• HABARI MPYA

    Sunday, May 13, 2018

    YANGA SC YACHEZA MECHI YA SABA MFULULIZO BILA KUSHINDA…MARA YA MWISHO ILISHINDA CHINI YA LWANDAMINA

    Na Mwandishi Wetu, MOROGORO
    YANGA SC leo imecheza mechi ya saba bila ushindi, baada ya kuchapwa 1-0 na Mtibwa Sugar katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.
    Na bao lililoizamisha Yanga SC leo limefungwa na mchezaji wao wenyewe wa zamani, kiungo Hassan Dilunga dakika ya 82.
    Kipigo hicho kinazidi kuwaweka Yanga katika mazingira magumu ya kumaliza Ligi Kuu ndani ya nafasi tatu za juu, kwani sasa wakiwa wamecheza mechi 26 wanazidiwa pointi nne na Azam FC walio nafasi ya pili kwa pointi zao 52 za mechi 28.

    Mara ya mwisho Yanga kushinda ilikuwa ni Aprili 7, mwaka huu walipoichapa 2-0 Welayta Dicha ya Ethiopia katika mchezo wa kwanza wa mchujo wa kuwania kuingia hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika wakiwa chini ya kocha wao, Mzambia George Lwandamina.
    Baada ya mchezo huo, Lwandamina alipakia mizigo yake kurejea kwao na tangu hapo Yanga hawajashinda tena, katika mechi saba, wakifungwa tano na kutoa sare mbili.
    Baada ya mchezo wa leo, Yanga SC inarejea Dar es Salaam kwa ajili ya mchezo wake wa Jumatano wa Kundi D Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Rayon Sport ya Rwanda Uwanja wa Taifa.
    Mechi nyingine ya Ligi Kuu leo, Mbeya City imelazimishwa sare ya 0-0 na Tanzania Prisons katika mechi ya mahasimu wa Jiji la Mbeya Uwanja wa Sokoine.
    Kikosi cha Mtibwa Sugar kilikuwa; Benedictor Tinocco, Rodgers Gabriel, Issa Rashid, Kasiani Ponera, Hassan Isihaka, Shabani Nditi , Ismail Aidan Mhesa, Saleh Khamis Abdallah, Hussein Javu, Hassan Dilunga na Salum Kihimbwa.
    Yanga SC; Youthe Rostand, Juma Abdul, Salumu Hassan, Abdallah Shaibu, Juma Makapu, Pato Ngonyani, Yohana Nkomola, Maka Edward, Matheo Anthony, Thabani Kamusoko na Emanuel Martin.
    Yanga SC haijashinda mechi tangu kocha Msambia, George Lwandamina aondoke mwezi uliopita

    REKODI YA YANGA SC TANGU AONDOKE LWANDAMINA
    Aprili 11, 2018; 
    Yanga 1 – 1 Singida United (Ligi Kuu)
    Aprili 18, 2018; 
    Welayta Dicha 1-0 Yanga SC (Kombe la Shirikisho)
    Aprili 22, 2018; 
    Mbeya City 1-1 Yanga SC (Ligi Kuu)
    Aprili 29, 2018; 
    Simba 1 – 0 Yanga SC (Ligi Kuu)
    Mei 6, 2018; 
    USM Alger 4-0 Yanga SC (Kombe la Shirikisho)
    Mei 10, 2018; 
    Tanzania Prisons 1-0 Yanga SC (Ligi Kuu)

    Mei 13; 2018; 
    Mtibwa Sugar 1-0 Yanga SC (Ligi Kuu)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YACHEZA MECHI YA SABA MFULULIZO BILA KUSHINDA…MARA YA MWISHO ILISHINDA CHINI YA LWANDAMINA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top