• HABARI MPYA

    Friday, January 25, 2013

    LYON YAONGOZA USAJILI DIRISHA DOGO

    Wachezaji wa African Lyon

    Na Boniface Wambura
    KLABU ya African Lyon ndiyo klabu iliyoongoza kwa kusajili wachezaji wengi kwenye dirisha dogo kwa ajili ya mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom utakaotoa bingwa wa Tanzania Bara, lakini pia timu tatu ambazo msimu ujao zitarudi kucheza Ligi Daraja la Kwanza.
    Kati ya wachezaji 65 waliotua katika klabu mbalimbali katika dirisha hilo, Lyon ndiyo iliyoongoza kwa kuwanasa 12. Miongoni mwao hao, wawili (Ibrahim Job na Shamte Ally) imewachukua kwa mkopo kutoka Yanga.
    Pia watano imewapandisha kutoka katika kikosi chake cha U 20. Wachezaji hao ni Nurdin Musa, Salvatory Jackson, Mohamed Athuman, Athuman Kajembe na jarufu Kizombi. Wengine walioingia katika timu hiyo katika dirisha dogo ni Juma Seif (Huru), Buya Jamwaka (Burkina Faso), Takang Valentine (Huru) na Yusuf Mgwao (Huru).
    Nayo Polisi Morogoro katika kuhakikisha inaondoka mkiani mwa ligi imesajili wachezaji wanane katika dirisha dogo kama ilivyofanya Oljoro JKT ya Arusha.
    Wachezaji wa kigeni walioingia katika dirisha dogo ni Humphrey Mieno, Brian Umony, Jockins Atudo (Azam), Donald Obimma na Ulugbe Chika (Toto Africans), Zuberi Hamis na Tinashe Machemedze (Coastal Union), Musa Mudde na Abel Dhaila (Simba).
    Mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara unaanza kesho (Januari 26 mwaka huu) kwa raundi ya 14 ambapo timu 12 kati ya 14 za ligi hiyo zitakuwa katika viwanja sita tofauti.
    Mabingwa watetezi Simba watakuwa wenyeji wa African Lyon katika mechi itakayochezwa saa 10 jioni kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Hiyo itakuwa mechi ya kwanza kwa kikosi cha Simba tangu kiliporejea kutoka Oman kwenye ziara ya mafunzo.
    Pia Kocha wake mpya, Mfaransa Patrick Liewig anatarajiwa kwa mara ya kwanza kukiongoza kikosi hicho katika mechi ya VPL akisaidiwa na Moses Basena na Jamhuri Kihwelo.
    Mwamuzi wa kimataifa Israel Mujuni ndiye atakayechezesha mechi hiyo ambapo African Lyon inatarajiwa kuongozwa na Kocha Charles Otieno baada ya kusitisha kibarua cha Pablo Velez kutoka Argentina kutokana na kufanya vibaya katika mzunguko wa kwanza.
    Uwanja wa Manungu ulioko Turiani mkoani Morogoro wenye uwezo wa kumeza watazamaji 8,000 ndiyo utakaohimili vishindo vya mechi kati ya Polisi Morogoro na wenyeji Mtibwa Sugar. Polisi Morogoro ambayo ni ya mwisho katika msimamo wa VPL ililazimisha suluhu katika mechi ya mzunguko wa kwanza.
    Coastal Union ambayo kwenye dirisha dogo imesajili wachezaji sita akiwemo Mzimbabwe Tinashe Machemedze itaoneshana kazi na wana-Tanga wenzao Mgambo Shooting kwenye Uwanja wa Mkwakwani, jijini Tanga.
    Timu zinazo katikati ya msimamo wa ligi, Ruvu Shooting na JKT Ruvu zitapimana ubavu kwenye Uwanja wa Mabatini ulioko Mlandizi mkoani Pwani ambapo sheria 17 zinazotawala mpira wa miguu zitakuwa chini ya usimamizi wa refa Dominic Nyamisana kutoka Dodoma.
    Wawakilishi wa Tanzania kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho, Azam baada ya mechi za kirafiki nchini Kenya wanarejea kwenye Ligi Kuu ya Vodacom kwa kuikaribisha Kagera Sugar ya Kocha Abdallah Kibaden kwenye Uwanja wa Chamazi.
    Ni mechi ya kulipa kisasi kwa Kagera Sugar baada ya kulala bao 1-0 katika mechi ya mzunguko wa kwanza iliyochezwa Septemba 15 mwaka jana Uwanja wa Kaitaba, mjini Bukoba.
    Maafande wa Oljoro JKT wanaanza kuchanga upya karata zao katika mzunguko wa pili kwa kuikaribisha Toto Africans ya Mwanza kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Kaluta Amri Abeid, jijini Arusha.
    Yanga iliyopiga kambi ya mazoezi kwa takribani wiki mbili mjini Antalya, Uturuki itaanza mzunguko wa pili dhidi ya Tanzania Prisons katika mechi itakayochezwa keshokutwa (Januari 27 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Vinara hao wa VPL wakiongoza kwa tofauti ya pointi tano dhidi ya Azam wanaowafuatia wanaikabili Tanzania Prisons ambayo imetumia dirisha dogo kuongeza wachezaji wawili akiwemo mshambuliaji mkongwe Emmanuel Gabriel.
    Timu hizo zilitoka suluhu katika mechi ya mzunguko wa kwanza iliyochezwa Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine, jijini Mbeya. Hivyo kiu ya washabiki ni kutaka kujua nani ataibuka mbabe kati ya timu hizo msimu huu.
    Wakati ameingiza wachezaji wawili kwenye dirisha dogo, Kocha wa Tanzania Prisons, Jumanne Chale amempoteza David Mwantika katika dirisa hilo. Beki huyo ametua katika timu ya Azam.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: LYON YAONGOZA USAJILI DIRISHA DOGO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top