• HABARI MPYA

    Wednesday, September 12, 2018

    NAHODHA WA TAIFA STARS MBWANA SAMATTA SASA ANAFIKIRIA KUMILIKI NDEGE BINAFASI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    NAHODHA wa Tanzania, Mbwana Samatta anayechezea KRC Genk ya Ubelgiji amesema kwamba anaanza kupambana ili atimize ndoto za kumiliki ndege binafsi.
    Samatta ameposti picha akiwa kweye mlango wa ndege binafasi ya klabu yake, Genk na kuandika; “Ndoto za kumiliki ndege binafsi zimeanza baada ya kupiga picha hii, siyo kila ndoto inaweza kutimia. Ila, acha vita ianze,”.
    Samatta amerejea Ulaya baada ya Jumamosi kuichezea Taifa Stars mechi ya Kundi L kufuzu Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwakani nchini Cameroon ikilazimisha sare ya 0-0 na wenyeji, Uganda Jumamosi Uwanja wa Mandela, Namboole mjini Kampala.
    Mbwana Samatta amesema kwamba anaanza kupambana ili atimize ndoto za kumiliki ndege binafsi



    Lakini Samatta amerejea Ubelgiji akiwa hana furaha baada ya kukosa bao la wazi Jumamosi Namboole kiasi cha kulazimika kuwaomba radhi Watanzania, akisema kwamba hakuwa na bahati siku hiyo, kwani amekuwa akifunga mabao katika mazingira magumu mno, lakini siku hiyo alishindwa kutumia nafasi nyepesi.
    “Mimi ninafikiri huwa nakuwa sina shaka na ubora wangu hususan za ufungaji. Na kitu ambacho nilikuwa nacho pale ni kwamba naenda kufunga, hiyo ilikuwa haina shaka kwamba naweza kufunga. Na ilikuwa ni nafasi nyepesi ukilinganisha na nafasi nyingine ambazo huwa ninafunga,”. 
    “Kwa hiyo naweza kusema sikuwa na bahati labda, inaweza kuwa hivyo ilitokea (juzi) bahati mbaya sijafunga, lakini ninadhani ni kitu ambacho kiliniumiza sana kwa sababu ni nafasi ambayo nilikuwa nikiitafuta katika mchezo mzima niweze kuipata, lakini baada ya kuipata nikashindwa kuitumia,”.
    Samatta alisema kwamba si kitu kizuri kwa mshambuliaji kupoteza nafasi nzuri za aina ile na ndiyo maana usiku wa kuamkia jana hakupata usingizi akikesha anafikiria nafasi ile na kujutia kwa kuipoteza.
    “Siyo kitu kizuri kwa mshambuliaji, ni kitu ambacho kwa kweli kilinifanya nisipate usingizi usikuwa jana (juzi) nikijaribu kuikumbuka ile nafasi nikijaribu kuitafuta kuiangalia, kuirudia rudia nione ni wapi nilishindwa na kwa nini ilikuwa vile,”alisema Samatta aliyejiunga na KRC Genk Januari mwaka 2016 akitokea TP Mazembe ya DRC, ambayo nayo ilimnunua Simba SC ya nyumbani, Tanzania. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NAHODHA WA TAIFA STARS MBWANA SAMATTA SASA ANAFIKIRIA KUMILIKI NDEGE BINAFASI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top