![]() |
| Hans Poppe |
Na Mahmoud Zubeiry
MWENYEKITI
wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe amesema kwamba Mwenyekiti
wa Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Soka
Tanzania (TFF), Wakili Alex Mgongolwa anaipotosha Ibara ya 44.3, kwa kuielezea
nusu nusu katika hukumu ya pingamizi la klabu yao dhidi ya Yanga, kuhusu
mchezaji Kevin Yondan.
Akizungumza na
BIN
ZUBEIRY leo, Hans Poppe ambaye ni Kapteni wa zamani wa jeshi la Wananchi
Tanzania (JWTZ), alisema kwamba Mgongolwa anapotosha na kwa ujumla Kamati yake
imekosea kumuidhinisha beki wao Yondan kuchezea Yanga, kwa kuwa klabu hiyo
haikufuata taratibu za kumsajili kulingana na maelekezo ya Ibara hiyo.
Ibara ya 44.3
kuhusu masharti maalum yanayohusu mikataba kati ya wachezaji wa kulipwa na
klabu inasema; Klabu inayotarajia kuingia
mkataba na mchezaji wa kulipwa, haina budi kuiarifu klabu yake ya sasa kwa
maandishi, kabla ya kufanya makubaliano na mchezaji huyo wa kulipwa. Mchezaji wa
kulipwa atakuwa huru tu kuingia mkataba na klabu nyingine, iwapo mkataba wake
na klabu yake ya sasa utakuwa umekwisha, au unakwisha ndani ya miezi sita,
uvunjwaji wowote wa sheria hii, utastahili vikwazo vinavyofaa.
Lakini Hans
Poppe amesema kwamba anashangaa sana kuona taarifa ya Mgongolwa inasema kwa
mujibu wa Ibara ya 44 (3) ya Kanuni za Uhamisho wa Wachezaji za TFF, Yanga
ilifuata taratibu zote katika kumsajili Kevin Yondan, hivyo ni mchezaji wake
halali.
“Si kweli,
huyu bwana anapotosha, na mbona hakuinukuu yote Ibara hiyo katika taarifa yake?
Sasa hii ndio maana sisi tumesema, tunakutana kupanga tarehe ya Mkutano Mkuu,
kuomba Baraka za wanachama tujitoe tu kwenye ligi, kwa sababu hatutendewi haki,
haki si sahihi,”alisema Hans Poppe.
Aidha,
Mwenyekiti huyo mpya wa Friends Of Simba (F.O.S.) alisema kwamba Ibara ya 45. 6
pia inakazia Ibara hiyo ya 44.3 na kwamba bado anashangaa kwa nini Mgongolwa,
ambaye kitaaluma ni Mwanasheria anapindisha sheria za usajili.
Ibara ya 45.
6 kuhusu Usajili na Uhamisho wa Wachezaji, inasema; Mchezaji ambaye ameingia mkataba wa zaidi ya
msimu mmoja hatoruhusiwa kujisajili na klabu nyingine, kabla ya klabu ya yake mpya kuafikiana na klabu yake ya zamani (kanuni
ya 44.3)
Alisema Yanga walimsainisha Yondan mkataba Mei 12, mwaka huu wakati mkataba wake wa awali na Simba ulikuwa unaisha Mei 30, inamaanisha walianza kuzungumza muda mrefu bila kuiarifu klabu yake ya sasa na wakati huo huo, mchezaji huyo aliongeza mkataba Novemba mwaka jana na Simba.
"Na kama Yanga wangefuata utaratibu huu wa kuzungumza na klabu yake, wangepewa taarifa kama amekwishasaini mkataba mpya,"aliongeza.
Mapema wiki hii, Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya TFF pamoja na kumuidhinisha Yondan kuchezea Yanga, iliitaka Simba kuthibitisha madai yake ya kuingia mkataba na beki huyo na kuwasilisha upya malalamiko yake kwenye kamati hiyo.
"Na kama Yanga wangefuata utaratibu huu wa kuzungumza na klabu yake, wangepewa taarifa kama amekwishasaini mkataba mpya,"aliongeza.
Mapema wiki hii, Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya TFF pamoja na kumuidhinisha Yondan kuchezea Yanga, iliitaka Simba kuthibitisha madai yake ya kuingia mkataba na beki huyo na kuwasilisha upya malalamiko yake kwenye kamati hiyo.
“Kwa mujibu
wa Ibara ya 44 (3) ya Kanuni za Uhamisho wa Wachezaji za TFF, Yanga ilifuata taratibu
zote katika kumsajili Kevin Yondan, hivyo ni mchezaji wake halali.
Kwa vile
Simba imesema mchezaji huyo vilevile alisaini mkataba na klabu yao, imetakiwa
kupitia mamlaka nyingine kuthibitisha hilo, na baada ya uthibitisho iwasilishe
malalamiko yake kwenye Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji, au
mamlaka zozote za kisheria kwa mujibu wa madai/lalamiko husika,”alisema
Mgongolwa katika taarifa yake aliyoituma BIN ZUBEIRY.
Mbali na
Mwenyekiti Mgongolwa, Wajumbe wengine wa Kamati hiyo waliohudhuria kikao hicho
ni Hussein Mwamba, Imani Madega, Ismail Aden Rage, Llyod Nchunga na Omari Gumbo,
ambao mwishowe walipiga kura kuamua beki huyo achezee timu gani msimu ujao na
ndipo Yanga ikashinda.
Hata hivyo,
inadaiwa katika upigaji kura, tatu zilimbakisha Yondan Simba na tatu zilimpeleka
Yanga, lakini kwa kuwa Mwenyekiti ana nafasi ya kupiga kura ya ziada, iwapo
kura zimegongana- na siku hiyo Mgongolwa aliitumia kura yake kumpeleka beki
huyo Jangwani.



.png)
0 comments:
Post a Comment