• HABARI MPYA

    Tuesday, July 31, 2012

    MKUU MKUU SIMBA SC, WANACHAMA WAKUMBUSHWA KULIPIA KADI


    Na Princess Asia
    MAANDALIZI ya Mkutano Mkuu wa mwaka wa Simba SC yanaendelea vizuri na utafanyika kama ulivyopangwa Agosti 5, mwaka huu kwenye ukumbi wa Polisi Oysterbay, Dar es Salaam.
    Katibu Mkuu wa Simba SC, Evodius Mtawala ameiambia BIN ZUBEIRY kwamba uongozi unarudia kuwakumbusha wanachama wote, ambao hawajalipia ada zao za uanachama kufanya hivyo mapema ili washiriki Mkutano huo.
    “Tunarudia kuwakumbusha wanachama wetu, ambao hawajalipia ada zao za uanachama kufanya hivyo mara moja, ili wapate haki ya kushiriki Mkutano Mkuu,”alisema Mtawala.
    Wiki iliyopoita, Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), leo ilikabidhi hundi ya Sh. Milioni 20 kwa klabu ya Simba SC ya Dar es Salaam, kwa ajili ya Mkutano huo.
    Akikabidhi mfano wa hundi hiyo kwa Makamu Mwenyekiti wa Simba SC, Geofffrey Nyange ‘Kaburu’, Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, inayozalishwa na TBL, George Kavishe alisema kwamba anawatakia mafanikio Simba SC katika mkutano wao huo Mkuu.
    Kwa upande wake, Kaburu au Perez ambaye klabu yake, inadhaminiwa na Kilimanjaro Beer, alisema kwamba anashukuru kwa fedha hizo na akawataka wanachama wote hai wa Simba kuhudhuria mkutano huo siku hiyo kujadili maendeleo ya klabu.
    Kaburu alisema kwamba, katika siku hiyo ya Mkutano watazindua Wiki ya Simba SC na jamii, ambayo itahusu wachezaji, viongozi na walimu wa timu hiyo kufanya ziara sehemu mbalimbali za kijamii, kama hospitali, vituo vya watoto wa yatima, shule za msingi na kiwanda cha TBL, wadhamini wao wakuu.
    Kaburu pia alikumbushia kuhusu tamasha la kila mwaka la Simba SC, Simba Day, ambalo na mwaka huu tena litafanyika Agosti 8, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. “Maandalizi ya Simba Day yamekwishaanza na yanaendelea vizuri na kwa sasa kocha yupo kwenye harakati za kuboresha timu,”alisema Kaburu.
    Kwa upande wake, Kavishe aliahidi siku ya Simba Day wataikabidhi Simba SC basi lake jipya kubwa, ambalo kwa sasa lipo kwenye hatua za mwishoni za matengenezo.

    RATIBA YA WIKI YA SIMBA NA JAMII:
    Agosti 5, 2012: Mkutano Mkuu wa mwaka Simba SC (Polisi Oystrebay)
    Agosti 6, 2012: Kutembelea watoto yatima Maungu Orphanage Center, K’ndoni Mkwajuni
    Agosti 7, 2012: Kutembelea wagonjwa Mwananyamala hospitali
    Agosti 8, 2012: Simba Day (Uwanja wa Taifa, burudani na mechi)
    Agosti 9, 2012: Kutembelea shule ya msingi Mgulani kuhamasisha michezo mashuleni
    Agosti 10, 2012: Kutembelea kiwanda cha TBL Ilala.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MKUU MKUU SIMBA SC, WANACHAMA WAKUMBUSHWA KULIPIA KADI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top