• HABARI MPYA

    Tuesday, January 01, 2013

    SUNZU AREJESHWA SIMBA SC, MFARANSA AMWAGA WINO LEO MSIMBAZI

    Patrick Liewig

    Na Mahmoud Zubeiry
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Zambia, Felix Mumba Sunzu Jr. ambaye awali ilielezwa atatemwa kwenye kikosi cha Simba SC, amerejeshwa kwenye kikosi hicho.
    Sunzu
    Katibu wa Simba SC, Evodius Mtawala ameiambia BIN ZUBEIRY Sunzu ameomba mwenyewe kurudi kazini na tayari amekwishawasili Dar es Salaam na ameanza mazoezi.
    “Kama utatakumbuka lilikuwa suala la kiafya, Sunzu alikuwa mgonjwa akaomba aachwe, lakini nadhani baada ya kurejea kwao na kutibiwa ameona amepona na ameomba kurudi kazini,”alisema Mtawala.
    Mtawala alisema Sunzu ni miongoni mwa wachezaji waliotarajiwa kuondoka jana mjini Dar es Salaam kwenda visiwani Zanzibar kwenye Kombe la Mapinduzi. Aidha, Mtawala pia alisema mshambuliaji Mrisho Khalfan Ngassa pia ameungana na wenzake mazoezini tangu jana.
    Wakati huo huo, kocha mpya wa Simba, Mfaransa Patrick Liewig aliyewasili jana mchana Dar es Salaam, leo anatarajiwa kusaini mkataba wa kuanza kazi Msimbazi.
    Mtawala alisema, Liewig atakaposaini mkataba atakwenda kuungana na kikosi cha Wekundu hao wa Msimbazi visiwani Zanzibar tayari kuanza kazi.
    Liewig ambaye ni kocha wa zamani wa Akademi ya Paris Saint Germain (PSG) ya Ufaransa, ASEC Mimosas ya Ivory Coast na Club Africain ya Tunisia, jana usiku alitambulishwa mbele ya Wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya Simba katika hoteli ya Spice.
    Liewig mwenye Stashahada ya Juu ya ukocha na Shahada ya tatu ya ualimu wa soka ya vijana aliyotunukiwa na Mkurugenzi wa Ufundi wa Ufaransa, Gerard Houiller, anatarajiwa kwenda Zanzibar kesho.
    Liewig pia amehudhuria kozi za ufundishaji mazoezi ya viungo Juni mwaka 1999 katika Chuo Kikuu cha Dijon.
    Kwa upande wa uzoefu, Liewig alifanya kazi PSG kuanzia mwaka 1989 hadi 1999 kama Kocha Mkuu wa akademi na kuna wakati alikuwa akishirikishwa pia katika programu za timu A, ingawa majukumu yake zaidi yalikuwa ni kwa Under 20, Under 18 aliowawezesha kutwaa Kombe la French Junior Gambardella na Under 16.
    Kuanzia mwaka 1989 hadi 1990:  alikuwa Meneja Mkuu wa Tomislav IVIC, 1990 hadi 1991 alikuwa Msaidizi wa Henri Michel, 1991 hadi 1994 alikuwa Msaidizi wa Artur Jorge, 1994 hadi 1996 alikuwa Msaidizi wa Luis Fernandez, 1996 hadi 1998: alikuwa Msaidizi wa Ricardo Gomez, 1998 hadi 1999 alikuwa Msaidizi wa Alain Giresse.
    Liewig pia alifundisha Al Wahda FC ya Abu Dhabi kuanzia 1999 hadi 2001, ambayo aliipa ubingwa wa Ligi Kuu ya nchi hiyo na Kombe la Ligi.
    Januari mwaka 2003 alikuwa Msimamizi wa Chama cha Soka UAE katika fainali za Afrika za U20 nchini Burkina Faso.
    Kuanzia mwaka 2004 hadi 2009 alikuwa Kocha wa ASEC Mimosas ya Ivory Coast aliyoipa mataji matatu ya Ligi Kuu ya nchini humo mfululizo, 2004, 2005 na 2006, Super Cup ya nchini humo 2005, 2007, 2008 na 2009 na akaiwezesha kufuzu hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa mara tatu, mara moja akiifikisha Nusu Fainali.
    Amekuwa Kocha bora wa Ivory Coast miaka mitatu mfululizo, 2004, 2005 na 2006 na tangu Septemba mwaka jana hadi Juni mwaka huu, alikuwa kocha wa Club Africain ya Tunisia.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: SUNZU AREJESHWA SIMBA SC, MFARANSA AMWAGA WINO LEO MSIMBAZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top