• HABARI MPYA

    Friday, September 21, 2018

    BODI YA LIGI YAAHIRISHA MECHI MBILI YA SIMBA NA YANGA LIGI KUU SABABU YA PAMBANO LA WATANI SEPTEMBA 30

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    BODI ya Ligi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imeahirisha mechi mbili za Ligi Kuu ya Tanzania Bara zinazozihusu klabu za Simba na Yanga kwa ajili ya kutoa fursa pana ya maandalizi ya pambano baina ya mahasimu hao wa jadi Septemba 30.
    Taarifa ya Mkurugenzi wa Bodi, Boniphace Wambura Mgoyo imesema mechi hizo ni Yanga dhidi ya JKT Ruvu na Simba SC dhidi ya Biashara United zilizopangwa kufanyika Septemba 25 na 26 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Sasa watani hao wa jadi watakuwa na mechi moja moja zaidi wikiendi hii, Simba SC wakimenyana na Mwadui FC Jumamosi mjini Shinyanga na Yanga SC Jumapili dhidi ya Singida United Dar es Salaam kabla ya mpambano baina yao Septemba 30.

    Kwa ujumla, Ligi Kuu itaendelea kesho na mbali na Mwadui na Simba Shinyanga, Biashara United nayo itawakaribisha JKT Tanzania Uwanja wa Karume mjini Musoma mkoani Mara na Ruvu Shooting wakiwakaribisha Coastal Union Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.
    Mbali na Yanga SC na Singida United, mechi nyingine za Jumapili ni kati ya Mbeya City na Kagera Sugar Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya na Alliance FC na Azam FC Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza na Jumatatu African Lyon watakuwa wenyeji wa Mtibwa Sugar Dar es Salaam, Mbao FC na Tanzania Prisons mjini Mwanza na Ndanda FC na Stand United mjini Mtwara.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BODI YA LIGI YAAHIRISHA MECHI MBILI YA SIMBA NA YANGA LIGI KUU SABABU YA PAMBANO LA WATANI SEPTEMBA 30 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top