• HABARI MPYA

    Friday, May 04, 2018

    MSHAMBULIAJI WA MAJI MAJI AWA MCHEZAJI BORA WA LIGI KUU APRILI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa Majimaji ya Songea mkoani Ruvuma, Marcel Kaheza (pichani kushoto) amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Aprili wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Kaheza alitwaa tuzo hiyo baada ya kuwashinda wenzake wawili, John Bocco na Emmanuel Okwi wote wa Simba ya Dar es Salaam katika uchambuzi uliofanywa wiki hii na kamati ya tuzo hizo.
    Kaheza aliisaidia Majimaj akifunga mabao 7 kwa mwezi huo, ambapo kati ya mabao hayo matatu ‘hat trick’ alifunga katika mchezo mmoja.
    Kwa mwezi huo Majimaji ilicheza michezo minne na kupata pointi saba, baada ya kushinda michezo miwili, kutoka sare mmoja na kufungwa mchezo mmoja, ikipanda kutoka nafasi ya mwisho iliyokuwepo mwezi Machi, hadi ya 14 kati ya timu 16 zinazoshiriki ligi hiyo.
    Kwa upande wa Bocco aliisaidia Simba mwezi huo kupata pointi 16 na kuendelea kuongoza ligi hiyo ikishinda michezo mitano na kutoka sare mmoja, huku Bocco akifunga mabao manne, wakati Okwi naye alichangia kwa kiasi kikubwa mafanikio hayo ya Simba ikiwa ni pamoja na kufunga mabao matatu. Kwa mwezi huo Simba ilicheza michezo sita.
    Kutokana na ushindi huo, Kaheza atazawadiwa tuzo, king’amuzi cha Azam na fedha taslimu sh. Mil. Moja kutoka kwa wadhamini Vodacom.
     Wachezaji wengine ambao tayari wameshinda Tuzo ya Mchezaji Bora wa mwezi wa VPL msimu huu na miezi yao katika mabano ni mshambuliaji wa Simba, Emmanuel Okwi (Agosti), beki wa Singida United, Shafiq Batambuze (Septemba) na mshambuliaji wa Yanga, Obrey Chirwa (Oktoba).
     Wengine ni kiungo wa Singida United, Mudathir Yahya (Novemba), mshambuliaji wa Mbao FC ya Mwanza, Habibu Kiyombo (Desemba), mshambuliaji wa Simba, John Bocco (Januari), kiungo wa Yanga, Papy Tshishimbi (Februari) na mshambuliji wa Lipuli, Adam Salamba (Machi).
    Tuzo za Mchezo Bora wa jumla wa Ligi Kuu Tanzania Bara zinatarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu katika tarehe itakayotangazwa, ambapo licha ya Mchezaji Bora, pia kutakuwa na tuzo nyingine tofauti kwa kategoria mbalimbali.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MSHAMBULIAJI WA MAJI MAJI AWA MCHEZAJI BORA WA LIGI KUU APRILI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top