• HABARI MPYA

    Friday, July 27, 2012

    NGASSA ASEMA YEYE NA YANGA HAWATUPANI


    Mrisho Ngassa

    Na Prince Akbar
    MRISHO Khalfan Ngassa, amesema kwamba alikwenda kushangilia bao la ushindi aliloifungia Azam FC na mashabiki wa Yanga jana, kwa sababu muda wote wameendelea kumuunga mkono japo aliondoka kwenye timu yao miaka miwili iliyopita.
    “Najua watu wanaweza kuleta tafsiri nyingi, lakini jibu ninalo mimi. Mara nyingi mchezaji nyota anapoondoka kwenye timu, mashabiki humchukia, lakini utaona mimi na mashabiki wa Yanga hakuna kitu hicho.
    Wameendelea kuniunga mkono siku zote hata nikiwa na jezi ya Azam, kwangu ni jambo la kujivunia na niliona njia pekee ya kuwalipa fadhila ni ile,”alisema Ngassa.
    Alipoulizwa kuhusu fainali, ambayo itamkutanisha na timu yake ya zamani, Yanga, Ngassa alisema kwamba itakuwa mechi bora na kali, kwa sababu timu zote zimeonyesha zina uwezo mkubwa.
    “Kama kuna mtu alikuwa hajaamini, basi leo (jana) amejiridhisha kwamba Yanga na Azam ni timu nzuri na zote zilistahili kucheza fainali. Sasa hakuna haja ya kuzungumza mengi, mpira unachezwa uwanjani, tusubiri hiyo Jumamosi tukamalize kazi. Kama nitapewa nafasi, nitacheza kwa uwezo wangu wote niisaidie timu yangu kutwaa taji hili.
    Nina kiu ya mataji, nimeshinda Ligi Kuu, nimeshinda Kombe la Challenge, lakini sijawahi kushinda Kombe hili, baba yangu alishinda taji hili (Khalfan Ngassa mwaka 1991 akiwa na Simba SC), nami nitafurahi nikishinda Kombe hili,”alisema Ngassa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NGASSA ASEMA YEYE NA YANGA HAWATUPANI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top