• HABARI MPYA

    Thursday, April 02, 2009

    WEMA SEPETU MBARONI TENA

    Wema na Jumbe wake katika pozi ya kimahaba


    NA SALEH ALLY
    INAONEKANA ni kama sikio la kufa halisikii dawa baada ya Miss Tanzania 2006, Wema Abraham Sepetu kuendeleza vituko visivyokuwa na mwisho kufuatia jana kufunguliwa mashtaka mengine na kuswekwa rumande kwenye kituo cha Polisi cha Kijitonyama, jijini Dar es Salaam.
    Wema pamoja na mpenzi wake, Jumbe wamefunguliwa mashitaka ya wizi wa televisheni, redio na microwave (inayotumika kuchemsha vyakula).
    Habari zilizopatikana zinaeleza kuwa Wema na Jumbe wamefunguliwa jalada namba KJN/RB/1977/09 linalohusiana na wizi huo na inaelezwa mrembo huyo alibeba vitu hivyo kutoka kwao na kupotea navyo kwa mpenzi wake huyo ambako alijichimbia kwa siku kadhaa.
    Wema ambaye amekuwa akiibua vituko mfululizo, bado kesi yake ya kuvunja kioo cha gari la aliyekuwa mpenzi wake, mwigizaji maarufu, Steven Kanumba inaendelea katika Mahakama ya Kinondoni.
    Jana asubuhi, mama yake pamoja na dada yake anayeishi Sinza walionekana kwenye kituo cha Kijitonyama kuhusiana na suala hilo na imeelezwa walikuwa wanataka waelezwe vilipo vitu hivyo ili wawatoe nje kwa dhamana.
    Hivi karibuni, hali ya Wema ilionekana kubadilika baada ya mama yake kumtafutia kazi, lakini siku chache zilizopita tabia yake ilibadilika tena na kuanza kurejea usiku nyumbani katika eneo la Sinza jirani na Lion Hotel ambako ni nyumbani kwa dada yake anakoishi baada ya kuibuka kwa tafrani mahakamani siku alipowekewa dhamana mwezi uliopita.
    Jumbe amekuwa akituhumiwa kumfundisha mrembo huyo kutumia dawa za kulevya na alishindwa hata kumwekea dhamana alipolazimika kulala mahabusu lakini alipotoka, mrembo huyo alimkimbilia na kumsahau hata mama yake aliyechukua jukumu la kumuwekea dhamana hiyo.
    Imeelezwa alipotea kwa dada yake eneo la Sinza kwa zaidi ya siku mbili na walikuwa hawajui aliko na baadaye ilielezwa alirejea tena kwa Jumbe ambaye ndugu zake wanamtuhumu kuwa 'amemchezea’ mrembo huyo ambaye anaonekana kutosikia .
    Tangu kuanzishwa kwa mashindano ya Miss Tanzania mwaka 1994, Wema aliyechipukia katika kitongoji cha Dar Indian Ocean, Kanda ya Kinondoni ndiye anaonekana kuwa mrembo mwenye vituko kuliko mwingine yoyote.
    Mrembo wa mwaka 2007, Richa Adhia pia kutoka Kinondoni akionekana kuwa mrembo aliyemaliza muda wake kimya kimya bila kuguswa na tafrani ya aina yoyote.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: WEMA SEPETU MBARONI TENA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top