• HABARI MPYA

    Friday, September 07, 2018

    YANGA SC KUWAVAA AFRICAN LYON JUMAPILI TAIFA BILA NINJA NA JUMA WOTE, ADUL NA MAHADHI

    Na Lulu Ringo, DAR ES SALAAM
    KLABU ya Yanga itawakosa wachezaji wake watatu, mabeki Juma Abdul, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ na kiungo Juma Mahadhi katika mchezo wa kirafiki dhidi ya African Lyon Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.
    Akizungumza na Waandishi wa Habari leo makao makuu ya klabu, Jangwani mjini Dar es Salaam, Ofisa Habari wa Yanga SC, Dismass Ten amesema kwamba wachezaji hao watakosekana kwa sababu ni majeruhi.
    Ten ametaja viingilio katika mchezo huo utakaoanza Saa 10:00 jioni Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam vitakuwa Sh. 15, 000 kwa VIP A, Sh. 10,000 VIP B na Sh. 5,000 kwa mzunguko.
    Yanga SC imeamua kumenyana na wapinzani wao hao wa Dar es Salaam baada ya kufuta mechi nyingine ya kirafiki dhidi ya Singida United iliyopangwa kufanyika Uwanja wa Lake Tanganyika mjini Kigoma leo.

    Kiungo Juma Mahadhi (kushoto) atakosekana Jumapili Yanga ikimenyana na African Lyon Uwanja wa Taifa 

    Baada ya Kocha Mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kuzuia timu kwenda Kigoma kwa sababu ya umbali, uongozi umefanikiwa kupata mechi ya karibu.
    Yanga SC inataka kuutumia mchezo huu kuiandaa timu yake kwa ajili ya mechi zijazo za Ligi Kuu, dhamira yake kubwa ikiwa ni kutwaa ubingwa wa. 
    Wiki yote hii kikosi cha Yanga kimekuwa kikifanya mazoezi Uwanja wa Chuo cha Maofisa wa Jeshi la Polisi, Kurasini mjini Dar es Salaam.
    Mechi za Yanga za Ligi, pamoja na za Azam FC na Simba zimesimamishwa kupisha maandalizi ya mchezo wa kufuzu Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) kati ya Tanzania na Uganda Septemba 8 mjini Kampala. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC KUWAVAA AFRICAN LYON JUMAPILI TAIFA BILA NINJA NA JUMA WOTE, ADUL NA MAHADHI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top