Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
KOCHA Joseph Marius Omog leo ataiongoza Azam FC katika mchezo wa 27 tangu ajiunge nayo Desemba mwaka jana akitokea Leopard FC ya Kongo Brazaville kurithi mikoba ya Muingereza, Stewart John Hall.
Azam FC, mabingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara jioni ya leo watamenyana na washindi wa pili wa msimu uliopita, Yanga SC katika mchezo wa Ngao ya Jamii Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Na katika mechi hizo 26 za awali, Omog hajawahi kufungwa na timu ya Tanzania, akiwa amepoteza mechi tatu tu dhidi ya timu za nje tupu, maana yake Yanga inawania kuwa timu ya kwanza kuifunga Azam ya Mcameroon huyo.
Azam FC chini ya Omog ilifungwa kwa mara ya kwanza mabao 3-2 na KCC ya Uganda katika Nusu Fainali ya Kombe la Mapinduzi Januari mwaka huu Zanzibar, ambao walikwenda kutwaa Kombe.
Kutoka hapo ikafungwa na Ferroviario 2-0 nchini Msumbiji katika mchezo wa Kombe la Shirikisho ikitoka kushinda 1-0 Dar es Salaam, hivyo kutolewa na Wamakonde hao.
Azam FC ilitoka sare ya bila kufungana ndani ya dakika 90 kabla ya kutolewa kwa penalti na El Merreikh ya Sudan katika Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame mjini Kigali, Rwanda. Merreikh pia ilikwenda kutwaa taji hilo.
Yanga SC inayofundishwa na Mbrazil, Marcio Maximo iliifunga Azam FC 1-0 katika mchezo wa Ngao ya Jamii mwaka jana ikiwa chini ya Stewart.
Yanga SC ndio washindi mara nyingi zaidi wa Ngao, mara ya kwanza wakitwaa mwaka 2001 walipoifunga mabao 2-1 Simba SC, enzi hizo Ligi Kuu inadhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), kupitia bia ya Safari Lager.
Baada ya hapo, haikuchezwa tena mechi ya Ngao hadi mwaka 2009 wakati Mtibwa Sugar ilipoilaza 1-0 Yanga SC.
Mwaka 2010 Yanga walirejesha Ngao kwenye himaya yao, baada ya kuwachapa tena wapinzani wao wa jadi, Simba kwa penalti 3-1 kufuatia sare ya bila kufungana ndani ya dakika 90.
Simba SC walitwaa mara mbili mfululizo Ngao na kufikia rekodi ya watani, kwanza 2011 walipoifunga 2-0 Yanga na 2012 walipotoka nyuma kwa 2-0 na kuilaza Azam 3-2.
Mwaka jana, Yanga SC ikaweka rekodi ya kuwa timu iliyotwaa mara nyingi zaidi Ngao ya Jamii, baada ya kuilaza 1-0 Azam FC, bao pekee la kiungo Salum Abdul Telela ‘Master’.
Lakini leo Yanga SC inakutana na kocha ambaye hafungiki kwa timu za Tanzania, Joseph Marius Omog. Mambo yatakuwaje? Bila shaka hilo ni jambo la kusubiri na kuona.
0 comments:
Post a Comment