VIGOGO, Simba SC wamefufua matumaini ya ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara baada ya ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya wenyeji, Mashujaa FC jioni ya leo Uwanja wa Lake Tanganyika mjini Kigoma.
Kiungo mshambuliaji wa Kimataifa wa Zambia, Clatous Chotta Chama amefunga mabao mawili dakika ya sita na 70, huku bao la tatu likifungwa na mshambuliaji mzawa, Suleiman Abdallah Mwalimu dakika ya 90’+2.
Kwa ushindi huo, Simba SC wanafikisha pointi 52, ingawa wanabaki nafasi ya pili wakizidiwa pointi mbili tu na mabingwa watetezi, Yanga SC baada ya timu zote kucheza mechi 23.
Kwa upande wao Mashujaa FC baada ya kupoteza mchezo huo wanabaki na pointi zao 26 za mechi 23 sasa nafasi ya tisa kwenye ligi ya timu 16.
Ikumbukwe mwisho wa msimu timu mbili zitashuka Daraja na mbili zitakazomaliza nafasi ya 14 na 13 zitamenyana baina yao kwa mechi mbili za nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu.
Timu itakayofungwa itakwenda kumenyana na timu kutoka Ligi ya Championship katika mechi nyingine mbili za mchujo nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla ndiye atacheza Ligi Kuu msimu ujao.



.png)
0 comments:
Post a Comment