Said Bahanuzi, mfungaji bora Kombe la Kagame akiwapungia mikono mashabiki jana Uwanja wa Jamhuri baada ya timu kufika uwanjani- mechi mbili hajafunga bao Ligi Kuu |
Na Mahmoud Zubeiry
KOCHA wa Yanga,
Mbelgiji Tom Saintfiet amesema kwamba wachezaji wake wamelewa sifa baada ya
mwanzo mzuri wa msimu na kila mmoja sasa anajiona ‘staa’ kiasi cha kutocheza
kwa kujituma, hali ambayo imechangia timu yake kuanza vibaya katika Ligi Kuu ya
Vodacom Tanzania Bara.
Akizungumza na
BIN
ZUBEIRY leo, Mtakatifu Tom alisema kwamba wachezaji wanatakiwa
kubadilika haraka, vinginevyo mabadiliko yatahitajika katika timu.
Kocha wa Yanga, Mtakatifu Tom kushoto akiwa na Meneja, Hafish Suleiman |
“Nimesononeshwa
mno tena, na ninaomba radhi kwa mashabiki, wanastahili ushindi, tuna mashabiki
wazuri, katika mechi ya jana tulipata nafasi nane nzuri asilimia 100, mita tano
kutoka langoni kwa wapinzani, tulipoteza hadi penalti. Si kawaida,”.
“Mtibwa Sugar
si timu mbaya, walipata nafasi nne na wakafunga mabao matatu, mashuti mawili ya
kiwango cha dunia. Kama tusingetengeneza nafasi, ingekuwa rahisi kwangu kama
kocha kulaumiwa, lakini sasa sisi makocha hatuwezi kupiga mpira kupeleka
nyavuni, na wachezaji ndio wanatakiwa kufanya hivyo,”.
“Hii inauma,
kufanya vizuri Kombe la Kagame na kuanza vibaya katika ligi, wachezaji fulani si
wachezaji tena, wanajiona mastaa, hivyo wanatakiwa kuzinduka haraka, vinginevyo
mabadiliko yanahitajika,”alisema Mtakatifu Tom.
Mechi ya
jana inakuwa ya pili kwa Yanga kufungwa chini ya Saintfiet tangu aanze kazi
Julai mwaka huu, akirithi mikoba ya Mserbia, Kostadin Bozidar Papic aliyetupiwa
virago, katika mechi 14 alizoiongoza timu hiyo hadi sasa, ambazo ndani yake
zipo sita za Kombe la Kagame, aliloiwezesha timu hiyo kutwaa.
Yanga iliyoanza
ligi kwa sare ya bila kufungana na Prisons mjini Mbeya, jana ilifungwa 3-0 na Mtibwa
Sugar katika mchezo wake wa pili, kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.
Jana, Yanga
ilizidiwa mno na hadi mapumziko, tayari Mtibwa Sugar walikuwa mbele kwa mabao
2-0, yaliyotiwa kimiani na beki wa kati, Dickson Daudi dakika ya 11
akiunganisha kwa kichwa kona ya beki wa kushoto Malika Ndeule.
Bao hilo
lilitokana na uzembe wa mabeki wa Yanga ambao walishindwa kumuweka ulinzi
mchezaji mrefu kuliko wote, Daudi.
Yanga
walijaribu kutaka kusawazisha, lakini mipango yao haikuwa na tija na kujikuta
wakiendelea kushambuliwa na dakika ya 43, Hussein Javu aliwainua tena vitini
mashabiki wa Simba waliokuwa wakiwashangilia kwa nguvu leo kwa kufunga bao la
pili.
Kwa ujumla
kipindi cha kwanza, Yanga walicheza ovyo- pasi zao nyingi zilikuwa hazifiki,
walishindwa kuwabana wapinzani wao na zaidi Haruna Niyonzima alishindwa
kuiongoza vema timu, jambo ambalo lilifamnya kiungo mkabaji Athumani Iddi
‘Chuji’ kupanda mbele zaidi kusaidia, ingawa haikusaidia.
Mabeki
wawili wa kati wa Mtibwa, Daudi na Salvatory Ntebe waliwadhibiti vema
washambuliaji wawili wa Yanga, Hamisi Kiiza na Saidi Bahamnuzi katika dakika 45
za kipindi cha kwanza.
Kipindi cha
pili, Kocha wa Yanga, Mbelgiji Tom Saintfiet alianza kwa mabadiliko akiwatoa Frank
Damayo na David Luhende na kuwaingiza Simon Msuva na Stefano na Mwasyika,
lakini bado ukuta wa Mtibwa ulikuwa mgumu mbele ya Watoto wa Jangwani.
Katika
kuongeza mashambulizi, Mtakatifu Tom alimtoa beki Mbuyu Twite na kumuingiza na
mshambuliaji Didier Kavumbangu, lakini bado mambo yaliendelea kuwa magumu kwa
Yanga.
Dakika ya 86
Hussein Javu aliifungia Mtibwa bao la tatu kwa shuti la mbali, wakitoka
kushambuliwa na kufikia hapo, Yanga ‘walikufa’ na mashabiki wao wakaanza
kuuacha Uwanja wa Jamhuri.
Huu unakuwa
mchezo wa pili kwa Yanga tangu kuanza kwa ligi wakiwasononesha mashabiki wao,
baada ya mechi ya kwanza kulazimishwa sare ya bila kufungana na Prisons kwenye
Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.
Waswahili
wanasema siku ya kufa nyani, miti yote huteleza, Hamisi Kiiza alipaisha mkwaju
wa penalti dakika ya 89, baada ya Daudi kuunawa mpira kwenye eneo la hatari.
Yanga SC; Ally Mustafa ‘Barthez’, Juma Abdul,
, Mbuyu Twite/Kavumbangu, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Athumani Iddi
‘Chuji’, Frank Domayo/Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Said Bahanuzi, Hamisi
Kiiza na David Luhende/Stefano Mwasyika.
Mtibwa Sugar; Shaaban Hassan Kado, Malika Ndeule, Issa
R Issa, Dickson Daudi, Salvatory Ntebe, Shaaban Nditi, Jamal Mnyate/Babu Ally
Seif, Awadh Juma, Hussein Javu, Shaaban Kisiga ‘Malone’ na Vincent Barnabas/Ally
Mohamed ‘Gaucho’.
Katika mechi
nyingine, Simba SC iliendeleza wimbi la ushindi, baada ya kuichapa JKT Ruvu
mabao 2-0 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, licha ya kucheza pungufu baada ya
Emanuel Okwi kutolewa nje kwa kadi nyekundu.
Mabao ya Simba yalitiwa kimiani na
viungo Amri Kiemba na Haruna Moshi ‘Boban’ na kwa matokeo hayo, Simba
inaendelea kuongoza ligi kwa kufikisha pointi sita, baada ya awali kuifunga
African Lyon 3-0.
Simba SC; Juma Kaseja, Nassor Masoud ‘Chollo’,
Amir Maftah, Shomary Kapombe, Juma Nyosso, Mwinyi Kazimoto, Amri Kiemba, Haruna
Moshi ‘Boban’, Daniel Akuffo, Mrisho Ngassa na Emanuel Okwi.
Katika mechi nyingine za ligi hiyo,
Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza Azam imelazimishwa sare ya 2-2 na wenyeji
Toto African, Uwanja wa Kaitaba Bukoba, wenyeji Kagera Sugar wametoka sare
ya bila kufunga na JKT Oljoro ya Arusha, wakati Uwanja wa Sokoine Mbeya,
wenyeji Prisons wametoka sare ya 1-1 na Coastal Union ya Tanga na kwenye Uwanja
wa Chamazi, African Lyon imeifunga Polisi Morogoro 1-0, wakati Uwanja wa
Mabatini, Mlandizi, Ruvu Shooting imeifunga 2-1 Mgambo JKT.
Babu Ally, shabiki wa Yanga ambaye jana 'alitia huruma' Uwanja wa Jamhuri baada ya 3-0 |
REKODI YA SAINTFIET YANGA
1.
Yanga
Vs JKT Ruvu (Kirafiki) 2-0
2.
Yanga
Vs Atletico (Burundi, Kagame) 0-2
3.
Yanga
Vs Waw Salam (Sudan, Kagame) 7-1
4.
Yanga
Vs APR (Rwanda, Kagame) 2-0
5.
Yanga
Vs Mafunzo (Z’bar, Kagame) 1-1 (5-3penalti)
6.
Yanga
Vs APR (Rwanda, Kagame) 1-0
7.
Yanga
Vs Azam (Kagame) 2-0
8.
Yanga
Vs African Lyon (Kirafiki) 4-0
9.
Yanga
Vs Rayon (Kirafiki, Rwanda) 2-0
10.
Yanga
Vs Polisi (Kirafiiki, Rwanda) 2-1
11.
Yanga
Vs Coastal Union (Kirafiki) 2-1
12.
Yanga
Vs Moro United (Kirafiki) 4-0
13.
Yanga
Vs Prisons (Ligi Kuu) 0-0
14.
Yanga
Vs Mtibwa (Ligi Kuu) 0-3
0 comments:
Post a Comment