Mussa Mudde akipasua ukuta wa Express |
Charles Ayikoh |
Na Prince Akbar
KOCHA wa klabu bingwa Uganda, Express ‘Red Eagles’, Charles
Ayikoh amesema kwamba Yanga ni timu bora na hatari zaidi ya Simba, baada ya
kucheza na timu hizo jana na leo, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Akizungumza na BIN ZUBEIRY baada ya mechi ya leo
dhidi ya mabingwa wa Tanzania, Simba SC, Uwanja wa Taifa, Ayikoh alisema kwamba
kama itatokea mechi ya kuwania Kombe, akiambiwa achague timu ya kucheza nayo,
atachagua Simba.
“Nitachagua Simba kwa sababu najua nitashinda, ila Yanga ni
hatari sana, siwezi kuomba kukutana nao,”alisema.
Akifafanua, Ayikoh alisema Yanga inacheza kwa kushambulia mfululizo
na muda wote wanakuja tu kwenye lango lako, wakati Simba wanapiga pasi zaidi na
hawana makali katika kushambulia.
“Leo mabeki wangu walikuwa likizo, hawakuwa na kazi, jana
ilikuwa hatari sana kwao, Yanga wanashambulia sana,”alisema leo Ayikoh, baada
ya sare ya bila kufungana na Simba SC.
Express ambayo ilifungwa 2-1 na Yanga jana, awali ilicheza
na Simba mjini Shinyanga wakatoka sare ya kufungana bao 1-1.
Hata hivyo, katika mchezo wa leo, Simba ilicheza bila
washambuliaji wake watatu hatari, Mganda Emmanuel Okwi, Mzambia Felix Sunzu na
mzalendo Haruna Moshi ‘Boban’.
Jana Yanga ilichanganya wachezaji wake wote hatari, wapya na
wa zamani- labda alikosekana Haruna Niyonzima pekee. Jerry Tegete alicheza
pamoja na mshambuliaji mpya Simon Msuva kutoka Moro United, wakati viungo walikuwa
Frank Damayo, Said Bahanuzi, Nizar Khalfan na Athumani Iddi ‘Chuji’.
Simba leo pale mbele alianza Abdallah Juma aliyesajiliwa
kutoka Ruvu Shooting, aliyecheza nyuma ya viungo hodari kama Patrick Mbivayanga,
Mussa Mudde, Uhuru Suleiman, Christopher Edward na Amri Kiemba.
Simba na Yanga wapo kwenye maandalizi ya Klabu Bingwa Afrika
Mashariki na Kati, maarufu kama Kombe la Kagame, inayotarajiwa kuanza Julai 14,
mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Yanga waliopo Kundi C, watafungua dimba na Athletico ya
Burundi Julai 14, wakati Simba waliopo Kundi A wataanza na URA ya Uganda Julai
16.
Timu nyingine inayoshiriki michuano hiyo ni Azam FC
iliyopangwa Kundi B, ambayo itafungua dimba na Mafunzo ya Zanzibar Julai 15,
Uwanja wa Chamazi.
0 comments:
Post a Comment