• HABARI MPYA

    Thursday, January 22, 2009

    DEO MUNISHI: DIDA WA MSIMBAZI


    DEO MUNISHI:

    Dida wa Simba aliyekifuata kivuli cha Kaseja

    ..alicheza ligi nne, timu nne ndani ya mwaka mmoja

    “KILA mechi ninayocheza najiona mpya katika soka, kwani nimeweza kuwa katika hali ya kurekebisha makosa yanayotokea katika michezo ya nyuma yake”.
    Amecheza mechi tatu tu za Ligi Kuu ya Tanzania, lakini ameweza kumashawishi kocha mkuu wa timu ya taifa, Marcio Maximo kumuita katika kikosi cha timu yake kujiandaa na mchezo wa jana dhidi ya Cape Verde.
    Umbo lake limeweza kumshawishi kocha wake, Krasimir Bezinski kumuamini na kumpa nafasi ya kucheza katika mechi tatu za Ligi Kuu ambazo aliweza kupumzisha mawazo ya wanachama na mashabiki wa Simba.
    Anaitwa Deogratius Bonaventure Munishi ambaye wengi humuita Dida, wakimlinginisha na Nelson Dida kipa wa timu ya taifa ya Brazil anayecheza katika timu hiyo na klabu yake ya AC Milan ya Italia.
    Ingawaje umekuwapo utata juu ya jina lake, lililoandikwa hapo juu ndilo sahihi kwani Deo Mushi aliitwa kimakosa wakati anasajiliwa Manyema, ilitokea kiongozi mmoja kukosea herufi za jina lake la mwisho.
    Urefu wake wa wastani unaoruhusiwa kuwa kipa ulimwezesha kujiunga na mpira wa miguu na moja kwa moja kuchagua nafasi hiyo badala ya 10 zilizobaki uwanjani.
    “Hata watu waliokuwa wakioniona awali walipendekeza niwe kipa ili niweze kuzuia vyema hasa mipira ya juu, nashukuru tokea wakati huo nimeweza kucheza katika kiwango kinachoniruhusu kucheza,” anasema Dida.
    Ukimuangali kwa mbali waweza kukisia kama ana umri mkubwa, lakini ukweli ni kuwa hajatimiza jata miaka 20, lakini uwezo alionao umeweza kupunguza mawazo ya ana Simba baada ya kuondokewa na aliyekuwa kipa wake namba moja, Juma Kaseja, aliyejiunga na Yanga.
    Lakini kutokana ‘siasa’ za soka za Tanzania, anaonekana kama kuwa namba moja katika timu yake kutokana na kufukuzwa kwa kipa Amani Simba aliyesajiliwa ili kuziba pengo la Kaseja.
    “Siwezi kukubali kama mimi ni namba moja sababu sijaambiwa kitu kama hicho, lakini kama ndivyo nipo tayari kupokea kwa mikono miwili hali hiyo,” anasema Dida aliyewahi kubeba mipira ya Simba katika mazoezi ya timu hiyo miaka michache iliyopita wakati inafanya mazoezi katika Uwanja wa Chuo Cha Polisi Kurasini.
    Anasema kitu pekee kinachomfanya kuwa na uwezo wa kudaka vizuri siku zote ni, utiifu wake katika mazoezi ya timu yake sambamba na yale binafsi anayofanya nje ya Simba.
    Wakati anasajiliwa Simba aliwakuta makipa wawili, Juma Kaseja na Ali Mustapha ‘Barthez’ lakini hakuwa na shaka, kwani aliamini katika methali isemayo ‘Mvumilivu Ula Nyama Mbichi’, hii ilikuja kuthibitika baada ya Kaseja kuamia Yanga.
    “Sikuogopa kusaini Simba eti kwa sababu yupo Kaseja na Barthez, niliamini nami nina siku yangu katika mpira ambayo sasa imejidhihirisha hivyo,” anasema Dida.
    Alisajiliwa Simba katika usajili wa dirisha dogo Novemba mwaka jana na kufanikiwa kucheza mechi moja tu ya msimu uliopita wa Ligi Kuu ya Tanzania. Huo ulikuwa ulikuwa ni mchezo dhidi ya Polisi Dodoma uliochezwa katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na matokeo kuwa sare ya mabao 2-2.
    “Sikufurahi kucheza mchezo wangu wa kwanza Simba na kutoka sare, unajua kila mchezaji anatamani anapocheza mechi ya kwanza katika timu mpya apate ushindi mnono ili awe na kumbukumbu nzuri maishani mwake,” anasema Dida.
    “Nafurahi angalau mwaka huu katika mechi saba tulizocheza mpaka sasa, nimecheza tatu ambazo mbili tumlishinda na moja tulipoteza,” anasema Dida.
    Mchezo wake wa kwanza katika Ligi Kuu msimu wa 2008/09, ulikuwa dhidi ya Villa Squad ya Kinondoni, katika mchezo huo Simba ilishinda mabao 4-1 na kuanza vyema harakati zake za kuwania ubingwa wa Tanzania.
    Alikuwamo katika kikosi cha Simba kilichoifunga Mtibwa 1-0 na kufufua matumaini ya kufanya vizuri katika Ligi Kuu, lakini alikumbana na balaa la kufungwa mabao mawili yalikosa majibu katika mchezo dhidi ya Azam FC amba Simba ilifungwa 2-0.
    “Ninachoamini mimi tulifungwa kwa sababu za makosa ya kimchezo na hakuna jambo lingine nje ya uwanja lililosabaisha kufungwa kwetu,” anasema Dida.
    Baada ya kuonyesha uwezo mkubwa katika mechi chache alizocheza Simba mwaka huu, ameitwa katika kikosi cha timu timua ya taifa ‘Taifa Stars’.
    “Ni kipa chipukizi …na kama ilivyo sera yangu ya kuwainua wachezaji vijana, nimemuita katika kikosi changu ili kukuza kipaji chake ili awe tegemeo la taifa siku za usoni.
    Anahitaji muda kidogo ili aweze kupata nafasi kikosi cha kwanza, lakini kwa siku chache nilizokaa naye anaonekana kuwa mpokeaji mzuri wa mazoezi,” anasema Maximo alipoulizwa kuhusu uwajibikaji wa Dida katika kikosi cha Stars.
    Dida aliyezaliwa mwaka 1989 Moshi, Kilimanjaro katika familia ya Mzee Bonaventure Munishi na mama Hilda Temu akiwa ni mtoto wa pili katika familia hiyo ya watoto wanne. Nduguze ni Ismail, Kasija na George.
    Alisoma Madenge shule ya msingi kuanzia mwaka 1996 mpaka 2002 kisha kujiunga na Makongo sekondari mwaka uliofuata lakini alisoma kwa mwezi mmoja tu na kujikita katika soka.
    Alianza kucheza soka mwaka 1993 katika viwanja vya Temeke msikiti wa Tungi kisha alijiunga na timu ya Temeke Kids mwaka 2000 iliyokuwa chini ya Kocha Tunge na kufanya mazoezi katika viwanja vilivyokuwapo jirani ya Uwanja wa Taifa wa zamani (sehemu hiyo sasa imemegwa na Uwanja Mkuu wa Taifa).
    Mwaka 2004 alisajiliwa na Coastal Union ya Tanga na kucheza Ligi daraja la kwanza, mwaka uliofuata alijiunga na timu ya Chuoni ya Zanzibar iliykuwa ikishiriki Ligi daraja la kwanza visiwani humo.
    Mwaka uliofuata alijiengua katika timu hiyo na kurudi Dar es Salaam na kuendelea kujifua katika viwanja vya tungi Temeke. Februari 2007 alijiunga na timu ya Makondeko ya Temeke na kuhsiriki Ligi ya taifa, lakini Machi mwaka huohuo alijiunga na Mkunguni ya Ilala kushiriki Ligi ya Taifa pia.
    Hapo hakuka sana kwani Aprili, 2007 alijiunga na Manyema kucheza Ligi daraja la kwanza na kufanikiwa kuipandisha timu hiyo mapak Ligi Kuu, ndipo Simba ilipomuona na kumsajili mwezi Novemba mwaka huo huo kutokana na uwezo aliouonyesha katika timu hiyo.
    Hii ina maanisha alicheza ligi nne na timu nne ndani ya mwaka mmoja tu wa 2007.
    “Nataraji kuongeza elimu yangu na kucheza katika timu kubwa nje ya bara la Afrika kwa maslahi,” anamaliza Dida.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: DEO MUNISHI: DIDA WA MSIMBAZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top