roma ya Italia na Blackburn ya England, kisoka haswa ‘alizaliwa’ Yanga ambako aliibuliwa kutoka kwenye kikosi cha pili.
    Aliingia Tanzania miaka ya 1990 kama mkimbizi akitokea Burundi na mwaka 1995 alikuwa kwenye kikosi cha pili cha Yanga, Black Stars kilichokuwa kikisukwa na Tambwe Leya (sasa marehemu). Mwaka uliofuata alipandishwa kikosi cha kwanza, sambamba na nyota wengine aliokuwa Black Stars.
    Mwaka 1996, Nonda alinunuliwa na Vaal Professionals ya Afrika Kusini, ambako hata kabla hajatimiza mwaka, alinunuliwa na Zurich.
    Yanga iliyotwaa mara tatu taji la Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame katika miaka ya 1975, 1993 na 1999 msimu ujao tena itashiriki Ligi ya Mabingwa Afrika kwa mara ya sita, tangu mwaka 1997 ilipoanzishwa michuano hiyo.
    Mwaka 1997 ilitolewa Raundi ya awali, 1998 ilifika hatua ya makundi, 2001 ilitolewa raundi ya pili, 2006 ilitolewa raundi ya kwanza na 2007 ilitolewa raundi ya pili, ikaangukia kwenye kapu la kuwania kucheza Kombe la Shikrikisho.
    Yanga iliyotwaa mara moja tu Kombe lingine la Afrika Mashariki, Tusker mwaka 2007, imeweza kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania mara 15, katika miaka ya
    1968, 1969, 1970, 1971, 1974, 1981, 1983, 1987, 1991, 1996, 1997, 2000, 2005, 2006 na 2008, wakati lililokuwa Kombe la Nyerere imetwaa mara tatu katika miaka ya 1975, 1994 na 1999.
    Naam, hiyo ndiyo Yanga, klabu inayokuja na makali mapya baada ya kupata udhamini wa bia ya Kilimanjaro Premium Lager.

    REKODI ZA YANGA:
    UBINGWA WA LIGI KUU:
    Imechukua mara 15, miaka ya 1968, 1969, 1970, 1971, 1974, 1981, 1983, 1987, 1991, 1996, 1997, 2000, 2005, 2006 na 2008.

    LILILOKUWA KOMBE LA NYERERE:
    1975, 1994 na 1999.

    KOMBE LA KAGAME:
    1975, 1993 na 1999.

    KOMBE LA TUSKER:
    2007.

    KIKOSI CHA YANGA 2008:
    MAKIPA:
    Obren Curkovic
    Juma Kaseja
    Steven Marashi

    MABEKI:
    Wisdom Ndlovu
    Abubakar Mtiro
    Shadrack Nsajigwa
    Hamisi Yussuf
    Fred Mbuna (Nahodha)
    George Owino
    Nadir Haroub
    Nurdin Bakari

    VIUNGO:
    Abdi Kassim
    Credo Mwaipopo
    Mrisho Ngasa
    Amir Maftah
    Athumani Iddi
    Shamte Ally
    Kigi Makasi
    Geoffrey Bonny
    Castory Mumbara
    Razack Khalfan
    Ally Msigwa

    WASHAMBULIAJI:
    Jerry Tegete
    Boniphace Ambani
    Gaudence Mwaikimba
    Vincent Barnabas
    Benard Mwalala
    Maurice Sunguti
    Mike Barasa
    Iddi Ally Mbaga
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC: Mabingwa wenye ari mpya na Kilimanjaro Premium Lager Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top