![]() |
| Binti mikononi mwa Polisi |
KATIKA
Fainali ya Kombe la Mapinduzi jana kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar alikatiza binti
mmoja wa umri kati ya miaka 14 na 16 uwanjani dakika ya 89, wakati timu hizo
zikiwa zimefungana bao 1-1 akiingilia jukwaa la Urusi na kutokea upande wa
jukwaa kuu, ambako alipokewa na Polisi na kutolewa nje ya Uwanja.
Refa
Ramadhan Rajab Ibada ‘Kibo’ alijaribu kumsimamisha kumsemesha, lakini hakuzungumza
chochote na aliendelea kukatiza Uwanja hadi nje ambako alipokewa na askari
Polisi na kutolewa nje kabisa ya Uwanja. Mtangazaji wa Uwanja wa Amaan, Farouk
Karim aliwatuliza mashabiki akisema binti huyo ametoroka hospitali ya vichaa,
Kidongo Chekundu na tayari Polisi wamemkamata na kumrejesha huko.
Hadi dakika
90 zinamalizika timu hizo zilikuwa zimefungana bao 1-1 na ndipo zikaongezwa
dakika 30, ambako Gaudence Exavery Mwaikimba aliipatia Azam bao la ushindi
dakika ya pili tu tangu kuanza kwa muda wa nyongeza.
Baada ya
tukio hilo, na kudaiwa binti huyo alikuwa chizi na alitoroka hospitali kuna
maswali matano ya kujiuliza kulingana na jinsi alivyotambulishwa.
![]() |
| Tazama jinsi alivyoshikwa mikono kwa nguvu naye ameshika vitu vyake kwa nguvu kulia |
1.
Farouk
Karim alisema binti ni chizi alitoroka hospitali ya vichaa, alijuaje na sisi
tuliokuwa tunapiga picha uwanjani tulimfuatilia binti huyo hadi anatolewa nje
ya Uwanja hakuzungumza chochote mbele ya askari ambao walijaribu kumuhoji na
wakati huo huo ndipo MC huyo akatoa tangazo hilo?
2.
Binti
alitambulishwa chizi aliyetoroka hospitali, aliingiaje uwanjani na aliruhusiwa
vipi na kali zaidi alitokea sehemu ambayo timu hutokea kuingia uwanjani (Dressing
rooms)- huko kuna ulinzi mkali na walinzi huhakikisha yeyote asiyehusika hata
Mwandishi wa Habari haingii huko?
3.
Alikuwa
mwenye kujiamini kupita kiasi na alitaka kupita njia alizotaka yeye, kwa mfano
Polisi walitaka kumpandisha jukwaani, ila yeye akaendelea kuongoza mbele hadi
kwenye geti ambalo walimtolea, kwa nini Polisi walimtii namna ile?
4.
Kuna
vitu alikuwa amevishika mkononi wakati anatakiza Uwanja na aliendelea kuvishika
kwa umakini hadi alipotiwa nguvuni na Polisi na kwa nini askari hawakutaka
kujua ameshika nini, labda alikuwa amebeba kitu cha hatari mfano wa bomu. Haikutokea
hatari hiyo, lakini kwa nini ilichukuliwa kwa urahisi tu?
5.
Kwa
nini alitokea uwanjani wakati ambao refa na wachezaji wa timu zote wapo kwenye
lango la timu moja, (la Tusker) wakisubiri kupigwa mpira wa kona- na alipita
upande wa katikati ya mstari wa kuugawa Uwanja, jambo ambalo lilimsaidia kukatiza
bila kukumbana na kashikashi za mchezo hadi refa aliposhituka kutokana na
kelele za mashabiki ndipo akamfuata?
![]() |
| Refa akimzuia binti |
![]() |
| Binti anakatiza tu, refa kama anambembeleza hivi |
![]() |
| Binti kwa kujiamini kabisa anakatiza Uwanja |
HITIMISHO;
Lengo la makala
hii, ni kupingana na desturi ya kuchukulia mambo kirahisi kutokana na hisia au
dhana, kwani wakati mwingine inaweza kutokea hatari kubwa. Tumeshuhudia nchi
hii watu wakijifanya machizi kakini katika hadhara, lakini mwisho wa siku
wanafanya mambo ya hatari, mfano kupigwa kiatu kwa rais Mstaafu Alhaj Ally
Hassan Mwinyi au namna Ubalozi wa Marekani ulivyolipuliwa nchini mwaka 1998,
lazima kuna aina fulani ya uzembe au kuchukulia mambo kirahisi ulifanyika.
Wale watu wa
Uamsho tunajua jitihada zao ziliishia wapi, au ilichukuliwa kama tukio la
kishirikina tu kama lile la paka kukatiza uwanjani hapo mwaka 1992 wakati wa
mechi ya Simba na Yanga tu, watu wakaamua kutuliza mashabiki kwa kusema ni
chizi? Nawasilisha.







.png)