• HABARI MPYA

    Wednesday, September 19, 2012

    SIMBA YACHEZA LIGI KWELI LEO, YANGA WANA KAZI KWA MTIBWA, AZAM KUMALIZANA NA TOTO

    Akuffo ataendelea kuwainua vitini mashabiki wa Simba leo?

    Na Mahmoud Zubeiry
    LIGI Kuu ya soka ya Vodacom Tanzania Bara inatarajiwa kuendelea leo, timu zote 14 zikijitupa uwanjani kwa mara ya pili, macho na masikio ya wengi yakielekezwa katika viwanja vya CCM Kirumba mjini Mwanza, Jamhuri mjini Morogoro na Taifa mjini Dar es Salaam.
    Wakati mabingwa watetezi, Simba SC wakiwa wageni wa JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Mtibwa Sugar watakuwa wenyeji wa Yanga kwenye Uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro na Mwanza, Toto wataikaribisha Azam FC.
    Viingilio kwa mechi ya Uwanja wa Taifa vitakuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 wakati kwenye Uwanja wa Jamhuri itakuwa sh. 3,000 kwa sh. 10,000.
    Mechi nyingine za ligi hiyo zitakazochezwa leo ni African Lyon vs Polisi Morogoro kwenye Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam. Nayo Ruvu Shooting itashuka kwenye Uwanja wake wa Mabatini, Mlandizi kuikabili Mgambo Shooting kutoka Handeni mkoani Tanga.
    Tanzania Prisons itakuwa kwenye Uwanja wake wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya kuisubiri Coastal Union ya Tanga wakati Oljoro JKT itaitembelea Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.
    Kocha Mkuu wa Yanga SC, Mbelgiji Tom Saintefiet amebeba wachezaji 18 kwa mchezo wa leo na Mtibwa Sugar, kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro ambao ni makipa; Yaw Berko, Ally Mustafa ‘Barthez’, mabeki Shadrack Nsajigwa, Juma Abdul, Godfrey Taita, Mbuyu Twite, Kevin Yondan,  Nadir Haroub ‘Cannavaro’, David Luhende, Oscar Joshua na Stefano Mwasyika.
    Aliwataja viungo ni Athumani Iddi ‘Chuji’, Haruna Niyonzima, Frank Domayo, Nizar khalfan, Shamte Ally na Simon Msuva, wakati washambuliaji ni Didier Kavumbangu, Said Bahanuzi na Hamisi Kiiza, wakati waliobaki Dar es Salaam ni kipa Said Mohamed, mabeki Ladislaus Mbogo, Job Ibrahim, viungo Rashid Gumbo, Juma Seif ‘Kijiko’, Salum Telela, Omega Seme, Nurdin Bakari, Idrisa Assega, Issa Ngao wa Yanga B anayekomazwa kikosi cha kwanza na mshambuliaji Jerry Tegete.
    Huo utakuwa mchezo wa pili kwa Yanga katika ligi hiyo, baada ya awali kulazimishwa sare ya bila kufungana na Prisons kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya Jumamosi.
    Saintfiet juzi aliwaomba radhi mashabiki wa Yanga kwa sare ya Jumamosi kwenye Uwanja wa Sokoine na akawatupia lawama viongozi wa klabu hiyo, kwa maandalizi mabovu.
    Saintfiet alilalamikia kulala kwenye hoteli mbaya, yenye vitanda vichache na vidogo, vilivyosababisha watu wakalala mzungu wa nne, na chakula kibaya na kwa ujumla alisema hawakuwa vizuri kabla ya mechi hiyo.  Alisema yeye alilala kitanda kimoja na Louis Sendeu na Mbuyu Twite alibanana na Didier Kavumbangu na hoteli haikuwa na mabomba vyooni wala bafuni, hivyo kulazimika kuingia na ndoo na kuogea kata.
    Alisema pia hoteli hiyo ilikuwa katikati ya mji na karibu na stendi ya mabasi, kila alfajiri kelele nyingi na kwa ujumla timu iliingia uwanjani ikiwa haiku vizuri.
    “Mimi kwa mfano sijaoga siku mbili, kwa kweli tulikuwa katika mazingira magumu na wapinzani wetu walicheza soka ya kuudhi tangu mwanzo, kupoteza muda, na marefa hawakuchukua hatua, tulipoteza nafasi kupitia kwa Kiiza (Hamisi) na Msuva (Simon), siwezi kulaumu mchezaji wangu yeyote, lakini hiyo ndiyo hali halisi,”alisema Saintfiet.
    Alisema anajua hata Uwanja wa huko, Jamhuri si mzuri na mechi itakuwa ngumu kwa sababu Mtibwa Sugar nao walitoka sare ya bila kufungana na Polisi katika mchezo wao wa kwanza Jumamosi na anaiheshimu timu hiyo kama moja ya timu tano kubwa Tanzania, pamoja na Simba, Azam na Coastal Union.
    “Lakini pamoja na kwamba Simba wamependelewa kupangiwa ratiba ya kuanza kucheza nyumbani mechi tano mfululiuzo, nakuambia Mei mwaka 2013 Yanga ndio itavishwa taji la ubingwa wa Ligi Kuu, acha wafurahie sasa hivi, watalia mwisho,”alisema Mtakatifu Tom.
    Simba SC juzi na jana ilifanya mazoezi kwenye Uwanja wa Kinesi, Manzese eneo la Urafiki, Dar es Salaam na Felix Sunzu alikuwa kivutio kwenye mazoezi hayo na haitakuwa ajabu leo kocha Milovan Cirkovick akimchezesha japo kwa kutokea benchi.
    Sunzu alijituma sana mazoezini juzi na jana- ingawa Daniel Akuffo na Abdallah Juma nao walifanya kazi nzuri ya kumvutia kocha Milo.
    Awali, Milo, alikaririwa na BIN ZUBEIRY akisema kwamba anamuhitaji Sunzu, ambaye ni mchezaji ghali katika timu yake, lakini anaweza kucheza bila yeye.
    Milo alisema kwamba Sunzu hakumtumia kwenye mechi ya kwanza ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya African Lyon kwa sababu alichelewa kurudi Dar es Salaam kutoka kwao Zambia. “Ilikuwa kila siku anasema atakuja kesho, kesho, haji,”alisema.
    Sunzu aliyetua Dar es Salaam siku moja kabla ya mechi na Lyon, katika kipindi cha takriban wiki tatu hakuwa na timu, kwanza akienda kwenye msiba wa dada yake Lubumbashi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na aliporejea akaomba ruhusu ya kwenda kwao Zambia.
    Alipoulizwa kama mchezaji huyo anayelipwa mshahara mkubwa zaidi kuliko wachezaji wote wa klabu hiyo, dola 3,500 kwa mwezi, zaidi ya Sh. Milioni 5 za Tanzania, ni muhimu kwa sasa kwenye kikosi chake, Mserbia huyo alisema; “Ndiyo, ni muhimu, namuhitaji, lakini naweza kucheza bila yeye,”alisema.
    Inaonekana sasa Milo anatiwa jeuri na washambuliaji wake wapya, Mghana Daniel Akuffo, Abdallah Juma, Salim Kinje, Mrisho Ngassa na wengine ambao yupo nao tangu msimu uliopita akina Emmanuel Okwi, pamoja na viungo wenye uwezo wa kufunga kama Mwinyi Kazimoto, Haruna Moshi na wengineo.
    Awali ya hapo, Milo alisema kwa sasa hawatumii mabeki wake wapya, Komabil Keita kutoka Mali na Paschal Ochieng kutoka Kenya, kwa sababu anataka kwanza waone timu hiyo inavyocheza wakiwa nje, ili wajifunze.
    Profesa huyo wa Kiserbia alisema kwamba mabeki hao wawili wa kati wanahitaji muda kabla ya kuanza kucheza kwa mfumo wa Simba, ingawa amewasifia wote ni wazuri.
    Alisema wakati wowote wanaweza kurudi uwanjani, iwe kwa pamoja au kupangwa na wachezaji wengine na inawezekana hata kwenye mechi  ya leo, Jumatano dhidi ya JKT Ruvu, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Azam FC jana walifanya mazoezi kwenye Uwanja wa Kirumba mjini Mwanza, ili kuuzoea kabla ya mechi yao na Toto African leo.
    Juzi Azam walifanya mazoezi kwenye Uwanja wa Chuo cha Ualimu (TTC), Butimba mjini humo kujiandaa na mechi hiyo ambayo tayari imekuwa gumzo mjini Mwanza, wakazi wa Jiji hilo wakiwa na hamu ya kuwaona mastaa wa Azam wanachezaje.
    Azam iliyoanza vema ligi hiyo kwa ushindi wa 1-0 kwenye Uwanja wa Kaitaba, Bukoba, bao pekee la Abdulhalim Humud dhidi ya wenyeji Kagera Sugar, imepania kuondoka na pointi zote sita katika mechi zake zote mbili za Kanda ya Ziwa.
    Toto Africans itahitaji ushindi kwenye mchezo huo, ili kurejesha imani kwa mashabiki wake baada ya kulazimishwa sare ya 1-1 na JKT Oljoro, katika mchezo wa ufunguzi Jumamosi.
    Mserbia anayeinoa Azam, Boris Bunjak ameomba marefa wachezeshe kwa haki, kwani anaamini vijana wake wanaweza kushinda pale tu sheria 17 zinapotekelezwa uwanjani na si vinginevyo.
    Kocha huyo aliwalalamikiwa marefa waliochezesha mechi yao ya Ngao ya Jamii na Simba kwamba waliwabeba mno wapinzani wake, hata wakatoka nyuma kwa 2-0 na kushinda 3-2.
    Kwa upande wake, Kocha wa Toto, John Tegete amesema kwamba baada ya kulazimishwa sare na Oljoro, Jumatano watapigana kufa na kupona ili kushinda mechi ya kwanza ya Ligi Kuu.
    “Sare ya juzi kwa kweli hatukuitarajia, tulicheza vizuri, tulipata nafasi nyingi tukapoteza, lakini kwa siku mbili hizi tutafanyia kazi makosa yetu na Jumatano tunaomba mashabiki waje kwa wingi kushuhudia mabadiliko, tunawaahidi ushindi,”alisema baba huyo wa mshambuliaji wa Yanga, Jerry Tegete.

    MSIMAMO WA LIGI KUU BARA
                                 P    W  D   L    GF       GA      GD      P
    Simba SC             1    1    -     -     3          -           3          3
    Azam FC              1    1    -     -     1          -           1          3
    Coastal                 1    1    -     -     1          -           1          3
    JKT Ruvu             1    1    -     -     2          1          1          3
    Toto African          1    -     1    1    1          -           -           1
    JKT Oljoro            1    -     1    1    1          -           -           1
    Yanga SC             1    -     1    -     -           -           -           1
    Prisons                 1    -     1    -     -           -           -           1
    Polisi Moro            1    -     1    -     -           -           -           1
    Mtibwa Sugar       1    -     1    -     -           -           -           1
    African Lyon         1    -     -     1    -           3          -3        0
    Kagera Sugar       1    -     -     1    -           -           -           0
    JKT Mgambo        1    -     -     1    -           1          -1        0
    Ruvu Shooting     1    -     -     1    1          2          -1        0
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA YACHEZA LIGI KWELI LEO, YANGA WANA KAZI KWA MTIBWA, AZAM KUMALIZANA NA TOTO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top