• HABARI MPYA

    Tuesday, April 14, 2009

    AMBANI ANG'OLEWA JINO BAGAMOYO


    MPACHIKA bao bora Tanzania, Boniphace Ngairah Ambani, juzi alilazimika kung’olewa jino lake moja na daktari, baada ya kuumia mazoezini kwenye kambi ya klabu yake, Yanga ya Dar es Salaam huko Bagamoyo mkoani Pwani.
    Akizungumza na bongostaz kwa simu jana, Ambani amaye ni raia wa Kenya, alisema kwamba kutokana na kuumia jino mazoezini Jumatatu, alijikuta anapata maumivu makali, jambo ambalo lilimlazimu kwenda kung’olewa na sasa anajisikia vizuri.
    “Naendelea vizuri rafiki yangu baada ya kung’olewa jino, na niko fiti kabisa naendelea na maandalizi ya mchezo wetu wa Jumapili dhidi ya watani wetu wa jadi, Simba,”alisema nyota huyo wa timu ya taifa ya Kenya, Harambee Stars.
    Ambani ambaye anaongoza kwa kufunga mabao kwenye Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, akiwa amekwishapachika kimiani mabao 16 hadi sasa, nyuma yake kukiwa na Hussein Bunu wa JKT Ruvu mwenye 11, amekwishasema anataka kumaliza Ligi akiwa ana mabao 20.
    Alipanga kufunga mabao hayo katika mechi tatu, kuanzia Yanga na Polisi Dodoma, ambao alitoka kapa na sasa ana nafasi mbili tu za kutimiza ndoto yake hiyo, nazo ni kwenye mechi dhidi ya Simba Jumapili na Villa Squad Aprili 26, ambao utakuwa mchezo wa mwisho wa Ligi Kuu.
    Mpachika mabao huyo, tayari anachungulia mlango wa kutokea Yanga, kwani amepata timu nyingine ambayo ni Greentown FC ya Zheijang, China.
    Kwa msimu mmoja alioichezea Yanga, Ambani amefunga jumla ya mabao 22, moja kwenye michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, maarufu kama Kombe la Kagame, matano kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika na 16 ya kwenye Ligi Kuu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AMBANI ANG'OLEWA JINO BAGAMOYO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top